Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » WANANCHI WAHIMIZWA KUJITOKEZA KWA WINGI KUPIMA AFYA ZAO KUELEKEA DESEMBA MOSI, 2015.‏

WANANCHI WAHIMIZWA KUJITOKEZA KWA WINGI KUPIMA AFYA ZAO KUELEKEA DESEMBA MOSI, 2015.‏

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Wito umetolewa kwa wananchi kote nchini kuyatumia maadhimisho ya Siku ya UKIMWI duniani ambayo huadhimishwa kila ifikapo Desemba 1 ya kila mwaka kupima afya zao ili kudhibiti maambukizi mapya ya VVU.

Akizungumza na waandishi wa Habari leo jijini Dar es salaam Mwenyekiti Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Kudhibiti UKIMWI nchini Tanzania Dkt. Fatma Mrisho amesema  Siku ya Ukimwi Duniani nchini itaadhimishwa kwa  kuwahimiza wananchi kujitokeza kwa wingi  kupima afya zao na kupata elimu ya kujikinga  na maambukizi ya ugonjwa huo.

Ameeleza kuwa  maadhimisho ya mwaka huu yataambatana na shughuli mbalimbali zikiwemo za Utoaji wa Elimu ya Afya na Upimaji wa hiari wa VVU katika maeneo mbalimbali kote nchini kupitia vituo vitakavyowekwa, Kufungua kituo cha maarifa cha udhibiti UKIMWI eneo la Manyoni mkoani Singida ambayo ni njia kuu kuelekea mikoa ya Kanda ya Ziwa na nchi za Jirani za Burundi na Rwanda.

Ameongeza kuwa Tume kwa kushirikiana na wadau mbalimbali itaendesha mikutano ya kitaalam kuhusu UKIMWI, Zoezi la upimaji wa hiari wa VVU kwa wananchi, Kupokea tamko litakalotolewa na Baraza la Watu wanaoishi na VVU pamoja na Uzinduzi wa taarifa ya tathmini ya Sheria zinazotumika  zinazohitaji kurekebishwa zinazozuia malengo ya sifuri 3.

 Aidha Tume itapokea taarifa ya hali ya maambukizi ya VVU duniani itakayotolewa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon kuhusu dunia na mapambano dhidi ya VVU.

Dkt. Fatma amefafanua kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho hayo anatarajiwa kuwa  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ambapo pamoja na mambo mengine atazindua Mfuko wa UKIMWI ambao utakuwa chachu ya kupunguza maambukizi ya VVU nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa ufuatiliaji na tathmini kuhusu UKIMWI wa TACAIDS Dkt.Jerome Kamwela amesema kuwa kiwango cha maambukizi ya UKIMWI kwa mujibu wa takwimu za mwaka 2011/2012 kimepungua na kufikia asilimia 5.3 huku mikoa ya nyanda za juu kusini ya Njombe, Iringa  na Mbeya ikiongoza kwa kuwa na maambukizi zaidi  na mikoa ya Manyara, Tanga na Lindi  ikiwa na maambukizi ya chini ya asilimia mbili.

Dkt. Kamwela amesema kuwa maambukizi ya VVU ni mengi hasa kwa kundi la watu wenye umri wa miaka 19-24 huku makundi ya wanaojidunga, wanaume wanaofanya mapenzi ya jinsia moja, wanawake wanaofanya biashara ya ngono yakiendelea kuwa katika hatari ya kuathiriwa zaidi na maambukizi ya VVU.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa