Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Naibu
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi,Uchukuzi na Mawasiliano - Sekta ya
Mawasiliano, Injinia Angelina Madete amesema uanzishaji wa Taasisi ya
Teknolojia ya Ufundi (ICoT), utasaidia kupunguza pengo lililopo sasa
baina ya wahandisi, mafundi sanifu na mafundi mchundo hapa nchini.
Akifungua
warsha ya wataalam washauri na wadau wa Taasisi ya Teknolojia ya Ufundi
Jijini Dar es salaam leo, Mhandisi Madete amewataka wataalam hao
kufanya uchambuzi wa kina ili kuwezesha taasisi hiyo mpya kukidhi
mahitaji ya mafundi sanifu na mchundo na hivyo kukidhi uwiano wa
kimataifa unaotaka mhandisi mmoja, fundi sanifu watano na mafundi
mchundo 25.
“Tunataka kuwa nchi ya viwanda vya kati ifikapo
mwaka 2025, hivyo ni lazima tuwe na wahandisi, mafundi sanifu na mafundi
mchundo wa kutosha watakaofanyakazi kwa weledi na kumudu ushindani
katika soko la ajira”, amebainisha Injinia Madete.
Mhandisi
Madete amesema kuwa pengo la wahandisi, mafundi sanifu na mafundi
mchundo limeongezeka kutokana na vyuo vingi vya kati kutoa shahada hivyo
uwepo wa ICoT utakabiliana na kumaliza changamoto hiyo.
Aidha
amezungumzia umuhimu wa taasisi hiyo mpya kuanzisha kozi ya waendesha
mitambo ambayo mahitaji yake ni makubwa hapa nchini na kwa sasa hakuna
chuo kinachotoa kozi hiyo.
Hakikisheni taasisi hii inapata
ithibati ya Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE), ili kuwawezesha
wahitimu wote wa ICoT kupata fursa za kujiendeleza na elimu ya juu.
Naye
mratibu wa wataalam wa uanzishaji ICoT Profesa Peter Chonjo amesema
wamejipanga kuhakikisha taasisi hiyo ya teknolojia ya ujenzi inakuwa ya
mfano hapa nchini kwa kuwa itawezesha wataalam wengi wa ujenzi kuwa na
weledi unaokubalika na kuibua uwezo wa ushindani katika soko la ajira na
hivyo kuwezesha Tanzania kufikia malengo yake ya kuwa nchi ya viwanda
na uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.
Tanzania inakadiriwa kuwa
na mtandao wa barabara wenye zaidi ya kilometa elfu 87 na kati ya hizo
elfu 35 ni barabara za kitaifa na elfu 52 ni barabara za Wilaya ambazo
ujenzi wake unahitaji wataalam wa kutosha katika fani ya ujenzi na
uendeshaji wa mitambo.
0 comments:
Post a Comment