Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
SHIRIKA la Trust Care Tanzania Foundation kwa
kushirikiana na Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL) wameandaa semina ya
kuwajengea uwezo wa kifikra wanafunzi wa vyuo vikuu mbalimbali vya
jijini Dar es Salaam ikiwa na lengo la kuwabadili wanafunzi kwa ujumla
kuwa na mawazo chanya yatakayowawezesha kutumia fursa anuai
zinazowazunguka katika jamii mara baada ya masomo yao.
Akizungumzia semina hiyo inayotarajiwa kufanyika Jumamosi ya tarehe
20/05/2017 katika ukumbi wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Dar es Salaam
(DUCE) kuanzia majira ya saa tatu asubuhi, Mkurugenzi Mtendaji wa Trust
Care Tanzania Foundation, Zambert Mbwafu alisema semina hiyo ni maalum
kwa wanafunzi waliopo vyuoni kwa ajili ya kuwajengea uwezo.
Alizitaja mada ambazo wanafunzi wanatarajia kufundishwa ni pamoja na
Umuhimu wa Kujiamini na Kujijengea Uwezo, Uwezo wa Uthubutu, Vipaji na
Jinsi ya Kuviendeleza, Maadili na Nidhamu katika Kazi na Ubunifu katika
Kufikia Malengo. "Semina inawaandaa vijana waliopo na ambao wanatarajia
kumaliza elimu yao ya juu hivi karibuni kupata elimu na ujuzi
utakaowasaidia wakiwa shule na baada ya kumaliza masomo yao ili waweze
kwenda sambamba na mahitaji ya ulimwengu wa sasa..." alisema Bw. Mbwafu.
Akifafanua zaidi Mkurugenzi, Zambert Mbwafu, alivitaja vyuo
vitakavyoshiriki katika semina hiyo; ni pamoja IFM, CBE, DIT, DUCE, TIA,
UDSM, MUHAS, CHUO CHA DIPLOMASIA, KIU, CHUO CHA USTAWI WA JAMII NA CHUO
KIKUU CHA TUMAINI.
Kwa upande wa wadhamini wakuu wa semina hiyo Kampuni ya TTCL, Injinia
Enocent Msasi Mkurugenzi wa Biashara TTCL alisema kampuni hiyo inaunga
mkono kampuni ya Trust Care Tanzania kwa dhumuni lake la kuisaidia jamii
katika maeneo mbalimbali, ikiwemo sekta za kiafya, kielimu na kijamii.
Aliongeza kuwa lengo hilo linashabihiana na lengo la TTCL kuhakikisha
inakuwa na jamii bora zaidi kiteknolojia, kielimu, kiafya na kimaendeleo
kwa ujumla.
"TTCL imedhamini semina hii kwasababu inatoa mchango mkubwa katika
kujenga taifa lenye vijana wachapakazi, vijana wenye mtizamo chanya,
vijana wenye uwezo wa uthubutu, na kupambana na changamoto mbalimbali za
kimaisha, " alisema Msasi na kuongeza kuwa TTCL kupitia huduma zake
bora za intaneti, sauti na SMS inawaunga mkono vijana mara zote na
itakuwa mstari wa mbele kufanikisha juhudi zao za kuleta mabadiliko
chanya katika jamii.
"TTCL kwa miaka mingi tumekuwa tukipokea vijana wanaokuja kufanya
mafunzo kwa vitendo kutoka vyuo na taasisi mbalimbali za elimu zinazotoa
elimu katika fani tofauti tofauti. Lakini safari hii tumekuja kivingine
zaidi, kwa kuja na programu ambayo itasaidia vijana kupata uzoefu baada
ya kumaliza masomo yao. Hii itasaidia kuondoa changamoto ya vijana wetu
waliomaliza elimu ya juu ambao mara nyingi hupoteza fursa mbalimbali za
ajira kwa kukosa sifa ya uzoefu."
Vijana watakao pata fursa ya kufanya kazi na TTCL watajifunza mengi kawa
vitendo huku wakiongozwa kwa wataalamu wabobezi katika fani mbalimbali.
Tunaamini watakapomaliza programu hiyo vijana hao watapata fursa kupata
ajira kwenye taasisi na makampuni mbalimbali, au kujiajiri wenyewe,"
alisisitiza Enocent Msasi akizungumza na wanahabari leo.
0 comments:
Post a Comment