Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » MUSWADA SHERIA YA ULINZI WA TAARIFA BINAFSI WAJA

MUSWADA SHERIA YA ULINZI WA TAARIFA BINAFSI WAJA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

 Imeandikwa na Matern Kayera
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Edwin Ngonyani
SERIKALI iko kwenye hatua za mwisho za kupeleka bungeni Muswada wa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi ili kudhibiti matumizi mabaya ya simu za mkononi, barua pepe na mitandao ya kijamii.
Hayo yalisemwa na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano jana, Edwin Ngonyani (pichani) wakati akifungua mkutano wa pamoja kati ya Wachina na Watanzania uliofanyika kwenye Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam.
Sheria hiyo ya kudhibiti matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii itakuwa ya tatu baada ya Sheria ya Uhalifu wa Kimtandao na Sheria ya Miamala ya Kimtandao kupitishwa mwaka 2015.
Imeelezwa kuwa muswada huo wa sheria hautachukua zaidi ya mwaka mmoja kupitishwa kuwa sheria na itakapokuwa sheria kamili itawapa fursa watu watakaochafuliwa au kutendewa uhalifu wa kimtandao kudai fidia.
Kwa mujibu wa Naibu Waziri Ngonyani, watumiaji wa simu waliosajili simu zao za mkononi imeongezeka kutoka 300,000 mwaka 2000 hadi kufikia milioni 39 kwa sasa. Kuhusu idadi ya mitandao ya kijamii inayotumika nchini, Ngonyani alisema kwamba ni vigumu kwa sasa kuidhibiti mitandao hiyo kwa asilimia 100 kwa kuwa wanaoimiliki wako nje ya nchi na hasa Marekani na siyo Watanzania.
Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi itasaidia kumjua mtu mahususi atakayefanya uhalifu kupitia simu yake ya mkononi au hata kama atatumia simu ya mtu mwingine, na hivyo hivyo kwenye mitandao ya kijamii na barua pepe.
Naye Balozi wa China nchini, Dk Lu Youqing alisema matumizi ya mitandao ya kijamii yameimarisha zaidi ushirikiano kati ya Tanzania na China. Alisema ushirikiano kati ya Tanzania na China umekuwa na manufaa katika nyanja mbalimbali kama vile kisiasa, kiuchumi, kiutamaduni, amani na usalama, ushirikiano wa kimataifa na ushirikiano baina ya mtu na mtu. Kuhusu maendeleo ya intaneti alisema kwamba kati ya kampuni 10 kubwa za intaneti duniani, kampuni nne zinatoka China.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa