Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Wataalam
wa masuala ya maji kutoka nchi 25 za Bara la Afrika wamekutana kujadili
njia zitakazowezesha upatikanaji wa maji safi na salama mijini na
vijijini ifikapo mwaka 2030.
Mkutano huo umefunguliwa leo Jijini Dar es Salaam na Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Mhandisi Gerson Lwenge ambaye amesema kuwa majadiliano
hayo yameanzishwa baada ya azimio la Umoja wa Mataifa Namba 6 kuzitaka
nchi zote Duniani kuhakikisha kuwa wananchi wao wanapata huduma ya maji
safi na salama ifikapo mwaka huo.
“Ili
kuhakikisha agizo la Umoja wa Mataifa linatekelezwa, nchi za Umoja wa
Afrika ziliamua kuunda kamati za wataalam watakaojikita katika kupanga
mikakati endelevu ya kutekeleza agizo hili,”alisema Mhandisi Lwenge.
Mhandisi
Lwenge ameongeza kuwa baada ya majadiliano hayo wataalam watapeleka
taarifa katika kikao cha Baraza la Mawaziri wa Maji Afrika (AMCOW)
kinachotegemewa kufanyika mwezi Septemba mwaka huu ili kuweza kupata
tathmini ya kila nchi namna inavyotekeleza azimio hilo.
Aidha,
Mhandisi Lwenge amefafanua kuwa kwa miaka mitano ijayo, Tanzania
imejipanga kuhakikisha kuwa wananchi wanaokaa mijini wanapata maji safi
na salama kwa asilimia 95 na vijijini asilimia 85, uondoaji wa maji taka
kwa asilimia 30 pamoja na kuhakikisha nyumba za vijijini zina vyoo.
Kwa
upande wake Katibu Mtendaji wa AMCOW, Dkt. Conisius Kanangire amesema
kuwa mkutano huo umewashirikisha wataalam pamoja na wadau kutoka
mashirika mbalimbali yanayohusika na uangalizi wa mabonde ya maziwa na
mito Afrika ili nao waweze kutoa mchango wa mawazo utakaopelekea nchi za
Afrika kuwa na maendeleo makubwa katika sekta ya maji.
”Baraza
la Mawaziri wa Maji pekee haliwezi kuleta mafanikio makubwa
tunayoyataka kwa Afrika ndio maana tumeamua kuwashirikisha wataalam wa
maji kutusaidia namna ambavyo tutaweza kuwa na mikakati mizuri ambayo
itawezesha upatikanaji wa maji safi na salama kwa nchi zote,” alisema
Dkt. Kanangire.
Dkt.
Kanangire ameishkuru Serikali ya Tanzania kwa kushiriki bega kwa bega
katika kuhakikisha baraza hilo linafanya kazi nzuri hivyo anategemea
kuwa kikao hicho kinachoendelea nchini kitatoa majibu ya uhakika juu ya
upatikanaji wa maji safi na salama.
0 comments:
Post a Comment