Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » MSAADA WA JAPAN WAFIKIA BIL.250/-

MSAADA WA JAPAN WAFIKIA BIL.250/-

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Imeandikwa na Matern Kayera
JAPAN kupitia Shirika lake la Maendeleo la Kimataifa (JICA) imetenga bajeti ya Sh bilioni 251.2 kwa ajili ya misaada ya maendeleo kwa Tanzania kwa mwaka wa fedha 2017/18 tofauti na Sh bilioni 90 ilizotenga kwa mwaka uliopita 2016/17.
Fedha hizo ni mwendelezo wa Serikali ya Japan wa kutoa misaada na mikopo kwa Serikali ya Tanzania tangu ushirikiano wa kimaendeleo kati ya mataifa hayo mawili uanze mwaka 1963. Mwakilishi Mkuu wa Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Japan (JICA), Toshio Nagase alisema jana Dar es Salaam kuwa misaada ya Kijapani kwa Tanzania inakaribia dola za Kimarekani milioni 3,855.31 kati ya kipindi cha mwaka 1963 hadi 2015.
Alisema kuwa kiasi hicho cha fedha ni kikubwa kutolewa kwa Tanzania ikilinganishwa na wapokeaji wengine wa misaada ya maendeleo kwa nchi za Afrika zilizo kusini mwa Jangwa la Sahara na ya kwanza kwa Afrika Mashariki ikifuatiwa na Kenya (dola 3,835.41), Zambia (dola 2,598.33). “Tunaridhishwa na matumizi ya fedha za misaada na mikopo tunazotoa kwa Serikali ya Tanzania na miradi ambayo Japan imeisaidia Tanzania.
Kwa mfano, JICA imesaidia kuboresha barabara za jiji la Dar es Salaam tangu mwaka 1980 ikiwemo daraja la Selander, Barabara ya Morogoro, Barabara ya Ali Hassan Mwinyi, barabara mpya ya Bagamoyo, eneo la Kariakoo, Sinza, Mwananyamala, Ilala, Tabata, Kijitonyama na Barabara ya Kilwa,” alisema Nagase na kuongeza: “Katika mwaka 2016/17, JICA ilitekeleza majukumu yake kwa ufanisi hasa katika kuwekeza katika miundombinu na rasilimali watu.
Baadhi ya uwekezaji katika miundombinu inajumuisha ujenzi wa barabara za juu Tazara (Tazara flyover), uendelezaji wa barabra za ukanda wa Mtwara (Mtwara corridor development project), uendelezaji wa barabara za ukanda wa kaskazini ambao ni sehemu ya barabara kuu ya Afrika Na. 4 (Cairo- Cape-Trans-African Highway No. 4) na ujenzi wa laini ya umeme kutoka Iringa hadi Shinyanga.” Imeelezwa kuwa mradi wa ujenzi wa barabara za juu Tazara ndiyo mradi mkubwa kati ya miradi ambayo JICA imeitekeleza nchini Tanzania.
Kwa mujibu wa Meneja wa Mradi wa Tazara, Nobuhiko Maruni, barabara za juu Tazara zina urefu wa mita 425 na zina uwezo wa kutumika kwa miaka 100 ijayo kama zitatunzwa na kufanyiwa ukarabati wa mara kwa mara. Nagase aliongeza kuwa Japan huipa Tanzania kila mwaka msaada wa kimaendeleo wa dola za Kimarekani milioni 20 na mkopo wa dola za Kimarekani milioni 100.
Kuhusu rasilimali watu, Mwakilishi huyo wa JICA alisema kwa mwaka uliopita waliweza kuwekeza katika rasilimali watu katika sekta mbalimbali kama vile kilimo katika maeneo mbalimbali nchini, biashara, afya, uvuvi, lakini pia upatikanaji wa maji safi na salama katika mkoa wa Tabora na Zanzibar, ufadhili wa masomo nchini Japan kwa vijana wa Tanzania kupitia mpango wake ujulikanao kama elimu ya biashara Afrika (African Business Education-ABE).
Kwa mujibu wa Nagase, JICA iliweza kuwasaidia Watanzania 18,613 kupata fursa ya mafunzo nchini Japan kuanzia mwaka 1963 hadi mwaka 2015. Kwa kiwango cha shahada ya uzamili jumla ya Watanzania 81 wamesaidiwa kupata elimu hiyo kuanzia mwaka 2014 hadi mwaka 2017.
Aidha, shirika hilo limesema kuwa limejipanga kuendelea kuboresha mipango ya kilimo kwenye wilaya mbalimbali kwa mwaka 2017/18 kupitia mpango wa TANSHEP (Tanzania Small Holder Horticulture Empowerment Promotion) pamoja na kumalizia ujenzi wa barabara za juu Tazara ikiwa ni sehemu ya kukabili changamoto za maendeleo ya Tanzania kulingana na mpango wa pili wa maendeleo wa miaka mitano na matakwa ya utawala wa Rais John Magufuli.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa