Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » MATUMIZI YA MITANDAO LAZIMA YAZINGATIE SHERIA NA KUHESHIMU MAADILI

MATUMIZI YA MITANDAO LAZIMA YAZINGATIE SHERIA NA KUHESHIMU MAADILI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


Na. Bushiri Matenda-MAELEZO
Serikali imesisisitiza kuwa matumizi ya mitandao lazima yazingatie sheria zilizopo na kuheshimu maadili, utamaduni na ustaarabu wa watumiaji. 

Hayo yameelezwa jana na Naibu Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo, Anastazia Wambura alipokuwa akifunga mkutano juu ya njia mpya za mawasiliano ulioandaliwa na Serikali ya Tanzania na China uliofanyika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Mwalimu Nyerere Jijini Dar es Salaama. 

“Matumizi ya mitandao ni lazima yasimamiwe, yaratibiwe na yafanyike kwa mujibu wa sheria ili mitandao iweze kuendelea na kuimarika chini ya utawala wa sheria,” amesema Wambura. 

Aliongeza kuwa katika hali ya sasa ya matumizi ya mitandao ni lazima juhudi zaidi ziongezwe katika kuimarisha maadili na kuhimiza ustaarabu na msisitizo zaidi uwekwe katika ufundishaji wa maadili katika matumizi ya intaneti ili kusaidia kukua zaidi kwa mitandao katika hali salama na yenye maadili. 

Wambura aliwaambia washiriki wa mkutano huo kuwa, Serikali ya Tanzania inayapa uzito mkubwa maendeleo ya intaneti, kwa kuwa intaneti ni moja ya njia muhimu katika kusaidia kuinua hali za maisha ya wananchi wake kupitia matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano. 

“Tangu mwaka 1995 ambapo Tanzania iliunganishwa na huduma za intaneti, tumekuwa tukichukua hatua kuhakikisha matumizi sahihi ya huduma hiyo ambapo tumetunga sheria na mfumo wa usimamizi na usalama wake, pia tunaendelea kuimarisha miundombinu ya teknolojia ya habari na mawasilino pamoja na kufanya maisha ya wananchi wetu kuwa mazuri zaidi kupitia matumizi ya teknolojia hiyo” alibainisha Wambura. 

Aidha Wambura alieleza kuwa kila siku Dunia inashuhudia kasi kubwa ya maendeleo ya teknolojia ya habari kupitia intaneti ambayo yameifanya Dunia kuwa kijiji na kurahisisha mawasiliano ambapo watu wanawasiliana kwa urahisi wakati wote bila vizuizi. 

Alisema kuwa upo umuhimu kwa Serikali hizo mbili kuweka mazingira wezeshi kisheria na uratibu utakaoweza kuhamasisha ukuaji wa matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano na kuvutia ubunifu kwa kizazi cha sasa. 

“Ushirikiano unaozingatia haki, usawa na kuaminiana ni kitu kisichoepukika ikiwa Dunia inataka kuwa na mtandao salama na wenye manufaa kwa wote,” alifafanua Wambura. 

Mkutano huo umehudhuriwa na wadau wa habari kutoka Tanzania na China ambapo uliongozwa na kauli mbiu ya “Maendeleo ya vyombo vya habari yanayochochewa na ubunifu.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa