Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Ni mtu mmoja kati ya watu 20 wenye umri zaidi ya miaka 60, na
mtoto mmoja kati ya watano wenye umri chini ya miaka mitano wanaopata
huduma na matibabu bure, kwa mujibu wa utafiti wa Taasisi ya Twaweza.
Idadi hiyo kwa watu wenye umri zaidi ya miaka 60
ni sawa na asilimi sita tu, wakati idadi ya watoto wenye umri chini ya
miaka mitano ni asilimia 18 tu kwa mujibu wa utafiti huo.
Awali, mpango wa Serikali ni kutoa bure huduma kwa wagonjwa wa nje kutoka makundi hayo mawili.
Taasisi ya Twaweza ilifanya utafiti wake kwa
makundi hayo walioupa jina la Je, Vituo vya Afya Vipo kwa Ajili ya
Kuwahudumia Watu? Wananchi na Watumishi wa Afya Wazungumzia Huduma za
Afya.
Taarifa ya muhtasari huo, kwa mujibu wa Twaweza,
umetokana na takwimu kutoka sauti za wananchi, utafiti kwa njia ya simu
za mkononi na wenye uwakilishi wa kitaifa uliofanyika kwenye kaya zote
Tanzania Bara.
Inasema huduma za afya ni muhimu kwa kuwa
zinahitajiwa na wananchi wengi. Zaidi ya nusu ya Watanzania ambao ni
sawa na asilimia 57, waliotembelea vituo vya afya kati ya Mei na Juni
2013, walikwenda kwenye vituo hivyo kwa dhumuni la kutibiwa au
kumsindikiza mgonjwa.
Waliohojiwa ambao ni sawa na asilimia 77, walitembelea zaidi vituo vya afya vya Serikali kuliko vya binafsi au vya dini.
Wengine ambao ni sawa na asilimia 63 wanaamini
kuwa Serikali inashughulikia vibaya suala la uboreshaji wa huduma za
afya. Upatikanaji wa huduma za afya, pia hutegemea watumishi na
upatikanaji wa dawa.
Taarifa hiyo inasema kuwa Septemba 2013, Sauti za
Wananchi iliripoti kuwa wagonjwa ambao ni sawa na asilimia 41,
hawakupata dawa kwenye vituo vya afya.
Utafiti umebaini pia kuwa zahanati na vituo vya
afya vina upungufu mkubwa wa wafanyakazi na sehemu kubwa vinaendeshwa
vikiwa na nusu ya idadi ya watumishi tofauti na ilivyopendekezwa na
Serikali kwa watumishi wa kada za waganga na wauguzi.
Kwa upande mwingine, theluthi moja ambayo ni sawa
na asilimia 31 ya watoa huduma za afya, hawakuwepo vituoni wakati vituo
hivyo vilipotembelewa na pia ilibainika kuwa hawakutoa taarifa ya
kutofika kwao kazini.
Upungufu wa watumishi walioajiriwa na kutokuwepo
kwao kazini, vinaweza kusababisha wagonjwa kusubiri kwa muda mrefu na
wakati mwingine kupata huduma duni.
Wagonjwa wengine ambao ni sawa na asilimia 70 wanaotembelea
vituo vya afya vya Serikali, wanalazimika kusubiri kwa zaidi ya dakika
30 ndipo wahudumiwe, tofauti na vituo binafsi ambavyo inaelezwa kuwa
nusu ya asilimia 45 ya wagonjwa husubiri kwa muda huo huo.
Vilevile, wagonjwa ambao ni sawa na asilimia 53 ya
wagonjwa wote wanaotembelea vituo mbalimbali vya afya, hulazimika
kusafiri kwa zaidi ya dakika 30 kukifikia kituo cha afya.
Akizungumzia hali hiyo, Elvis Mushi, mtafiti
kutoka Twaweza alisema: “Wagonjwa wananyimwa haki zao za kupata huduma
kikamilifu za kiafya kutokana na uhaba wa dawa muhimu, upungufu wa
wafanyakazi na utoro wa watumishi.”
Naye mkuu wa taasisi ya Twaweza, Rakesh Rajani alisema kuwa wazee na watoto wanaumia kwa sababu Sera hazitekelezwi.
Chanzo:Mwananchi
Chanzo:Mwananchi
No comments:
Post a Comment