WIZARA YA AFYA,
MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO
TAARIFA KWA UMMA
KUHUSU MAADHIMISHO YA SIKU YA MTOTO WA AFRIKA: TAREHE 16/6/2017
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee
na Watoto, inautaarifu umma kuwa Tanzania
inaungana na Nchi nyingine za Afrika kuadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika, tarehe
16 Juni 2017.
Chimbuko la Maadhimisho haya ni Azimio
lililopitishwa na uliokuwa Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU) mwaka 1990 kwa lengo la kuwakumbuka watoto wa
kitongoji cha Soweto nchini Afrika
ya Kusini waliouawa tarehe 16 Juni, 1976 kutokana na ubaguzi wa rangi.
Watoto
hao walikuwa wakidai haki zao za kutobaguliwa pamoja na haki nyingine za kibinadamu ikiwemo haki ya kupata elimu
bora na hivyo kupinga mifumo ya elimu ya kibaguzi.
Kufuatia tukio hili, OAU iliazimia kuwa tarehe 16 Juni ya kila mwaka iwe Siku
ya Mtoto wa Afrika.
Kupitia Maadhimisho haya, Serikali na
wadau wengine tunakumbushwa kuandaa mipango
thabiti ya kuwaendeleza watoto na kukuza ufahamu wa wazazi, walezi na jamii kuhusu utatuzi
wa changamoto zinazowakabili watoto wa Afrika na kuzitafutia ufumbuzi.
Aidha, maadhimisho haya ni fursa
ya kutathmini utekelezaji wa Sera za Taifa zinazohusu maendeleo ya watoto kwa kuwapatia huduma stahiki ikiwa ni
pamoja na afya, elimu, ulinzi na malezi
bora ili kuwarithisha stadi mbalimbali na tunu za kitaifa kwa manufaa yao,
familia na taifa kwa ujumla.
Kwa mwaka huu Maadhimisho haya yatafanyika kimkoa hivyo
kila Mkoa utaadhimisha siku hii kwa kuzingatia mazingira ya mkoa
husika.
Kaulimbiu
ya mwaka huu ni “Maendeleo Endelevu 2030: Imarisha Ulinzi na Fursa Sawa kwa Watoto” Kaulimbiu hii inawataka
wazazi, walezi, Serikali na wadau wengine kuzingatia wajibu wetu
katika kuimarisha mifumo ya ulinzi na maendeleo ya Mtoto ili iweze kudhibiti changamoto ya ongezeko la vitendo vya ukatili nchini pamoja
na kutoa haki sawa kwa watoto wote bila ubaguzi wa aina yoyote.
Wizara inatoa wito kwa wanahabari, Asasi za Kiraia na wadau wengine kushirikiana na Serikali katika kuadhimisha
Siku hii na kuelimisha jamii kutekeleza kaulimbiu ya mwaka huu. Utekelezaji wa
Kaulimbiu hii utasaidia kuimarisha ulinzi, usalama wa Mtoto na kutoa haki sawa kwa watoto
wote kwa lengo la kufikia Malengo ya Maendeleo Endelevu ifikapo mwaka 2030.
Mwisho, tunapenda kuwakumbusha
Watanzania wote kutambua kuwa kila mmoja wetu ana
wajibu wa kuhakikisha kuwa watoto
wanapata Haki zao za Msingi kuanzia katika ngazi ya familia ambayo ni kitovu cha maendeleo ya Mtoto, jamii na
taifa kwa ujumla.
S.
Nkinga
KATIBU MKUU
WIZARA YA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO - 10/6/2017
0 comments:
Post a Comment