Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » TANZANIA BILA RUSHWA INAWEZEKANA

TANZANIA BILA RUSHWA INAWEZEKANA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


“HONGERA MAGUFULI, TANZANIA BILA RUSHWA  INAWEZEKANA”
Na Judith Mhina - MAELEZO
“Rushwa ni adui wa haki, sitapokea wala kutoa  rushwa.” Haya ni baadhi ya maneno yaliyomo kwenye ahadi za Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Nyerere ni mfano wa kuigwa duniani kwa kupinga rushwa. Hakika maneno hayo yanaonyesha uzalendo, utii na uwajibikaji.
Serikali ya Awamu ya Tano, katika kipindi cha mwaka mmoja, kupitia Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imeweza kuokoa fedha za umma kutoka bilioni saba ambazo zimeongezeka mpaka bilioni 53, huku kukiwa na mafanikio makubwa katika kuthibiti mianya ya  rushwa.
Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, katika moja ya hotuba zake amewahi kusema kuwa kuna haja ya kutunga sheria inayosema kwamba “mtu yeyote atakayepatikana akitoa rushwa na yule anayepokea wote wawili wana makosa sawa.”
Rushwa ni vita endelevu iliyoanza Awamu ya Kwanza, na imeendelezwa  na Marais waliofuatia wakiwemo Waheshimiwa Ali Hassan Mwinyi, Benjamin Mkapa na Jakaya Mrisho Kikwete. Pamoja na juhudi binafsi kama Marais na kwa kupitia TAKUKURU mwitikio wa Wananchi katika kupiga vita rushwa bado ulikuwa mdogo. Hivyo, rushwa ilikuwa inaendelea.
Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli, imeonyesha dhamira kubwa ya kuendeleza mapambano dhidi ya rushwa kwa vitendo na kwamba “Tanzania bila rushwa inawezekana”. Ili kushinda vita hivi kila mtu anatakiwa kumuunga mkono Mheshimiwa Rais, naye kwa kushiriki kivitendo.
Mara tu baada ya kuapishwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Rais alifanya ziara katika baadhi ya ofisi za Serikali ikiwemo Benki Kuu na Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA). Kufuatia ziara hiyo, Mheshimiwa Rais alijionea mwenyewe mazingira ya kazi ambayo yalionyesha kutowajibika na kuwepo kwa mianya mingi ya rushwa.
Mheshimiwa Rais hakusita kuchukua hatua mara moja kama msemo wa Kiswahili usemao “linalowezekana leo lisingoje kesho”. Aliamua kufanya mabadiliko makubwa ya uongozi, lengo ni kuhakikisha kuwa Wateule wapya wanatekeleza majukumu yao kulingana na kasi anayoitaka, kipaumbelele kikiwa ni mapambano dhidi ya rushwa ili kujenga uchumi na maendeleo ya nchi.
Katika ziara aliyoifanya Benki Kuu, Mheshimiwa Rais aliwakumbusha Watumishi juu ya uwajibikaji ikiwa ni pamoja na kuzingatia muda wa kufanya kazi katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku wawapo kazini. Aidha, Mheshimiwa Rais aliwaambia kuwa Benki Kuu ina jukumu kubwa la kukusanya na kutunza fedha zinazotokana na mapato ya Serikali, hivyo wawe makini katika kazi hiyo.
Katika ziara aliyoifanya TPA Mheshimiwa Rais alifichua upotevu wa Makontena 600 ambayo hayakulipiwa Kodi. Kutokana na upotevu huo ambao ulionekana kufanyika katika mazingira ya rushwa na muelekeo wa  Serikali kupoteza mapato mengi.
Aidha, Mheshimiwa Rais aligundua uaribifu wa mashine za kufanyia kazi wakati wa kukagua mizigo jambo ambalo lilionyesha kuwa ni sehemu ya mianya ya rushwa. Aliagiza mashine hizo zitengenezwe haraka iwezzekanavyo na wakati huo huo aliamuru mashine za kutolea risiti kielektroniki - EFDs zitolewe bure kwa Wafanyabiashara ili waweze kulipa kodi. 
Sambamba na matumizi ya mashine za EFDs, Mheshimiwa Rais amewahamasisha Wananchi kudai risiti kila wanapokwenda dukani kununua bidhaa. “Ukinunua dai risiti ukiuza toa risiti” alisisitiza katika ujumbe alioutoa kwa Wananchi. Aidha, aliagiza kukoma kwa matumizi ya bei elekezi (indicative prices) katika mchakato wa uthaminishaji wa bidhaa bandarini na usajili wa magari.
Vile vile, Mheshimiwa Rais aliagiza kuendelea kudhibiti mianya ya ukwepaji kodi ya juu, kusimamia kwa karibu zaidi matumizi ya EFDs na utoaji wa risiti,  kufuatilia na kudai malimbikizo ya kodi kutoka kwa wadaiwa sugu,  ukaguzi wa kodi kwa wafanyabiashara  na uthibiti wa misamaha ya kodi.
Pamoja na maekelezo hayo, Mheshimiwa Rais alilazimika kufanya mabadiliko ya uongozi wa TPA na TRA ambapo baadhi ya Watendaji wake walichukuliwa hatua mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutengua nyadhifa zao, kusimamishwa kazi, kuhamishwa na kupelekwa mahakamani. Kufuatia mabadiliko hayo na maelekezo ya Mheshimiwa Rais, pato la Serikali sasa limeongezeka kutoka Bilioni 800,000 hadi 1.1 Trilioni  kila mwezi.
Maeneo mengine ambayo Mheshimiwa Rais alifuatilia katika suala la ukwepaji wa kodi ni uwanja wa ndege wa Dar Es Salaam. Uwanja wa ndege ulikuwa ni eneo jingine ambalo lilikuwa likitumika kupitisha bidhaa kwa njia ya rushwa zikiwemo rasilimali za misitu,  maliasili, madini, nyara za serikali,  na madawa ya kulevya.  
Kutokana na matukio mbalimbali ya ukamataji wa Watuhumiwa na bidhaa haramu, Tanzania ilionekana kuwa kinara katika usafirishaji wa madawa ya kulevya Afrika Mashariki na Kusini mwa jangwa la Sahara.
Kuhusu utendaji wa mahakama katika kusikiliza kesi mbalimbali hususani makosa ya rushwa, Mheshimiwa Rais alionyesha kutofurahishwa na maamuzi yenye dalili za mazingira ya rushwa yanayoendelea katika chombo cha haki. Alitolea mfano maamuzi yanayotolewa pale mtu anapokamatwa na vielelezo vyote, na kupelekwa  mahakamani maamuzi huchukukua nuda mrefu kwamba upelelezi unaendelea.
Mheshimiwa Rais alihoji ni upelezi gani unaoendelea wakati vielelezo vyote vipo? Aidha, ili kudhibiti rushwa nchini Mheshimiwa Rais ameamua kuanzishwa kwa Mahakama ya Mafisadi kwa ajili ya kuwashughulikia wala rushwa.
Vita dhidi ya rushwa na madawa ya kulevya inayoendelea nchini Tanzania ikiongozwa na Rais wetu Mheshimiwa John Pombe Magufuli imeacha simulizi katika Ukanda huu wa Maziwa Makuu, Afrika na Dunia kwa ujumla. Harakati hizi amezianza tangu alipotangaza baraza lake la Mawaziri ambalo ni dogo ukilinganisha na Mabaraza ya Serikali za Awamu zilizopita. Lengo likiwa ni kupunguza gharama za matumizi ya Serikali ili fedha nyingi zitumike katika kutoa huduma muhimu za kijamii na maendeleo ya nchi kwa aujumla.
Viongozi wa nchi mbalimbali duniani, zilizoendelea na zinazoendelea, tajiri na masikini, Mashirika ya Kimataifa na watu binafsi wamejitokeza na wanaendelea kujitokeza hadharani kumpomgeza Mheshimiwa Rais kutokana na ujasiri alionao katika kutetea haki za Wanyonge, kuleta mapinduzi ya uongozi wenye kuleta tija, kupiga vita rushwa na kuzisimamia rasilimali za nchi ili ziweze kutumika kwa maendeleo ya Wananchi na Taifa kwa ujumla.
Baadhi ya nchi na Mashirika hayo yakiwemo yale ambayo yalisitisha kutoa msaada kwa Tanzania yamenza kutoa fedha kwa ajili ya maendeleo ya nchi katika Sekta za miundombinu, nishati, kilimo nk. ili kuunga mkono juhudi anazozifanya Mheshimiwa Rais.
Katika ukurasa wake wa Tweeter, Mfanyabiashara maarufu na mmiliki wa Vyombo vya Habari nchini Dkt Reginald Mengi ameandika “Nampongeza Rais Dkt John Pombe Magufuli kwa kuonyesha kwa vitendo kwamba Tanzania bila rushwa inawezekana, haya ni mafanikio makubwa na ya kihistoria Tumuombee Amewataka Wananchi kumwombea na kumuunga mkono katika harakati hizo.
Mheshimiwa Rais anaendelea kufanya mabadiliko ya Watendaji Wakuu katika Wizara, Idara, Makampuni na Mashirika ya Umma, Wakala na Taasisi mbalimbali nchini ikiwa ni hatua ya kuweka safu mpya ya uongozi ambao utatekeleza majukumu ya Serikali kwa kuzingati misingi ya sheria na utawala bora.
Madhara ya rushwa yanagusa kila mtu sio tu kwa Wanachama wa CCM ambapo imetamkwa kwenye ahadi, bali Watanzania wote  wakiwemo vijana wanaoandaliwa kulitumikia Taifa lao.. Ni dhahiri maneno haya bado yana nguvu kubwa katika kuhamasisha jamii hususani vijana mashuleni katika kuunga mkono vita dhidi ya rushwa nchini.
Hakuna atakayepinga kuwa Mheshimiwa Rais Magufuli amethubutu na sasa anahitaji kuungwa mkono katika vita dhidi ya rushwa, hamna vita ya mtu mmoja sote tushiriki. Hongera Mheshimiwa Rais ni kweli unahitaji kuombewa na Wananchi wote wanaoitakia mema nchi yetu. Mungu Ibariki Tanzania, Mungu Ibariki Afrika.
MWISHO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa