Na: Mwandishi wetu
Dar es Salaam.
Wadadisi au wakusanyaji taarifa za kitakwimu rasmi katika tafiti
mbalimbali zinazoratibiwa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) wametakiwa
kuwa wamehitimu Mafunzo ya Ukusanyaji Takwimu Rasmi angalau kwa ngazi ya
cheti.
Taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu
Dkt. Albina Chuwa imesema matakwa hayo ni kwa mujibu wa Sheria ya
Takwimu Na. 9 ya mwaka 2015 inayoipa mamlaka ofisi hiyo ya kuratibu na
kusimamia ukusanyaji wa Takwimu rasmi nchini.
Taarifa hiyo imefafanua kuwa utumiaji wa wadadisi ambao wamepitia
mafunzo ya ukusanyaji takwimu angalau kwa ngazi ya cheti kutasaidia
kuboresha zaidi upatikanaji wa takwimu rasmi nchini.
Aidha, taarifa hiyo imeeleza kuwa Mafunzo ya Ukusanyaji Takwimu
Rasmi yanatolewa na Chuo cha Takwimu Mashariki mwa Afrika "Eastern
Africa Statistical Training Centre (EASTC) kilichopo Changanyikeni
jijini Dar es Salaam.
Ofisi ya Taifa ya Takwimu ina jukumu la kukusanya, kuchambua na
kusambaza Takwimu Rasmi Nchini kwa mujibu wa Sheria ya Takwimu ya mwaka
2015.
0 comments:
Post a Comment