Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » MEYA KINONDONI AVALIA NJUGA SAKATA SHAMBA LA SUMAYE

MEYA KINONDONI AVALIA NJUGA SAKATA SHAMBA LA SUMAYE

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Meya wa Manispaa ya Kinondoni, Boniface Jacob.
Meya wa Manispaa ya Kinondoni, Boniface Jacob, amesema hawatakubali kuona Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye, anaonewa, kunyanyaswa na kudhalilishwa kwa kutumia mwavuli wa wavamizi wa ardhi huku kukiwa na siasa ndani yake.
 
Akizungumza na waandishi wa habari jana ofisini kwake jijini Dar es Salaam, alisema kinachoendelea katika shamba la Sumaye ni kutengeneza wavamizi na kwenda kuzungumza nao kuonyesha kuwa suala hilo linashughulikiwa kwa mujibu wa taratibu.
 
“Hakuna mahali kokote unaweza kuendesha kesi baina ya wavamizi na mmiliki halali, mwenye mamlaka na ardhi ni Baraza la Madiwani, vyombo vingine ni kulinda amani na mmiliki halali anajulikana, tunachokiona kwa sasa ni kutengeneza jambo na kutafuta ‘kiki’ ya kisiasa,” alisema na kuongeza:
 
“Kama inafanyika hivi, watambue kuwa nasi tunawafahamu vigogo wa CCM walioshikilia maeneo makubwa na hawajaendelezwa, na pembeni ya eneo la Sumaye kuna eneo la Chuo cha IFM  hilo halijavamiwa...sitakubali kuona mwananchi wangu au kada wetu ananyanyaswa, tutamtetea kwa mujibu wa sheria.”
 
Alisema manispaa hiyo iliwahi kuendesha operesheni ya kubomoa nyumba za wavamizi 350 kwa kushirikiana na aliyekuwa Mkuu wa Wilaya, Jordan Rugimbana, lakini kwa uongozi wa wilaya wa sasa, wavamazi wanatambuliwa na kusikilizwa.
 
“Wakati wa kampeni za uchaguzi mwaka jana kulikuwa na vitisho kwa madaka wa CCM waliohama chama, kinachoonekana ni utekelezaji wa uonevu. Hawana mamlaka ya kujadili suala hilo, ni siasa zenye lengo la kumnyanyasa kada wetu, wamefanya kosa la jinai, lazima wachukuliwe hatua na siyo kuwekwa kikao,”alisisitiza.
 
Alisema uvamizi wa ardhi umekithiri katika Kata za Bunju, Wazo, Mabwepande, Bweni na Kawe.
 
Alisema inashangaza kuona makada wa CCM wanalibeba suala hilo kwa mwavuli wa serikali huku ndani yake wakifanya siasa na kutafuta umaarufu na kwamba uonevu na unyanyasaji wowote haukubaliki katika manispaa hiyo.
 
Shamba la Sumaye lenye ukubwa kwa heka 33 lilivamiwa mwishoni mwa mwaka jana, na watu ambao walijigawia viwanja na kuanza ujenzi.
 
Hivi karibuni, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda, alitembelea shamba hilo akiwa na Sumaye na polisi na kuwataka wavamizi hao kusitisha ujenzi huo haraka hadi watakapokagua vibali vya umiliki wake.
 
Katika hatua nyingine alisema mipango aliyoanza nayo kuwa ni kusafisha jiji kwa kununua magari 40 ya kuzoa taka na ya kuzishindilia na kwamba baada ya mwaka mmoja tani 2,026 za taka zinazozalishwa kila siku zitazolewa.
 
Kuhusu makusanyo ya mapato alisema atahakikisha yanafika Sh. bilioni 100 kutoka Sh. bilioni 51 za mwaka 2015/16.
 
Aidha, alisema Manispaa hiyo haitafanya kazi na wakandarasi walioshindwa kutekeleza ujenzi wa miundombinu kwa viwango na kwamba wataandika barua kwenda kwa mammlaka zote kuhakikisha hawapewi kazi kwingine baada ya kuharibu.
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa