Na Abushehe Nondo na Beatrice Lyimo-MAELEZO
Dar es Salaam
Serikali
kupitia Wakala wa Misitu Tanzania imewataka watendaji kuanzia ngazi ya
kijiji kupanda miti takribani kiasi cha hekta 185,000 za miti kwa mwaka
ili kukabiliana na changamoto ya upungufu wa misitu nchini.
Hayo yamesemwa leo na Mkurugenzi wa Mipango na Matumizi ya Rasilimali, Wakala wa Misitu Tanzania Bw. Mohamed Kilongo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utaratibu wa uvunaji na usafirishaji wa mazao ya misitu.
Alisema kuwa ifikapo mwaka 2030 upungufu wa misitu utakuwepo endapo
serikali haitatekeleza mkakati wa upandaji wa miti, hivyo kuwataka
watendaji hao kutekeleza mkakati wa upandaji wa miti uliowekwa na Wakala
wa misitu.
“Tumekubaliana
katika mkakati wa kitaifa kuwa kila wilaya kupanda miti Milioni 1.5
kila mwaka ili kuondokana na tatizo la upungufu wa misitu nchini ifikapo
mwaka 2030” Alifafanua Bw. Kilongo.
Aliongeza
kuwa upungufu huo unatokana na kichocheo cha uvunaji haramu na holela
ndani ya misitu ya hifadhi, mapori ya akiba na hata ndani ya hifadhi za
taifa hivyo kuwataka wavunaji wa mazao ya misitu kufuata sheria na
taratibu zilizopo.
Naye Kaimu Mtendaji Mkuu wa Wakala wa huduma za Misitu Prof. Dos Santos Silayo alisema kuwa endapo wavunaji na wasafirishaji wa mazao ya misitu watatumia taratibu za uvunaji na usafirishaji wa mazao hayo itasaidia kuongeza pato la taifa.
“Vyombo
vyote vitakavyohusika na kusafirisha mazao ya misitu ni lazima viwe
wazi ili ukaguzi ufanyike kwa urahisi na ufanisi ambapo kila
atakayesafirisha mazao ya misitu anapaswa kusimama kwenye kizuia kwa
ajili ya ukaguzi”alisema Prof Silayo.
Mbali
na hayo Wakala wa Misitu Tanzania imejipanga kutoa mafunzo maalumu kwa
wananchi juu ya uhifadhi, uvunaji,usafirishaji, usimamizi na utunzaji wa
mazao ya Misitu.
MWISHO
0 comments:
Post a Comment