NA MWANDISHI WETU, Dar es Salaam
KIJANA Juma Neti anayedaiwa kumweka rehani mdogo wake, Adamu Akida,
kwa maharamia wa dawa za kulevya nchini Pakistan, ametoroka nchini na
kukimbilia Afrika Kusini.
Taarifa za uhakika ambazo MTANZANIA inazo kutoka kwa mtu wa karibu wa
Neti, zimeeleza kuwa alitoroka usiku wa Julai 19 mwaka huu kwa kutumia
gari binafsi hadi Kenya ambako alipanda ndege kwenda Afrika Kusini.
Neti anadaiwa alitoroka nchini ikiwa ni siku moja kabla ya polisi na
vyombo vingine vya usalama kuvamia nyumbani kwake Kunduchi Ununio
wilayani Kinondoni Dar es Salaam juzi, kwa ajili ya kutaka kumkamata.
Chanzo hicho kilisema polsi waliambulia patupu kwa vile tayari Neti alikuwa ameondoka siku moja kabla.
Kwa mujibu wa chanzo hicho, kabla ya kutoroka, Neti alionekana akiwa
na mshirika wake wa biashara (jina linahifadhiwa kwa sasa) ambaye
humtambulisha kuwa ni ofisa masoko wa moja ya kampuni zake za ndani na
nje ya Tanzania.
Inadaiwa pia kuwa mshirika huyo ndiye msambazaji hodari wa madawa ya kulevya katika Ukanda wa Afrika Mashariki.
Taarifa zinasema kwamba watu hao kwa pamoja waliweza kutoroka kwa
kutumia gari ndogo kupitia mipaka isiyo rasmi kati ya Namanga na
Horohoro na kuingia Kenya.
Baadaye waliingia Nairobi kwa kutumia gari tofauti na walilotoka
nalo Tanzania. Jijini Nairobi walipanda ndege kupitia Uwanja wa
Kimataifa wa Jomo Kenyatta.
Mtoa taarifa huyo alieleza kuwa haikuweza kufahamika haraka ni ndege gani waliitumia kutoka Nairobi hadi Afrika Kusini.
Neti anadaiwa kumweka rehani Akida ambaye ni mtoto wa mama yake
mdogo, nchini Pakistani, kwa gharama ya Dola za Marekani 700,000 (zaidi
ya Sh bilioni 1.5) baada ya kuchukua madawa ya kulevya kutoka kwa
maharamia wanaomshikilia Mtanzania huyo.
Taarifa zinaeleza kuwa polisi wamekuwa wakimtafuta Neti kwa mda mrefu
bila mafanikio kwa tabia yake hiyo ya kujihusisha na biashara hiyo
haramu.
Inaelezwa kwamba Neti amekuwa na utajiri wa kutisha ghafla na amekuwa
miongoni mwa Watanzania wenye ukwasi mkubwa tofauti na miaka michache
iliyopita ambako alikuwa mtu wa kipato cha kawaida.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, hivi karibuni Neti aliingia ubia na
kampuni moja ya nchini China (jina halijafahamika) baada ya kuwekeza
Dola za Marekani 400,000 (zaidi ya Sh milioni 800).
Katika mlolongo huo wa matukio kuna taarifa za kuwapo mtandao mkubwa
unaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya ambao huwapeleka vijana
katika nchi zinazotengeneza dawa hizo na kuwaweka rehani.
Kwa mujibu wa mtandao huo, vijana wengi hupoteza maisha kwa kuuawa
na maharamia hao wakuu wa biashara hiyo ya ‘unga’ baada ya waliowaweka
rehani kushindwa kupeleka fedha.
Chanzo Na Mwananchi
0 comments:
Post a Comment