Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » LUKUVI AKAMATA MAFISADI ARDHI

LUKUVI AKAMATA MAFISADI ARDHI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

 Imeandikwa na Lucy Lyatuu

WAZIRI wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi
WAZIRI wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi ameendelea kusikiliza mashauri ya migogoro ya ardhi jijini Dar es Salaam na kubaini kuwepo kwa mafisadi wa utapeli wa ardhi wanaoshirikiana na maofisa ardhi. Pamoja na hayo, waziri huyo amebainisha kuwa wakazi wengi wa jiji hilo wamekuwa wakimiliki ardhi kutokana na hati feki na tayari amefuta hati 180 zilizokuwa zimedhulumiwa na maeneo hayo kurudishwa kwa wenyewe.Lukuvi alisema hayo Dar es Salaam jana wakati akisikiliza mashauri mbalimbali yanayohusu migogoro ya ardhi ndani ya jiji hilo kwa lengo la kuyatatua.
Alisema kuanzia juzi amesikiliza mashauri 99 na sehemu kubwa ya matatizo hayo yamesababishwa na watendaji wa serikali wakiwemo pia maofisa ardhi ambao wameanza kudhulumu wananchi ardhi tangu kipindi cha uongozi wa awamu ya kwanza hadi sasa. Alibainisha kuwa matapeli hao wa ardhi, walifikia hatua ya kuthubutu hadi kuchovya hati katika majani ya chai ili kuonekana ni ya zamani.
Alitoa mfano wa moja ya shauri alilosikiliza na kumbaini mkazi wa jijini hilo mwenye asili ya Kiarabu aliyetambuliwa kwa jina la Omar Mohamed Agil, anayetumia Kampuni ya Holland Investment, anayedaiwa kuchukua viwanja vya watu na kughushi hati na hata kuweza kuitumia kwa kukopa benki kiasi cha Sh milioni 300. “Omar aliweza kuingia ubia na mzee mmoja mkazi wa Mtoni na kisha kuchukua hati ya mzee huyo na kwenda kukopea benki.
Alienda hadi mkoani Mtwara na kutumia hati hiyo hiyo kwa kushirikiana na mjomba wake anayejulikana kwa jina la Hassan Salum ambaye naye amemjumuisha kuwa mbia wa hati hiyo na kwenda Benki ya Amana na kukopa shilingi milioni mia tatu,” alisema Lukuvi.
Aidha, alisema mtuhumiwa huyo pia alikwenda eneo la Kawe Mzimuni kwa mwanamke mmoja aliyetambulika kwa jina la Hamida Simba, na kuchukua hati ya mwanamke huyo na kuitoa nakala kivuli ya hati hiyo na kurudisha feki na kuondoka na halali. Kutokana na hayo aliyoyabaini, aliagiza kuwa ni marufuku kwa watendaji wote katika ofisi za ardhi nchini kufanya miamala yoyote ya hati, nyaraka ama kupokea chochote kutoka kwa mtuhumiwa huyo.
“Lakini pia nawaonya matapeli kutojaribu tena kunyang’anya raia ardhi zao, kwani sasa wamejulikana na hata hata wale wenye tabia ya kutumwa wizarani ni marufuku kuingia katika jengo hilo,” aliagiza Lukuvi. Akizungumzia hali ya utapeli wa viwanja katika jiji hilo, alisema hali ni mbaya kwani wananchi wengi wamedhulumiwa viwanja vyao wakapewa watu wengine, wengine wamejenga kwenye ardhi wasizomiliki, wametapeliwa na wengine wamepewa hati feki.
Alisema yapo maeneo ambayo hupimwa zaidi ya mara moja na watendaji hali inayosababisha watu wengi kumiliki eneo moja ambalo halitoshi, lakini watendaji hao hawajali bali huyapatia maeneo hayo michoro yote kuanzia wizarani hadi wilaya.
Lukuvi alisema pia kuna matapeli wanaokwenda kutembelea maeneo yaliyo wazi halafu wanakwenda ofisi za Halmashauri na maofisa ardhi na kuwapa ofa stahiki za watu wanaomiliki na wanapogundua anayemiliki ni nani wao hutengeneza ofa nyingine, halafu ofisa ardhi anasaini na kuchomoa ile ambayo ni halali katika faili na kuchomeka feki.
“Ili mpango huo uweze kufanikiwa, maofisa hao hubadili hata mwaka wa ofa hiyo na kuweka wa mwanzo zaidi, na ili ionekane kwamba ni ya zamani, hata hiyo huichovya katika majani ya chai na kuirudisha katika file,” alisema na kuongeza kuwa katika hati hufanya hivyo hivyo kwa kuchapa upya na kuweka mhuri na kuiga saini.
Alisema kwa wale wote waliokutwa na madhara hayo ya kuvamiwa na kunyang’anywa, serikali inarudisha ardhi kwa anayestahili na waliodhulumiwa na maofisa wa serikali, wanapewa maene mengine mbadala.
“Mpaka sasa watu 700 wameshapewa viwanja katika eneo la Pemba mnazi, Kigamboni, ili kuwafuta machozi kutokana na kudhululiwa huku,” alifafanua Lukuvi. Alisema watendaji waliofanya utapeli huo pamoja na kwamba wapo baadhi walishastaafu, waliopo kazini watachukuliwa hatua na tayari waliobainika wameshaanza kufukuzwa na kusimamishwa kazi.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa