Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » VIGOGO SUMA JKT HURU

VIGOGO SUMA JKT HURU

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imewaachia huru vigogo saba wa Shirika la Uchumi la Jeshi la Kujenga Taifa (Suma JKT) baada ya kuwaona hawana hatia katika mashtaka saba yaliyokuwa yakiwakabili ya kula njama na matumizi mabaya ya madaraka.
Vigogo walioachiwa huru jana na Hakimu Mkazi, Aloyce Katemana ni Kanali Ayoub Mwakang’ata, Luteni Kanali Mkohi Kichogo, Luteni Kanali Paul Mayavi, Meja Peter Lushika, Sajenti John Lazier, Meja Yohana Nyuchi na Mkurugenzi wa Miradi ya Matrekta, Luteni Kanali Felix Samillan.
Akisoma hukumu hiyo jana, Hakimu Katemana alisema amepitia ushahidi uliotolewa na mashahidi 10 wa upande wa mashtaka, vielelezo 25 vya ushahidi walivyoviwasilisha na ushahidi wa upande wa utetezi ulitolewa na washtakiwa, mashahidi wao tisa pamoja na vielelezo vitano na kwamba hakuna ubishi kuwa washtakiwa hao walikuwa wajumbe wa bodi ya Suma JKT pia wakurugenzi wa Bodi ya Takopa na watia saini wa kampuni hiyo walihamisha Sh3.8 bilioni kutoka Takopa kwenda Suma JKT kwa kufuata taratibu zote zilizowekwa na wanahisa hao kupitia nafasi zao.
“Hili shtaka la matumizi mabaya ya madaraka ni lazima lionyeshe lengo la kujipatia faida au manufaa, si tu kutekeleza sheria, kwa maana hiyo Mahakama hii kwa kulinganisha ushahidi uliotolewa na mashahidi wa upande wa mashtaka na utetezi, unathibitisha mashtaka yao hayawezi kusimama,” alisema Hakimu Katemana.
“Kwa kuwa walitekeleza majukumu yao kama watia saini wa Kampuni ya Takopa licha ya kuwa ni wajumbe wa bodi ya Suma JKT na hakuna kinachoonyesha kuwa walipata manufaa ya aina yoyote ile, hawana hatia na Mahakama inawaachia huru.
Julai 2, 2012, Mawakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Dominsian Kessy na Ben Lincoln waliwafikisha washtakiwa hao mahakamani kwa mara ya kwanza wakidaiwa kutenda makosa hayo.
Walidaiwa kutumia vibaya madaraka yao kinyume na Kifungu cha 31 cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ya 2007.
Wakili Kessy alidai kuwa Machi 5, 2009 katika chumba cha mikutano cha Ofisi ya Suma – JKT, wakiwa wajumbe wa Bodi ya Tenda ya shirika hilo, kwa makusudi walitumia madaraka yao vibaya kwa kutoa uamuzi wa bodi hiyo ambao ulionyesha kuwa umetolewa na Takopa kwa madhumuni ya kununua magari na vifaa vya ujenzi bila kupata idhini ya kutoka Bodi ya ya Wakurugenzi ya Takopa.
Alidai kuwa Machi 12, 2012 washtakiwa hao walitumia vibaya madaraka kwa kupitishia maazimio ya kununuliwa kwa magari na vifaa vya ujenzi ambavyo vilikuwa vimeshatumika kinyume na Kifungu cha 58( 3) cha Sheria ya Ununuzi wa Umma ya mwaka 2005.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa