Na:
Lilian Lundo - MAELEZO
Serikali kupitia Wakala
ya Serikali Mtandao (eGA) imeendelea kutekeleza uunganishwaji wa mtandao wa Mawasiliano
wa Serikali ambapo mpaka sasa Taasisi 72 zimeunganishwa na mtandao huo.
Hayo yamesemwa na Meneja
wa Habari, Elimu na Mawasiliano eGA Suzan Mshakangoto alipokuwa akiongea na waandishi wa habari
kuhusu utekelezaji wa miundombinu ya Tehama inayohusisha Serikali, leo Jijini
Dar es Salaam.
Suzan amesema kuwa
Taasisi za Serikali zilizounganishwa na mtandao huo zitakuwa zinawasiliana kwa
gharama ndogo kwa kutumia simu zitakazokuwa zikitumika kama ‘extension’ ambazo
zitakuwa zinatumia internet kupitia Mkongo wa Taifa.
“Mtumishi wa Taasisi
moja katika taasisi zilizounganishwa na mtandao huo anaweza kupiga simu kwenda
taasisi nyingine ya nje ikawa kama amepiga simu ya ‘extension’ ndani ya ofisi
moja,” alifafanua Suzan.
Vile vile Taasisi za
Serikali zitapunguza gharama za kuchajiwa huduma za internet kutoka kwa watoa
huduma binafsi ambao gharama zao ziko juu ukilinganisha na huduma inayotolewa
na wakala wa Serikali.
Aidha Taasisi na
Idara zote za Serikali zitakuwa ndani ya mtandao na mtoa huduma mmoja wa huduma
za mtandao ambapo itasaidia kwenye utunzaji wa nyaraka za Serikali na kurahisha
mawasiliano ndani ya taasisi hizo.
Hivyo basi, Ofisi ya
Rais, Utumishi na Utawala Bora kwa kushirikiana na wakala imetoa mafunzo kwa
wataalamu wa TEHAMA na Makatibu Muhtasi kutoka taasisi zilizounganishwa na
mtandao huo juu ya uendeshaji na usimamizi wa mtandao wa Serikali pamoja na
matumizi ya simu zinazotumia itifaki (IP Phones).
Mpango wa Serikali ni
kuzifikia Ofisi za Mikoa na Halamashauri zote hapa nchini ili kutumia
mawasiliano ya simu za itifaki, barua pepe na mifumo ya TEHAMA katika
kubadilishana taarifa, ambapo kufikia Disemba 2016 taasisi nyingine 77 kutoka
mikoa 20 ya Tanzania Bara zitakuwa zimeunganishwa kwenye mtandao huo.
0 comments:
Post a Comment