Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » SERIKALI KUTOZA KODI YA VIWANJA

SERIKALI KUTOZA KODI YA VIWANJA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

 Imeandikwa na Lucy Lyatuu
SERIKALI imesema kuanzia mwaka huu itatangaza kodi ambayo watu wote wenye viwanja nchini, wakiwemo wanaoishi katika makazi yasiyopimwa, wataanza kulipa kodi hiyo ya ardhi kwa kuhakikisha wananchi wote wanaishi katika makazi yaliyorasimishwa.
Imesema wanaoishi katika makazi yasiyopimwa watatambuliwa kwa kupewa leseni za makazi zitakazokuwa na ukomo, wakitakiwa kuishi kwa muda utakaopangwa na baada ya kipindi hicho kumalizika, watatakiwa maeneo yao yawe yameshapimwa tofauti na hivyo manispaa zitaagizwa kufunga nyumba zao. Aidha, imesema serikali haitojihusisha tena katika kupima maeneo yoyote ya ardhi kuanzia sasa, na badala yake kinachotakiwa ni wananchi wenyewe kuwajibika kwa kuunda kamati za urasimishaji zitakazosaidia maeneo yao kupimwa.
Kadhalika imesema katika kudhibiti matapeli wa ardhi, na migogoro mbalimbali ya ardhi, inaanzisha mradi mpya utakaoanzia katika Manispaa ya Ubungo na Kinondoni ambao utawezesha kutoa hati za makazi katika njia ya elektroniki. Hata hivyo, imetoa hati 84 za makazi kwa wananchi wa Kata ya Kimara, Mtaa wa Kilungule A Manispaa ya Ubungo jijini Dar es Salaam na tayari viwanja 4,333 vimeshapimwa, ikiwa ni utekelezwaji wa mpango darasa wa kupima viwanja 6,000 vya kata hiyo na mitaa yake sita.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi alisema hayo jana jijini Dar es Salaam wakati akikabidhi hati hizo kwa wananchi wa Mtaa wa Kilungule na kuongeza kuwa wenye viwanja vikubwa visivyopimwa nao watawajibika kulipa kodi na kuhakikisha maeneo hayo yanapimwa.
“Maeneo yote yasiyopimwa ambayo ni makazi holela watapewa leseni na baada ya muda fulani yatatakiwa kuwa yamepimwa,” alisema Lukuvi na kuongeza kuwa ni lazima maeneo yote nchini yarasmishwe na kuanzia sasa serikali haiwajibiki tena kupima na upimaji wa Kata ya Kimara ni wa mwisho, wananchi wakitakiwa kushughulika wao wenyewe wakianza kuwa kuunda Kamati za urasmishaji katika mitaa yao.
“Kamati hizo ni za wananchi wenyewe watakaoshughulika nazo, na fedha watakazokuwa wakichanga zisiende halmashauri au wizarani kwani zitaibiwa, wawe wenyewe na hata mtumishi wa serikali asiwe mtia saini,” alisema Lukuvi na kuongeza kuwa wananchi wenyewe ndiyo watakaoamua nani wamuweke wapi na watakaowaamini. Alisema nchi nzima ziundwe Kamati za Urasmishaji zitakazokuwa na mpango madhubuti wa urasmishaji na serikali itaingia kwa kupeleka wataalamu.
Kuhusu wenye viwanja vikubwa, waziri huyo alisema Dar es Salaam wapo wananchi wenye maeneo mengi yasiyopimwa huku akiishi kwa kutambuliwa na Serikali za Mitaa ambapo atatakiwa kuanza kulipa kodi. “Wapo watu wenye ekari mpaka mia tatu wanakaa tu, akiuza kiwanja kimoja kimoja kila mwaka, hakuna mtu atadumu na eneo kubwa mjini lisilopimwa na lisilolipiwa kodi, maana wapo wanaotunza tu maeneo, hakuna shambabubu mjini waende mikoani,” alieleza Lukuvi.
Alitolea mfano wenye maeneo makubwa eneo la Kigamboni kwamba watu wa aina hiyo wanatakiwa kulipia kodi kubwa zaidi ili manispaa zipange mipango yake ya mendeleo, kwa kuwa haiwezekani kuyashika tu maeneo. Alizitaka manispaa zote kutoruhusu watu kujenga ovyo, wakitakiwa kuwa macho na hata kama lipo eneo lililoko wazi walichukue na kulipima.
Kuhusu hati, alisema katika Jiji la Dar es Salaam eneo lisilopimwa ni asilimia 75, hivyo wananchi wengi wamekuwa wakiishi katika makazi yasiyopimwa na Serikali ya Awamu ya Tano inalenga kuwaondolea wananchi urasimu ama kero za ardhi na watu waliojiona mangimeza. Alisema wananchi walikwazwa na gharama za urasmishaji na tayari serikali imepunguza umilikishaji wa ardhi kwa asilimia 67, tozo hiyo kwa sasa nchi nzima itakuwa asilimia 2.5 na italipwa mara moja na baada ya mwananchi kupata hati, tozo hiyo ni ya mara moja kwa mwaka.
Alisema katika kupunguza kero hizo za ardhi, wizara yake imezungumza na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) ili kupunguza urasimu na itapeleka muswada bungeni ili utoaji wa vibali vya ujenzi katika manispaa upitishwe kwa haraka ndani ya wiki moja ili wananchi wapate fursa ya kujenga kwa haraka huku vibali vikipatikana.
Aliwaonya viongozi wa mitaa kuacha kushirikiana na matapeli wakitumia ovyo mihuri yao, kwamba wapo baadhi yao tabia zao ni za ovyo, waliogombea nafasi hizo wakiwemo wasiokuwa na sifa lengo likiwa ni kumiliki maeneo ya watu.
“Katika hili, wakuu wa wilaya fanyeni ukaguzi katika maeneo yenu muone kama wananchi wenu walijenga ama wanamiliki kwa mujibu wa sheria,” alisema Lukuvi na kuongeza kuwa wapo wenyeviti wa mitaa, watendaji wenye ndoa za kudumu na matapeli jijini.
“Wengine wamekuwa wakijifanya mapredeshee mijini wakivaa cheni kubwa kumbe ni wezi tu wa ardhi, nimeanza kutoa majina pale wizarani kwamba hakuna kupokea muamala au nyaraka yoyote, ubadilisho wa hati yoyote wakiona majina ya watu fulani fulani ambao ni matapeli, wako watu niliwahi kuwahamisha Dar na ninasikia wamerudi nitachunguza na nikigundua wamerudi nitawatupa Tanganyika,” alisema Lukuvi akisisitiza kuwa Jiji la Dar es Salaam limeharibika sana na wananchi wakionewa sana.
Awali akizungumza, Mkurugenzi wa Mipango Miji nchini, Profesa John Lupala alisema mradi wa urasimishaji Kata ya Kimara ulikuwa ni mpango darasa ili kujifunza na ulianza Januari mwaka jana na uandaaji ukianza Aprili, 2016.
Profesa Lupala alisema mpango huo ulihusisha Kata ya Kimara na Saranga kwa lengo kupima vipande 6,000, wakianza na urasmishaji, kufanya uchambuzi, michoro ya mipango miji, upimaji na kumilikisha. Alisema hadi Juni 30, 2017 wametambua vipande 4,768 na viwanja 4,333 vimepimwa na vilivyobakia 1,607, mradi ukitekelezwa kwa asilimia 79.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa