Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » PROFESA LIPUMBA ASIMAMISHA BUNGE

PROFESA LIPUMBA ASIMAMISHA BUNGE


Kukamatwa na kudhalilishwa kwa Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Prof. Ibrahim Lipumba na wafuasi wengine wa chama hicho jana, kulisababisha Spika wa Bunge, Anne Makinda, kulazimika kusitisha shughuli za Bunge.
 
Hatua hiyo ilifikiwa na Makinda baada ya wabunge wote wa upinzani kusimama bungeni na kugoma kukaa chini ili kuruhusu shughuli za Bunge za jana asubuhi kufanyika.
 
Shughuli hizo ni pamoja na taarifa za Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) na Kamati ya Bunge ya Bajeti.
 
Taarifa hizo zilipangwa kuwasilishwa katika kikao cha Bunge cha jana asubuhi kabla ya wabunge kupewa fursa ya kuzijadili.
 
Wabunge wa upinzani walfikia hatua hiyo wakipinga mwongozo uliotolewa na Makinda dhidi ya hoja iliyowasilishwa na Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia, ambaye alitaka Bunge lisitishe shughuli zake za jana ili kujadili kwa dharura suala la kudhalilishwa kwa Lipumba na wafuasi wengine wa CUF.
 
Mbatia aliomba mwongozo huo baada ya kipindi cha maswali na majibu kumalizika bungeni.
 
Alipopewa nafasi, alitoa hoja ya kulitaka Bunge lijadili kwa dharura suala la Jeshi la Polisi kumkamata, kumpiga na kumdhalilisha Prof. Lipumba na wananchi wengine waliopigwa mabomu ya machozi na jeshi hilo.
 
Mbatia alisema kitendo hicho kinahatarisha amani ya Taifa kwa kuwa Prof. Lipumba ni mwenyekiti wa chama, ambacho kina wabunge wengi ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na pia ni mwenyekiti wa chama kinachounda Serikali ya Umoja wa Kitaifa visiwani Zanzibar.
 
Alisema Jeshi la Polisi wakati likitekeleza suala hilo lilisema kuwa limepata maagizo kutoka juu, hivyo akataka suala hilo lijadiliwe ili ijulikane kuwa uko juu, ambako agizo lilitoka ni wapi.
 
“Hili Jeshi la Polisi lilisema kuwa limepata maagizo kutoka juu, nadhani tunahitaji kujua huko juu, ambako agizo hilo lilitoka kwa nani na kwa lengo gani?” alihoji Mbatia.
 
Alisema matukio ya Jeshi la Polisi kupokea maagizo ya kuvunja amani na kuyatekeleza yanahatarisha amani ya nchi na kwamba, suala hilo lisiposhughulikiwa mapema, linaweza kusababisha madhara makubwa kwa taifa.
 
“Mheshimiwa Spika, tusipoziba ufa, utajenga ukuta. Mwaka juzi waandishi wa habari waliuawa, matukio ya aina hii yanaendelea na yana madhara makubwa. Natoa hoja Bunge lako Tukufu liahirishe shughuli zake za leo ili tujadili suala hili kwa uzito wake,” alisema Mbatia.
 
Baada ya kutoa hoja hyo, wabunge wote kutoka vyama vya upinzani walisimama kuasharia kuiunga mkono.
 
Hata hivyo, Spika Makinda alisimama na kusema kwa mujibu wa kanuni, hoja za aina hiyo, huwa haziungwi mkono.
 
Alisema badala yake, kanuni inaelekeza kuwa Spika ataangalia mazingira na uzito wa hoja kwa kadri anavyoona inafaa na kuamua ijadiliwe au isijadiliwe bungeni.
 
Hata hivyo, alisema hoja hiyo ni kubwa na nzito, hivyo akaitaka serikali itoe kauli kabla ya Bunge kuanza kuijadili na kutoa uamuzi leo.
 
Makinda aliwaomba wabunge kuendelea na shughuli za Bunge za siku ya jana ili kutoa nafasi kwa serikali kujiandaa kulitolea kauli suala hilo bungeni.
 
Hata hivyo, mwongozo huo wa Spika Makinda ulipingwa na wabunge wa upinzani na kuzua tafrani bungeni.
 
“Kwa mazingira haya naagiza serikali kesho (leo) itoe kauli na ndipo turuhusu mjadala,” alisema Makinda.
 
Baada ya kutolewa kwa mwongozo huo, wabunge wote wa upinzani walisimama kuupinga, jambo lililomfanya Makinda kuketi kwenye kiti chake kwa zaidi ya dakika tano, kupisha malumbano yasiyo rasmi baina ya wabunge wa upinzani na wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).
 
Katika kujaribu kuwatuliza, Makinda alisikika akiwaeleza wabunge hao kuwa mwongozo alioutoa ni sahihi na unazingatia kanuni, hivyo kama hawaridhiki wanaweza kufanya kile walichokusudia.
 
“Kama mnataka kufanya mnachotaka kufanya fanyeni, lazima tutumie busara, kama mnataka kutoka tokeni, lakini huo siyo mtindo wa kufuata kanuni,” alisema Makinda huku akimwita Katibu aendelee na shughuli inayofuata.
 
Hata hivyo, wabunge wote wa vyama vya upinzani waliendelea kusimama, huku wakipiga kelele za kupinga mwongozo uliotolewa, wakishinikiza suala hilo lijadiliwe wakati huo.
 
Jitihada za Spika Makinda kuwataka wabunge hao kukaa kwenye viti vyao, ziligonga mwamba.
 
Hali hiyo ndiyo iliyomlazimisha kuahirisha kikao cha Bunge cha jana asubuhi hadi  jioni. Hata hivyo, jioni Spika aliliahirisha tena Bunge hadi leo.
 
NJE YA BUNGE
Nje ya Bunge, baadhi ya wabunge walitoa maoni kuhusiana na tukio hilo.
 
Wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) walidai kuwa wenzao wa upinzani wamekosa uvumilivu na wameonyesha utovu wa nidhamu, huku wabunge wa upinzani wakiunga mkono hatua hiyo.
 
Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nasari, alisema kuwa wanapuuza suala hilo kwa sababu wameshaona kuwa ni sahihi wapinzani kuonewa, kupigwa na kunyanyaswa, hivyo suala hilo ni kama haliwagusi.
 
“Sisi wapinzani kila wakati tumekuwa tukinyanyaswa na kupigwa, mimi mwenyewe wananiandama kila wakati, katika mazingira kama haya siwezi kuona suala hili likianza kupigwa danadana, tunajua hiyo ni janja yao ya kutaka wajipange namna ya kuzima hoja yetu,” alisema Nasari.
 
Alisema wamegundua kuwa lengo la Spika ni kuchelewesha mjadala wa suala hilo ili Prof. Lipumba afikishwe mahamani na baadaye wazuie suala hilo kujadiliwa kwa madai ya kuingilia muhimili wa Mahakama.
 
Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba, alisema kitendo cha wabunge wa upinzani kutotii maagizo ya Spika siyo cha kiungwana na kwa kufanya hivyo wameliingiza taifa hasara.
 
Alisema wabunge wote tayari walikuwa wamelipwa kwa ajili ya kufanya kazi za kibunge za jana, hivyo kitendo chao cha kugomea maelekezo ya Spika na kusababisha Bunge kuahirishwa kinamaanisha kuwa fedha walizolipwa zimepotea kwa kuwa hawakufanya kazi iliyokusudiwa.
 
“Ingawa unaweza usiione hasara hii moja kwa moja au ukaona kama wamefanya kazi nusu siku, lakini ikitokea kazi, ambazo zilipaswa kufanyika leo zikapangiwa siku nyingine, maana yake ni kwamba, lazima walipwe fedha nyingine kwa ajili ya siku hiyo kwa kazi, ambazo zingepaswa kufanywa leo, hii ni hasara kubwa kwa taifa,” alisema Mwigulu.
 
Hata hivyo, Mwigulu aliungana na wabunge hao kwa kukiri kuwa kitendo alichofanyiwa Prof. Lipumba cha kupigwa na kukamatwa na Jeshi la Polisi siyo cha kiungwana na wabunge hao wako sahihi kuhoji suala hilo.
 
Alisema kosa la wabunge hao ni kutotii maelekezo ya Spika na kwamba kitendo hicho ni utovu wa nidhamu, ambao kama utaendekezwa itakuwa vigumu kuendelea kuliongoza Bunge katika njia iliyo sahihi.
 
Alisema licha ya wabunge hao kusababisha shughuli za leo kusitishwa, bado hoja hiyo itajadiliwa leo kama ambavyo Spika alielekeza na hivyo walichofanikiwa ni kuliingiza taifa hasara kwa kuzuia shughuli za Bunge za jana asubuhi kufanyika.
 
Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Ester Bulaya, alisema wabunge wa upinzani licha ya kuwa na hoja yenye mashiko, wamekosea kutotii maelekezo ya Spika.
 
Alisema kitendo cha wabunge hao kinapanda mbegu mbaya kwa kizazi cha Kitanzania, ambacho kinaweza kuanza kuiga tabia mbaya ya kuwagomea viongozi wao.
 
 Mbunge wa Ileje (CCM), Aliko Kibona, alisema Watanzania wameridhia utawala wa sheria, hivyo polisi kama wataendelea na vitendo vyao hivyo, watashindwa kufanya kazi.
 
Hata hivyo, alisema mwongozo uliotolewa na Spika alitegemea kuwa wabunge wangevuta subira.
 
Hata hivyo, Mbatia aliwaambia waandishi wa habari katika viwanja vya Bunge baada ya Bunge kusitishwa jana asubuhi kuwa hawawezi kusubiri kama hadi leo kama alivyoamua Spika.
 
Alisema hiyo inatokana na kwamba, iwapo Prof. Lipumba na wafuasi wengine wa CUF waliokamatwa watafikishwa mahakamani, inaweza kujengwa hoja bungeni kwamba, kadhia hiyo isijadiliwe kwa kuwa suala hilo liko mahakamani.
 
Juzi Jeshi la Polisi lilitumia nguvu kuwatawanya wafuasi wa CUF kwa kurusha mabomu, risasi za moto na maji ya kuwasha na kumkamata Prof. Lipumba na wafuasi wengine 32.
 
Nguvu hiyo ya polisi ilitumika wakati wa kuzuia msafara wa Prof. Lipumba kuelekea eneo la Zakhem, Mbagala, kulikokuwa kumeandaliwa mkutano wa hadhara, kutoa taarifa kwa wafuasi waliokuwa wamekusanyika kuwa mkutano na maandamano yamezuiliwa na polisi.
 
CHANZO: NIPASHE
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa