Thursday, March 10, 2016

Jamii yatakiwa kuripoti Uhalifu unaofanywa kwa njia ya laini za simu na mitandao.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


Na. Benedict Liwenga-Maelezo.

JESHI la Polisi limewataka wananchi kuwa makini ili kuepukana kutapeliwa fedha na watu wasio waaminifu wanaojipatia fedha hizo kwa njia ya simu na mitandao.

Kauli hiyo imetolewa leo na Msemaji Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Mrakibu Mwandamizi (SSP), Advera Bulimba wakati akiongea na Mwandishi wa Idara ya Habari kwa njia ya simu ambapo amesema kuwa jamii hainabudi kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kuwaibua watu wanaojihusisha na uhalifu kwa njia ya laini za simu pamoja na njia ya mtandao kwa kutoa taarifa mapema katika vituo vya Polisi.

Ameongeza kuwa, watu wanatakiwa kuwa makini kabla ya kutuma pesa kwa watu wanaodaiwa kuhitaji kutumiwa pesa ili kujiridhisha nao na kuepuka kutapeliwa.

‘’Jeshi la Polisi limekuwa likifanyia kazi taarifa zinazotolewa na walalamikaji kwa kuwakamata watuhumiwa na kuwafikisha mahakamani ambapo mpaka hivi sasa tayari kuna baadhi tumewafikisha mahakamani na baadhi wanatumikia vifungo vyao,’’alisema Bulimba.

Aidha, pamoja na juhudi za Jeshi la Polisi katika kjutoa elimu kwa umma kuhusiana na wizi wa mtandao, amevitaka vyombo vya Habari pamoja na wadau wengine kutoa elimu hiyo pia kwa jamii kuhusiana na wizi wa aina hiyo.

‘’Zoezi hili la kuwabaini wahalifu kwa njia ya mtandao ni endelevu ili kupunguza ama kuondoa kabisa uhalifu wa aina hii’’, alisisitiza Bulimba.

Kwa upande wake Meneja Mawasiliano wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Bw. Innocent Mungy amesema kuwa wizi kwa njia ya simu na mitandao ni makosa ya kiuhalifu ambayo yanapaswa kuripotiwa Polisi ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa.

Amesisitiza kuwa watu wasithubutu kutuma fedha kwa watu bila kujiridhisha kwani kuna baadhi ya watu hutumia vitambulisho bandia katika kusajili laini zao za simu na hivyo hutumia kufanyia uhalifu kwa kutuma ujumbe mfupi wa maneno kwa watu kwa lengo la kuomba pesa.

‘’Sisi kama TCRA tunatoa elimu kwa umma ili wananchi waepuke kutapeliwa na pia tunawashauri kuripoti mara moja matukio ya uhalifu kwa njia za simu na mitandao katika vituo vya Polisi kwa uchunguzi na hatua stahiki,’’ alisema Mungy.

Hivi karibuni matukio ya wizi kwa njia ya simu na mitandao yamekuwa yakijitokeza ambapo baadhi ya watu wasiokuwa waaminifu wamekuwa wakituma ujumbe mfupi wa maneno na kuomba pesa kwa ndugu na jamaa ili kujipatia fedha kwa njia ya utapeli.

No comments:

Post a Comment