Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » MFUKO MAALUMU MKOPO WA WASTAAFU WAZINDULIWA

MFUKO MAALUMU MKOPO WA WASTAAFU WAZINDULIWA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

BENKI ya Posta Tanzania (TPB) kwa kushirikiana na mfuko wa pensheni wa LAPF wamezindua mpango maalum wa kutoa mikopo kwa wanachama wastaafu wa mfuko huo.

Akizungumza Dar es Salaam jana Waziri wa kazi Ajira na Vijana Gaudensia Kabaka mara baada ya uzinduzi huo, alisema lengo ni kuwasaidia wastaafu katika kukidhi mahitaji yao na maslahi yao kwa ujumla.

Alisema upatikanaji wa fedha hizo kwa wastaafu utawawezesha kumudu gharama za mahitaji muhimu ya muda mfupi na mrefu ambayo ni endelevu kama tafiti mbalimbali zinavyoonesha kwa wastaafu waliotangulia.

"Napenda kuwasisitiza wastaafu wenye sifa za kuomba mikopo hii wajitokeze kwa wingi kutumia fursa hii kujiendeleza kimaisha hivyo mikopo hii ikitumika vizuri itakuwa ndiyo chachu ya maendeleo kwa wastaafu kuishi maisha ya faraja,"alisema Kabaka.

Aliwataka wastaafu kukopa kwa sababu maalum ili kuepuka matumizi mabaya ambayo yatapelekea kuwa na uwezekano wa msongo wa mawazo.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa (TPB) Sabasaba Moshingi,alisema lengo ni kuwezesha wastaafu kukidhi mahitaji halisi ya fedha na hatimaye kuboresha maisha yao.

Alisema miongoni mwa mahitaji makubwa ya fedha kwa wastaafu ni pamoja na gharama za matibabu, ada za shule, kuendesha biashara na miradi mbalimbali.

Pia alisema kwa muda mrefu taasisi mbalimbali zimekuwa hazitoi mikopo kwa wastaafu wakidhani hawana uwezo wa kulipa na kujenga dhana ya kutokopesheka.

"Kwa kuliona hili na kutambua mchango wa wastaafu TPB kwa kushirikiana na LAPF wamebuni mpango huu wa kipekee nchini wa kuwakopesha wastaafu wa mfuko huo,"alisema Moshingi.

Hata hivyo alizitaka taasisi nyingine za fedha kuangalia namna ya kuweka mipango ya kusaidia wastaafu hapa nchini ambao kwa ujumla wana kiasi kikubwa cha fedha ambacho kikitumiwa vyema kinaweza kuleta mchango mkubwa katika uchumi wa nchi.

Alisema mstaafu anayetaka mkopo hatahitaji kuwa na dhamana na riba inayotozwa kwa mkopo mdogo ukilinganishwa na mikopo mingine.

Alisema mkopo huo umewekewa bima hivyo endapo mkopaji atafariki familia yake haitaendelea kudaiwa, hivyo wastaafu wa LAPF wanaweza kupata mikopo ambayo marejesho yake ni kati ya mwaka mmoja hadi miaka mitatu.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa