Na: Albert Fen
Dar es Salaam
Mkuu
wa Chuo cha Takwimu Mashariki mwa Afrika (EASTC) Prof. Innocent
Ngalinda amezindua mafunzo maalumu ya Ukusanyaji Takwimu Rasmi ambayo
yalianza tarehe 17 Oktoba mwaka huu chuoni Changanyikeni jijini Dar es
Salaam.
Akizungumza leo wakati wa uzinduzi wa mafunzo hayo, Prof. Ngalinda amesema mafunzo
hayo yameandaliwa kwa nia ya kumpatia mshiriki ujuzi katika ukusanyaji
takwimu kwa ajili ya kuzichakata na kuwa takwimu rasmi.
“Washiriki
hawa watafundishwa mbinu shirikishi, utatuzi wa matatizo mbalimbali
wakati wa ukusanyaji takwimu, sensa na viwango vya tafiti mbalimbali,
utunzaji wa Vifaa vya ukusanyaji takwimu kama vile simu za mkononi na kumpyuta mpakato pamoja na kubadilisha madodoso ya kawaida na kuwa ya kisasa”, amesema Prof. Ngalinda.
Akizungumzia
malengo ya mafunzo hayo Naibu Mkuu wa Chuo, Taaluma, Utafiti na Ushauri
wa Kitaalamu wa chuoni hapo Dkt. Frank Mkumbo amesema lengo ni
kuwawezesha wakusanyaji takwimu kukusanya takwimu halisi na zenye ubora
kwa ajili ya kupanga mipango mbalimbali ya Maendeleo.
“Lengo
kuu la mafunzo haya ni kuhakikisha kuwa wakusanyaji takwimu rasmi
wanakuwa na weledi wa kutosha katika kukusanya takwimu bora na zenye
tija kwa taifa” amefafanua Dkt. Mkumbo.
Jumla
ya washiriki 110 wamejiunga na mafunzo hayo maalumu ya muda wa miezi
miwili kwa awamu ya kwanza ambayo yatamalizika mwezi Disemba, 2016 na
watakaomaliza na kufaulu watapatiwa cheti cha Ukusanyaji Takwimu. Awamu
ya pili ya mafunzo hayo yanatarajiwa kuanza Novemba mwaka huu na
kumalizika Januari, 2017.
0 comments:
Post a Comment