Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imesema kupanda kwa gharama za
kampuni iliyoshinda tenda ya kuleta nchini mashine za kisasa za
kuandikisha wapigakura za Biometric Voters Registration (BVR) inatokana
na idadi ya mashine hizo kuongezeka kutoka 12,000 hadi 15,500.
Mashine za BVR zitaanza kutumika Septemba mwaka
huu katika uboreshaji wa daftari la kudumu la wapigakura likakalofanyika
kwa muda wa wiki mbili.
Awali, gharama za ununuzi wa mashine hizo ilikuwa
Sh78 bilioni lakini baada ya kampuni iliyoshindwa tenda hiyo kukata
rufaa katika Mamlaka ya Rufani za Manunuzi ya Umma (PPAA), NEC iliibuka
na kueleza kuwa gharama hizo zimepanda hadi Sh 117 bilioni.
Akizungumza jana katika mkutano kati ya Tume hiyo
na vyama vya siasa, Mkurugenzi wa Ununuzi na vifaa wa NEC, Gregory
Kaijage alisema katika awamu ya kwanza, NEC ilipanga kununua mashine
12,000 lakini kutokana na tume hiyo kuamua kuongeza vituo vya
kujiandikishia wapigakura, walilazimika pia kuongeza idadi za mashine
hizo.
“Uandikishaji utafanyika katika vituo vilivyopo
katika ngazi ya vitongoji, vijiji na mitaa. Kwa utaratibu huu vituo
vimeongezeka kutoka 24,919 hadi 40,015 ili kuwarahisishia wananchi
waweze kujiandikisha kwa wingi” alisema Kaijage.
Kaijage alisisitiza kuwa sababu nyingine za
kuongezeka kwa gharama zimetokana na kuanzishwa kwa ofisi za kanda, na
ufungwaji wa vifaa katika vituo mbalimbali.
Naye Mwenyekiti wa NEC, Jaji Damian Lubuva alisema
hadi itakapofika siku ya Uchaguzi Mkuu mwaka 2015 wananchi watakaokuwa
wamejiandikisha kwa ajili ya kupiga kura watakuwa 23,971,467, ukiondoa
wale ambao wanakadiriwa kuwa watakuwa wamefariki.
“Idadi hii itahusisha wote waliokuwa na miaka 15,
16 na 17 mwaka 2012 ambao watakuwa wamefikisha umri wa miaka 18 mwaka
2015,” alisema Jaji Lubuva.
Hata hivyo, viongozi wote wa vyama vya siasa
waliohudhuria mkutano huo waliilalamikia NEC kwa kutenga muda mfupi wa
wiki mbili kwa ajili ya kuandikisha wapigakura.
Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa
Ibrahim Lipumba alisema muda huo ni mfupi, huku akitolea mfano mikoa ya
Lindi na Mtwara ambayo kumezuiwa kufanyika kwa mikutano ya hadhara,
hivyo wananchi wa maeneo hayo hawataweza kupewa elimu na vyama vyao
kuhusu kazi hiyo kama ilivyoshauri NEC.
Profesa Lipumba pia alihoji kiasi cha Sh 263
bilioni kilichopangwa kutumiwa na NEC katika kazi hiyo, wakati tume hiyo
katika Bajeti ya mwaka 2014/15, imetengewa Sh 7 bilioni tu.
Makamu Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi Leticia Ghati
alisema licha ya muda kuwa mfupi pia wananchi hawakupewa elimu yoyote na
kwamba kwa muda uliobaki hautoshi kwa elimu hiyo kutolewa
Katibu Mkuu Chadema, Dk Wilbroad Slaa naye aligusia sakata la
Mtwara na Lindi, kusisitiza kuwa muda ni mfupi kwa ajili ya utekelezaji
wa kazi hiyo.
Mwenyekiti wa Tadea, Lifa Chipaka, Naibu Katibu Mkuu wa DP pamoja na Katibu Mwenezi wa TLP nao waliitaka NEC kuongeza muda huo.
Akijibu hoja hiyo, Jaji Lubava alisema muda huo unatosha kutokana na kuongezeka kwa vituo vya uandikishaji.
Chhanzo:Mwananchi
Chhanzo:Mwananchi
No comments:
Post a Comment