Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » LISSU ALITIKISA TENA BUNGE

LISSU ALITIKISA TENA BUNGE

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

KWA mara nyingine tangu kuanza mjadala wa kujadili sura ya kwanza na ya sita ya Rasimu ya Katiba kuhusu muundo wa Serikali, Mjumbe Maalum wa Bunge la Katiba, Tundu Lissu, ameendelea kutikisa Bunge hilo kutokana na hoja kuhusiana na uhalali wa Muungano.
Mbunge huyo alienda mbali zaidi na kusema kuwa hati za Muungano ambazo Serikali imeonesha saini za Abeid Aman Karume, zimeghushiwa na kutaka hati hiyo ipelekwe bungeni ili wabunge walinganishe saini hizo.
Lissu alitoa kauli hiyo mjini Dodoma wakati akichangia mjadala kuhusu sura ya kwanza na ya sita ya rasimu ya Katiba. Lissu alianza kuchangia akisema;
"Acha nijibu vioja kuwa Tundu Lissu amemtukana Baba wa Taifa, sasa mwaka 1995 Baba wa Taifa alihutubia mkutano wa Mei Mosi mkoani Mbeya na baadaye aliandika kitabu chake alichokiita 'TUJISAHIHISHE' na katika kijitabu chake alisema asiyekubali kukosolewa hawezi kuwa kiongozi bora."
"Baba wa Taifa aliyekuwa Mwenyekiti na mwanzilishi wa CCM alisema CCM si mama yangu hivyo Baba wa Taifa alikuwa binadamu, hakuwa Mungu hakuwa malaika na hajawa mtakatifu bado kwa hiyo tunaposema makosa yake tunathibitisha ubinadamu wake na Baba wa Taifa mwenyewe angekuwa wa kwanza kukubali kuwa alikuwa binadamu na si Mungu na kama binadamu alikuwa anakosea."
Alisema kwa wasiofahamu Baba wa Taifa aliwahi kuunga mkono vita ya Jamhuri ya Biafra iliyokuwa inataka kujitenga na Nigeria alikosea hakuwa Mungu; "Tunaposema alikosea hatumdhalilishi bali tunathibitisha ubinadamu wake," alisema.
Alisema, “kuna watu ambao wako humu ndani bungeni wakati wa uhai wake walikimbia chama chake na kujiunga na chama cha NCCR-Mageuzi na wakasubiri Mwalimu amefariki wamerudi CCM na leo hii ndiyo wanaojifanya kuwa watetezi wakubwa wa Baba wa Taifa.”
HATI ZA MUUNGANO
Akizungumzia hati za Muungano, Lissu alisema; "Kioja cha pili ni kuhusu hati ya makubaliano ya Muungano kuwa ipo au haipo kwani tumeoneshwa kitu hivi na kuna sahihi kwenye mitandao mlinganishe sahihi ya Sheikh Karume iliyoko kwenye hati ya Muungano katika sheria ya mabadiliko ya kwanza ya Katiba ya mpito ya mwaka 1965.
"Leteni hiyo hati mnayodai kuwa ina saini ya Karume tuwaoneshe hapa mlivyo waongo na kama hati hiyo ni halali iliwahi kutungiwa sheria ya kuithibitisha Zanzibar?
“Je na hiyo sheria ipo wapi na kwa mujibu wa Profesa Shivji kuwa Zanzibar haijawahi kuridhia Muungano hadi kesho kutwa, hivyo basi kama masharti hayakutimizwa kwa miaka 50 hiyo hati si halali."
Alisema hoja za msingi kwa mahali tulipofikia sasa kikatiba na kisiasa na kwa mujibu wa Dkt. Mwakyembe aliwahi kuandika kwenye kitabu chake kuwa muundo wa shirikisho wa Serikali tatu kama ilivyopendekezwa na Tume ya Jaji Nyalali, Kisanga, Warioba na wananchi ndiyo njia pekee ya kutatua matatizo ya Muungano.
"Nathibitisha ukweli wa maneno ya Dkt. Mwakyembe kwa katiba zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ile Katiba ya Zanzibar ambazo ni halali na ukisoma kama utaona kama vile unasoma katiba za nchi mbili tofauti kumbe ni nchi moja," alisema Tundu Lissu.
Alisema Rais Kikwete sio Mkuu wa nchi ya Zanzibar kwa Ibara ya 26 (1) ya Katiba ya Zanzibar inasema; "Rais wa Zanzibar atakuwa Mkuu wa nchi ya Zanzibar, hivyo Rais Kikwete si Amiri Jeshi Mkuu wa Zanzibar na ibara ya 123 ya katiba hiyo inasema Rais wa Zanzibar ndiye Amiri Jeshi Mkuu wa Vikosi vya ulinzi maana yake ni jeshi, hivyo tayari tuna nchi mbili tofauti," alisema Lissu.
Alisema Ibara ya 9 inasema kutakuwa na Mzanzibar yaani inazungumzia Mzanzibar na si Mtanzania; "Hivyo hakuna ambaye atasimama hapa na kusema sisi ni nchi moja... nani anayeweza kumbishia Dkt. Mwakyembe kuwa suluhisho la tatizo la Muungano ni Serikali tatu?" Alihoji Lissu.
Alisema hata kiprotokali Rais Kikwete, anapokuwa kwenye sherehe za Mapinduzi anapanga foleni kule Zanzibar na anayepigiwa mizinga 21 ni Dkt. Shein.
"Hauwezi kuwa na wakuu wa nchi wawili mmoja anaishi Magogoni na mwingine Mnazi Mmoja wakipishana kauli hali itakuwaje," alihoji Lissu.
Alisema baada ya miaka 50 tutengeneze utaratibu mpya na bila kuchukua hatua za haraka mbele ni giza na watakaoleta vita si wale wanaotaka kufanya marekebisho bali ni wale wanaofumbia macho wanaokwenda kuangukia kwenye vitindi virefu.
Kwa upande wake mjumbe mwingine wa Bunge hilo Maalum Bernad Membe, alisema yeye anaunga mkono msimamo wa chama chake wa kutetea Serikali mbili.
Alimshukia, Lissu akisema hakuna nchi yoyote duniani inayotukana viongozi wake na Bunge litakuwa la mwisho kufanya dhihaka kwa viongozi na waasisi wa Taifa hili wanaheshimika duniani kote.
Kuhusu hati ya Muungano, Membe alisema ameiona ni halali na ndio iliyokwenda Umoja wa Mataifa. Alisema Tume ya Jaji Warioba itakuja kulaaniwa kwa mauaji yatakayotokea kutokana na kubariki muundo wa Serikali tatu.
"Bunge hili litakuja kulaaniwa kwa kubariki mauaji," alisema Membe. Naye Mjumbe wa Bunge hilo, Zitto Kabwe, alisema Muungano ni imani hivyo muundo wowote wa Muungano unavunja Muungano kama hakuna mwafaka utavunjika.
"Tuwe wa Serikali mbili au moja au tatu kama hakuna mwafaka lazima utavunjika tu na mfano mzuri ni wa Serikali ya shirikisho ya Somalia, Ethiopia na Malaysia zilivunjika," alisema.
"Mchakato huu ulipaswa kutengeneza maridhiano katika nchi yetu, unajenga chuki, kutengana na majibizano ambayo wananchi huko nje wanatushangaa sana na tumesikia lugha kali sana za kibaguzi humu ndani na hakuna juhudi zozote kutoka kwa viongozi wetu kukemea ubaguzi hakuna sumu mbaya katika nchi zozote duniani kama ubaguzi" alisema Kabwe.
Alisema kauli za vitisho na kibaguzi zinatoka huku watu wanashangilia, lakini pia wanashangilia matusi ya kupandikiza chuki... hatuwezi kujenga nchi kwa mtindo huo, hivyo watu wajadiliane kwa hoja na watu wenye hoja zao watoe hoja zao na baadaye tukubaliane na tuamue.
Alisema kuna baadhi ya wajumbe wanazungumzia gharama kwa Serikali tatu zitakuwa kubwa, lakini hakuna hadi sasa utafiti wowote wa kitaalam ambao unathibitisha hilo na baadhi ya wachumi wameshindwa kuithibitisha.
Alisema kinachofanyika ni kuondoa mambo yale ya kidola unaweka pembeni na tutaweza kuwa na Rais mmoja, lakini wakuu wa Serikali ni wawili katika nchi moja ni jambo la Makubaliano kwani hatuhitaji kujenga Ikulu mpya.

"Chanzo:Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa