Imeandikwa na Gloria Tesha
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba amewataka
Watanzania kutolalamika kwa uamuzi wowote unaofanywa na serikali ya
sasa, kwani una nia njema kwa mustakabali wa Taifa.
Mwigulu amewataka Watanzania kuendelea kumwombea Rais John Magufuli
ambaye anadhihirisha kwa vitendo kuchukia wizi na ufisadi ili nia njema
aliyonayo kwa taifa, aifikie. Akitoa salamu katika ibada ya kuchangia
ujenzi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa
Mbezi Luis, Dar es Salaam jana, Mwigulu alisema kuna uamuzi Serikali
inaochukua huenda usieleweke kwa haraka lakini una lengo jema kwa taifa.
Alitoa mfano kuwa Rais Magufuli anachukia kwa vitendo rushwa na
ufisadi hivyo hawezi kucheka wakati akifanya uamuzi, kwa kuwa hakuna
dini yoyote inayomchekea shetani wakati wa kumkemea. “Ili nchi ipige
hatua kuna mambo yalikuwa lazima yafanyike. Kuna mambo si rahisi
kuyaelewa kwa haraka haraka, lakini niwasihi mwendelee kumwombea rais
kwa kuwa ana nia njema.
“Mkimwombea Rais na sisi tunapata lifti humo humo na mambo yanaenda,”
alisema Mwigulu. Alisema uovu ni lazima ukemewe na kutolea mfano Yesu
Kristo alipoingia hekaluni na kukuta biashara inafanyika, alipindua meza
na kufungulia njiwa kwa ukali na ndivyo anavyofanya Rais. “Mmeshawahi
kuona shetani anakemewa kwa upole? Uovu lazima ukemewe kwa nguvu,”
alisema Mwigulu.
Kuhusu kuchangia ujenzi wa kanisa hilo, Mwigulu alisema ni muhimu
kuchangia ujenzi wa nyumba za ibada kwa kuwa zinapunguza uovu katika
jamii. Alisema mikoa yenye nyumba nyingi za ibada, uovu nao unapungua na
ikiwa watu hawatajitoa kuchangia Mungu, huruhusu wapate hasara ili
ifidie uchoyo waliouonesha kumwibia Mungu. Kanisa hilo la Usharika wa
Mbezi Luis linajengwa kutokana na bomoabomoa inayoendelea katika
barabara ya Morogoro .
CHANZO HABARI LEO
0 comments:
Post a Comment