Naibu
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Dkt. Mhandisi Juliana
Pallangyo (wa pili kushoto) akifafanua jambo katika mkutano huo.
Mkurugenzi
Mtendaji wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF), Godfrey Simbeye (katikati)
akifafanua jambo katika mkutano huo. Kushoto ni Naibu Katibu Mkuu wa
Wizara ya Nishati na Madini Dkt. Mhandisi Juliana Pallangyo na kulia ni
Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya ya Watoa Huduma Katika Sekta ya Mafuta na
Gesi Tanzania (ATOGS), Abdulsamad Abdulrahim.
Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya ya Watoa Huduma Katika Sekta ya Mafuta na Gesi
Tanzania (ATOGS), Abdulsamad Abdulrahim (katikati) akielezea mikakati ya jumuiya
hiyo ya kuwezesha wadau mbalimbali wataoshiriki katika utoaji wa huduma kwenye
mradi wa ujenzi wa bomba la mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda hadi katika
Bandari ya Tanga nchini Tanzania kwenye mkutano wa waandishi wa habari uliofanyika
jijini Dar es Salaam tarehe 02 Agosti, 2017. Kushoto ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara
ya Nishati na Madini Dkt. Mhandisi Juliana Pallangyo na kulia ni Mkurugenzi Mtendaji
wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF), Godfrey Simbeye.
Na Greyson Mwase, Dar es Salaam
Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya ya Watoa Huduma Katika Sekta ya Mafuta na Gesi
Tanzania (ATOGS), Abdulsamad Abdulrahim, amesema kuwa jumuiya inakaribisha
makampuni mbalimbali nchini kujiunga na jumuiya hiyo na kuwezeshwa kwenye
ushiriki katika mradi wa ujenzi wa bomba la mafuta ghafi kutoka Hoima nchini
Uganda hadi katika Bandari ya Tanga nchini Tanzania.
Abdulrahim aliyasema hayo leo kwenye mkutano wa waandishi wa habari uliofanyika
jijini Dar es Salaam na kushirikisha Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini
Dkt. Mhandisi Juliana Pallangyo, na watendaji kutoka Jumuiya ya Watoa Huduma
Katika Sekta ya Mafuta na Gesi Tanzania (ATOGS), Baraza la Taifa la Uwezeshaji
Wananchi Kiuchumi (NEEC) na Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF).
Alisema kuwa tayari baadhi ya makampuni yameshaanza kujiunga na jumuiya hiyo na
kutaka watu binafsi wenye nia ya kushiriki katika utoaji huduma kwenye mradi wa
bomba la mafuta kujiunga na jumuiya hiyo ili kuwezeshwa.
Alisema kuwa kazi kubwa itakayofanywa na ATOGS ni pamoja na kuwawezesha
washiriki kupata utaalam wa utoaji wa huduma ikiwa ni pamoja na namna ya kupata
mikopo kwenye mabenki na taasisi mbalimbali za kifedha.
Aidha, alipongeza jitihada za serikali katika kuwezesha uchumi wa viwanda kupitia
mradi wa bomba la mafuta hali inayoleta matumaini ya kuwa nchi kutoka kwenye
orodha ya nchi masikini duniani na kuingia katika orodha ya nchi zenye kipato cha kati
ifikapo mwaka 2025 kama Dira ya Maendeleo ya Taifa, inavyofafanua.
Alisisitiza kuwa lengo la jumuiya ni kuwaunganisha watoa huduma wote na kuwapa
elimu ya namna bora ya utoaji wa huduma ili kuweza kushiriki kikamilifu katika mradi
wa bomba la mafuta.
Aliongeza kuwa mradi wa bomba la mafuta utaleta mageuzi makubwa ya kiuchumi
kuanzia kwa mwananchi mmoja mmoja hadi kwa taifa kwa ujumla na kuwataka
wananchi hasa waishio katika mikoa itakayopitiwa na miundombinu ya bomba la
mafuta kuchangamkia fursa na kuondokana na umasikini.
Aliendelea kutaja mikoa itakayopitiwa na miundombinu ya bomba la mafuta kuwa ni
pamoja na Kagera, Geita, Shinyanga, Tabora, Singida, Manyara na Tanga.
Wakati huo huo, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Dkt. Mhandisi
Juliana Pallangyo alipongeza uanzishwaji wa ATOGS na kusema kuwa jumuiya hiyo
imekuja wakati mwafaka wa mradi wa bomba la mafuta na kuwataka watanzania
kuchangamkia fursa zilizopo kupitia jumuiya hiyo.
Dkt. Pallangyo alitumia fursa hiyo kuwakaribusha watanzania kujitokeza katika uzinduzi
wa mradi wa bomba la mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda hadi katika Bandari
ya Tanga nchini Tanzania unaotarajiwa kufanywa na Marais Yoweri Museven wa
Uganda na Dkt. John Magufuli siku ya Jumamosi wiki hii.
Katika hatua nyingine, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF).
Godfrey Simbeye aliyataka makampuni yatakayopata tenda ya kutoa huduma kwenye
mradi wa bomba la mafuta kufanya kazi kwa umahiri na uadilifu mkubwa kwa manufaa
ya nchi.
“ Kutakuwepo na kazi nyingi sana zitakazotolewa kwa watanzania hususan huduma
kwa wakandarasi watakaojenga bomba, umakini na uadilifu wa hali ya juu unahitajika ili
kuleta sifa njema kwa nchi,” alisema Simbeye
Aliishauri serikali kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kuweka
mpango maaalum wa kutoa mafunzo wa namna ya kujenga mabomba ili baadaye
wataalam wa ndani ya nchi wafanye kazi ya kujenga mabomba na kupunguza
gharama.
Aliendelea kusema kuwa wakati serikali ikiimarisha mazingira mazuri ya uwekezaji
nchini, mabenki yajiandae kutoa mikopo mara moja kwa makampuni yatakayopata
tenda kwenye mradi wa bomba la mafuta.
0 comments:
Post a Comment