Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » USICHOKIJUA KUHUSU MUSWADA WA SHERIA YA HUDUMA ZA HABARI.

USICHOKIJUA KUHUSU MUSWADA WA SHERIA YA HUDUMA ZA HABARI.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


Na Beatrice Lyimo-MAELEZO
Sekta ya Habari na Utangazaji ni moja ya sekta za huduma za jamii nchini inayotoa huduma ya haki ya msingi ya raia kama ilivyojieleza katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.
 
Historia inaonyesha kuwa kwa zaidi ya miaka 20 sasa wadau wa  sekta ya habari wamekuwa wakipigania kuipa heshima taaluma ya habari  na kuifanya kuheshimika kama fani nyingine nchini.

Mwezi September mwaka huu katika mkutano wa tatu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, muswada wa huduma za habari ulisomwa kwa mara ya kwanza na kutolewa fursa kwa wadau wa habari kutoa maoni ili kuuboresha zaidi.

Jumla ya taasisi 10 ziliwasilisha maoni mbalimbali kuhusu muswada huo ikiwemo Baraza la Habari Tanzania (MCT), Tanzania Citizens Information Bureau (TCIB),Chama cha Wanasheria,Sikika, taasisi ya Nola, Jukwaa la Wahariri Tanzania na  Kituo cha Sheria na Haki za binadamu Tanzania  
 
Taasisi nyingine ni Chama cha waandishi wa habari Tanzania (TAMWA),Kituo cha kutetea haki za binadamu Tanzania, Chama cha wamiliki wa Vyombo vya Habari nchini (MOAT), na taasisi ya habari ya nchi za kusini mwa Afrika tawi la Tanzania (MISA – TAN)  .
 
Aidha Asilimia 90 ya maoni yaliyowasilishwa na wadau hao yamejumuishwa katika muswada huo ili kuwezesha muswada huo kuwa na sheria inayokidhi matakwa ya wanahabari, kwa kuzingatia mapendekezo waliyoyatoa.
Akiwasilisha Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari katika Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Maendeleo ya Jamii,Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye alisema kuwa muswada huo  unalenga kuihamisha sekta ya habari kuwa taaluma kamili na kuweka masharti ya kukuza na kuimarisha taaluma na weledi.
Waziri Nape alisema muswada huo umeandaliwa kukabiliana na changamoto mbalimbali zilizopo katika tasnia ya habari nchini ambazo ni pamoja na upungufu wa sheria zinazosimamia tasnia hiyo na mabadiliko ya teknolojia ya habari.
“changamoto kubwa katika sekta hii ya  taaluma ya habari ni  kutotambulika kama taaluma kamili inayopaswa kuheshimiwa, kukosekana vyombo madhubuti na huru vya usimamizi na badala yake mambo mengi kuwa chini ya serikali moja kwa moja,”
“Sheria hii italeta mageuzi makubwa katika usimamizi wa sekta ya habari hapa nchini ambayo inakwenda kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi yetu kuifanya rasmi sekta ya habari kuwa sekta rasmi kama zilivyo sekta nyingine za uhasibu, udaktari,” alisema Waziri Nape.
Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Hassan Abbas anasema lengo la muswada huu ni kuja na sheria itakayokuza na kuimarisha taaluma na weledi katika tasnia ya habari na kuweka mfumo wa usimamizi wa huduma za habari.

Aidha Abbas anasema  muswada huo utakusudia kuiongezea nguvu tasnia ya habari ikiwemo suala zima la kuzingatia sheria na mipaka ya nchi katika utoaji wa habari na taarifa maalum za Serikali kwa umma na kuzingatia ukomo wa kimataifa.

“Azimio la Umoja wa Mataifa la mwaka 1948, pamoja na kuzungumzia kuhusu haki ya kupata taarifa lakini pia limeanisha sheria mbalimbali ambazo hazina budi kuheshimiwa, na sheria hizo ni pamoja na sheria za ulinzi na usalama” alifafanua Mkurugenzi Abbas.

Anaongeza kuwa kifungu cha 19 cha mkataba wa geneva wa mwaka 1966 pamoja na mambo mengine umeeleza kuhusu haki ya kupata habari na taarifa ingawa imeanisha wajibu hasa katika maeneo yanayohusu usalama wa taifa.

Kwa kuzingatia mkataba huo wa kimataifa sehemu ya nane Masharti ya Jumla kifungu 55 katika muswada wa huduma za habari, Waziri atakuwa na mamlaka ya kuzuia uchapishaji au utangazaji wa maudhui yanayohatarisha usalama wa Taifa au afya ya jamii.

Katika hatua hiyo Mkurugenzi Abbas alisema kuwa yapo masuala kadhaa yanayopaswa kuchuliwa hatua za haraka za maamuzi ikiwemo suala la uchochezi, uasi wa kikundi fulani cha watu kinachotaka kuigombanisha Serikali na wananchi.

 “Uchochezi ni kuhatarisha amani ya nchi, lakini mwandishi akiikosoa Serikali haitokuwa uchochezi bali kwa atakayeleta habari za uchochezi kwa maana ya uasi atatakiwa kuwajibishwa” alifafanua Mkurugenzi Abbas.

Akifafanua zaidi alisema endapo mwandishi ataandika habari za kichochezi za kuhatarisha amani ya nchi hana budi kuchukuliwa hatua na kama hajaridhika na hatua hiyo ana uwezo wa kupeleka jambo hilo katika mamlaka husika ikiwemo kupeleka Mahakamani.

Akizungumza kuhusu suala la taaluma la mwandishi wa habari katika masuala ya Elimu, Abbas anasema suala hilo halitaainishwa katika sheria bali litaainishwa katika kanuni za Bunge ili kuweza kutolewa baadhi ya marekebisho.

Abbas alisema Sheria hiyo itumika Tanzania Bara pekee, kwa kuwa suala la habari si suala la Muungano japo sekta hizi zinashirikiana kwa namna moja au nyingine.

Mbali na hayo alisema kuwa lengo la muswada huu ni kusajili vyombo vya habari vyenye mfumo wa machapisho ikiwemo magazeti, majarida na si mitandao ya kijamii kama inavyosemwa na baadhi ya watu.  
MWISHO.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa