Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » WATEJA WA TIGO PESA KUVUNA BILIONI 6.04 GAWIO LA KUMI LA ROBO MWAKA

WATEJA WA TIGO PESA KUVUNA BILIONI 6.04 GAWIO LA KUMI LA ROBO MWAKA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Mkuu wa Huduma za Fedha kwa njia ya simu wa Tigo Ruan Swanepoel (kushoto), akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam leo asubuhi kuhusu, Wateja Tigo Pesa kuvuna 6.04bn/- (dola 2,763,636) gawio la kumi la robo mwaka. Kulia ni Meneja Masoko na Usambazaji Huduma za Kifedha wa Tigo, Catherine Rutenge.
Meneja Masoko na Usambazaji Huduma za Kifedha wa Tigo, Catherine Rutenge (kulia), akizungumza katika mkutano huo.
Mkutano na wanahabari ukiendelea.


Na Dotto Mwaibale

Kampuni inayoongoza kwa mtindo wa maisha ya kidijitali Tigo imetangaza  gawio jingine  la robo mwaka la shilingi bilioni 6.04 (sawa na dola za Marekani 2,763,636)  kwa watumiaji wa Tigo Pesa  ikiwa ni mara ya kumi katika mfululizo wa kampuni hiyo ya simu kugawa faida hiyo kwa watumiaji wake wa huduma ya fedha kwa njia ya simu.

Akizungumza katika mkutano wa waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo Mkuu wa Huduma za Fedha kwa njia ya simu wa Tigo Ruan Swanepoel alisema kwa ujumla  kampuni hiyo  imeshawalipa watumiaji wake wa huduma za fedha kwa njia ya simu  jumla ya shilingi bilioni 52.28 (sawa na dola za Marekani 23,763,636) ikiwa ni malipo ya  robo mwaka ya kumi  tangu  kuzinduliwa kwa huduma hiyo Julai 2014.

Hii ni mara ya tatu kwa mwaka huu kwa Tigo  kulipa  gawio kwa wateja wake.

 Swanepoel alisema kuwa katika robo ya tatu ya mwaka huu kiwango cha faida  kilipanda  na kufikia asilimia 9 ikiwa  kimepanda kwa asilimia 1 kutoka robo ya pili  ambako kumechangiwa  kwa kiwango kikubwa na kiwango kizuri cha riba katika mifuko ya dhamana  ndani ya  benki mbalimbali za biashara.

 “Faida hii ya hisa inalipwa kwa wateja binafsi, mawakala wa reja reja na washirika wengine wa kibiashara wa Tigo ambao kila mmoja anapokea malipo yake kulingana na thamani ya fedha zilizowekwa kielektroniki ndani ya pochi zao za Tigo Pesa,” alifafanua Swanepoel.

 Swanepoel  aliongeza, “Tunayofuraha kubwa kutangaza ongezeko hili la faida katika gawio la mara ya kumi mfululizo. Hii inaonesha  jinsi tulivyojikita katika  kuwawezesha wateja wetu kufikia  huduma za kifedha  pamoja na nchi zima kwa ujumla  kupitia huduma za Tigo Pesa.”

Aidha alidokeza  kuwa ongezeko kubwa katika kiwango cha gawio kumechangiwa na  kuongezeka kwa faida, kuboreshwa kwa mazingira ya soko na kukua kuliko imara kwa  idadi ya watumiaji wa Tigo Pesa kama nyenzo kuu katika ongezeko kubwa la kiwango cha faida  hususani katika  kundi la wafanya biashara. Tigo Pesa  hivi sasa  ina mtandao mkubwa wa wafanya biashara zaidi ya 50,000.


 Swanepoel  alisema kuwa kama ilivyokuwa hapo awali gawio kwa wateja  linakokotolewa kwa kuangalia wastani wa salio la kila siku la wateja la Tigo Pesa katika pochi zao za simu na kuongeza kuwa mpango huu wa kugawa faida umeainishwa katika kanuni za Benki Kuu iliyotolewa Februari 2014.

Mwaka 2014 Tigo Tanzania  ilikuwa kampuni ya kwanza ya simu duniani   kugawa faida iliyozalishwa na fedha za simu zilizopo katika Akaunti ya Udhamini kwa kipindi cha robo mwaka kwa wateja wake.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa