Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » VIWANJA KULIPIWA KWA SIMU

VIWANJA KULIPIWA KWA SIMU

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

 Imeandikwa na Halima Mlacha
WIZARA ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeanzisha rasmi mfumo mpya wa kulipia kodi ya ardhi kwa njia ya kieletroniki, unaolenga kupunguza kero wanazopata walipa kodi ya kutumia muda na mlolongo mrefu wakati wa kulipia.
Kuanzia sasa mmiliki yeyote mwenye ardhi iliyopimwa na kupatiwa hati ya umiliki, anaweza kuulizia kiasi cha fedha anazodaiwa na kulipia kodi hiyo ya mwaka kwa kutumia simu yake ya mkononi, tovuti ya wizara hiyo au kulipia kupitia benki. Pamoja na hayo, wizara hiyo, imepanga kushirikiana na serikali za mitaa kufanya ukaguzi maalumu wa maeneo yote ya ardhi yasiyopimwa, ili kuweza kujua ni wananchi wangapi wana maeneo hayo na maeneo gani, waweze kuingizwa kwenye mfumo wa kulipia kodi ya ardhi.
Akizungumza ofisini kwake Dar es Salaam jana, Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dk Moses Kusikula alisema mfumo huo utamuwezesha mmiliki wa ardhi kulipia ardhi hiyo kwa dakika chache, badala ya kutumia siku nzima kusubiri kupata huduma ya malipo.
“Zamani watu walikuwa wanatumia muda mwingi kufanikisha kulipia kodi ya ardhi, walilazimika kwenda kwenye vituo vyetu aulizie kwanza deni lake ndipo alipie, wakati wote huo hulazimika kupanga foleni ndefu kwa kuwa watu ni wengi wanaolipia huduma hiyo.
Sasa tumekuja na mfumo huu kwa ajili ya kuwarahisishia wananchi,” alifafanua. Alisema wizara hiyo imeingia mkataba na kampuni tatu za simu za mkononi zinazotumia huduma za fedha kwa njia ya mtandao ambazo ni Tigo, Vodacom na Halotel, lakini pia imeingia mkataba na benki mbili za NMB na CRDB kwa ajili ya huduma hizo za malipo ya kodi ya ardhi.
Alisema katika huduma hiyo ya eletroniki kila muamala utakuwa na risiti ya eletroniki, lakini pia endapo mmiliki wa ardhi atahitaji risiti za kawaida, atawasilisha kwenye vituo vya ardhi au wizarani ujumbe mfupi wa kukamilisha malipo na kupatiwa risiti yake. Hata hivyo, alisema changamoto inayoikabili mfumo huo kwa sasa ni elimu kwa wananchi kwani wengi wao bado hawajaelewa vyema namna mfumo unavyotumika hasa katika kulipia kodi hiyo.
Alisema kutokana na hali hiyo, wizara hiyo imepanga mwezi wote wa Agosti mwaka huu kupeleka wataalamu wake katika kila halmashauri kwa ajili ya kutoa mafunzo juu ya namna sahihi ya kutumia mfumo kwa wananchi. “Napenda kubainisha kuwa, zamani tulikuwa na akaunti za kukusanyia kodi hii, lakini sasa tunazifunga akaunti zote na kuachia mfumo huu wa eletroniki ndiyo uhusike na malipo ya kodi hii,” alieleza.
Akizumgumzia maeneo yasiyopimwa, Dk Kusiluka alikiri kuwa kwa sasa maeneo hayo hayapo kwenye mfumo huo wa elektroniki, lakini baada ya kufanya ukaguzi maalumu yataingizwa kwenye mfumo wa kulipia kodi hiyo, wakati utaratibu wa kupima ardhi ukiendelea nchi nzima.
Aliwatahadharisha wale wote wanaomiliki ardhi na kuwa na hati au ofa, kuhakikisha wanalipia kodi hiyo kwa wakati, vinginevyo muda wa malipo ukipita watatozwa faini na wasipolipa pia baada ya siku 14 wataburuzwa mahakamani. Kwa mujibu wa mfumo huo, wanaotumia mitandao ya simu wanatakiwa kupiga namba *152*00# na kufuata maelekezo, na kwa wale wanaotumia mtandao wa wizara waingie kwenye tovuti www.ardhi.go.tz.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa