Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » WAFANYABIASHARA WA JNIA WAPEWA MWEZI MMOJA NA WAZIRI MBARAWA..

WAFANYABIASHARA WA JNIA WAPEWA MWEZI MMOJA NA WAZIRI MBARAWA..

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

 Waziri Wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa (Katikati), akizungumza na wafanyabiashara wanaotoa huduma katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA), wakati alipofanya kikao cha pamoja, leo Jijini Dar es Salaam.

Waziri Wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, akizungumza na wafanyabiashara wanaotoa huduma katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA), wakati alipofanya kikao cha pamoja, leo Jijini Dar es Salaam.
Picha na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.


WAZIRI wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa ametoa Mwezi mmoja kwa wafanyabiashara wanaotoa huduma katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA) kulipa kodi ya Majengo kama mikataba yao inavyolekeza.

Waziri Mbarawa ametoa agizo hilo leo wakati alipokutana na wafanyabiashara hao ili kujadili changamoto mbalimbali zilizopo na jinsi ya kuzitatua ili kuendelea kutoa huduma bora katika uwanja huo.

“Kulipa kodi za majengo hapa ni suala la lazima, hivyo ifikapo Septemba mwishoni nataka kuona wafanyabiaashara wote mmeshalipa kodi ya pango, makusanyo haya ni muhimu kwetu ili tuendelee na hatua nyingine za uboreshaji wa viwanja vya ndege na huduma nyinginezo.” Amesisitiza Profesa Mbarawa.

Aidha, Profesa Mbarawa ameutaka uongozi wa Mamlaka ya viwanja vya ndege Tanzania (TAA), Kuhakikisha mikataba yote ya upangishaji wa majengo inapitiwa upya na kufanyiwa marekebisho ili thamani ya fedha iendane na wakati huu.

Profesa Mbarawa amewahimiza wafanyabiashara hao kubadilika na kuendana na mabadiliko ya Sayansi na Teknolojia ili kuweza akuendana na ushindani wa kibiashara uliopo ndani na nje ya nchi.

Ameongeza kuwa Serikali itaendelea kujenga mazingira mazuri kwa wafanyabiashara nchini ili waweze kufanya biashara zao ili kujiingizia kipato  binafsi na kukuza pato la Taifa.

Katika hatua nyingine Profesa Mbarawa amekagua sehemu ya kuingilia abiria katika uwanja huo ambapo amesema Serikali itaweka mpango maalum wa muda mfupi kwa wasafiri wanaoenda nje kutotumia muda mrefu katika ujazaji wa fomu wakiwa uwanjani hapo.

“Kwa kushirikiana na taasisi zote zinazotoa huduma katika uwanja huu tutaweka  mpango maalum utakaowezesha wasafiri kuhudumiwa kwa haraka na kwa muda mfupi, Msafiri yoyote anataka huduma za haraka ili waweze kuwahi na sisi tutahakikisho tunakidhi mahitaji ya wateja,” amesisitiza Profesa Mbarawa.

Kwa upande Kaimu MKurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Salim Msangi amesema Mamlaka imeshapitia mikataba yote ya wafanyabiashara kiwanjani hapo na hatua inayofata ni kufatilia madeni yote ili kuboresha huduma katika kiwanja hicho.

Bw. Msangi ameongeza kuwa kwa yale madeni ambayo hayataweza kulipwa kwa wakati taratibu za kisheria zitafuatwa.
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa