Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » SUMAYE ATAJA TISHIO LA AMANI NCHINI

SUMAYE ATAJA TISHIO LA AMANI NCHINI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

WAZIRI Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye, amesema tofauti ya kipato ambayo imeanza kujitokeza nchini baina ya matajiri wachache na wenye madaraka kwa upande mmoja na maskini walio wengi kwa upande wa pili si dalili nzuri na ameshauri kudhibitiwa mapema kabla haijaleta madhara makubwa nchini.

Sumaye alitoa kauli hiyo mjini Arusha jana katika Mkutano Mkuu wa Dayosisi ya Kaskazini Kati ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) uliofanyika katika Sekondari ya PeacHouse.

“Hali hii ni ya hatari sana kwa amani na utulivu wa taifa lolote kwa sababu walio wengi hawatavumilia kuona watu wachache wakiishi katika anasa za kutisha, wakati walio wengi hawamudu hata mahitaji ya lazima kwa maisha kama vile chakula, matibabu, maji nakadhalika,” alisema Sumaye na kuongeza;

“Tofauti hii imeleta vurugu katika nchi nyingi na kuathiri amani na utulivu, hapa kwetu hali hii ipo na dalili isiyo nzuri hivyo inahitajika kudhibitiwa kwa haraka kabla haijaleta madhara makubwa kwa taifa letu.”

Alisema maskini kwa walio wengi kwa upande wa pili husababishwa na mfumo mbaya wa uchumi na ubinafsi uliokithiri usiojali binadamu wengine.

Alifafanua kwamba umoja ni muhimu kwa amani na utulivu wetu, na pale ambapo umoja haupo hata maendeleo huwa duni sana. Alisisitiza kwamba bila umoja hakuna moyo wa uzalendo wa mtu kuipenda nchi yake na watu wake.

“Moyo wa uzalendo humfanya mtu kuipenda na kuitumikia nchi na watu wake kwa upendo wa dhati na kuweka masilahi ya taifa na umma mbele badala ya masilahi yake binafsi,” alisema Sumaye.

Aliongeza kwamba sababu mojawapo ya kukosa maendeleo katika bara la Afrika ni kukosekana kwa umoja.

Alisema kwa sasa viongozi wa kiroho wana kazi kubwa kuliko huko kipindi cha nyuma. “Leo nchi yetu ina matatizo makubwa ya maadili kuanzia vijana hadi wakubwa. Matatizo mengi tunayoyazungumza na yanayowakabili jamii kwa sehemu kubwa ni kutokana na upungufu wa maadili. Je katika upungufu huu wa maadili ya jamii viongozi wa kiroho mna nafasi ipi ya kudhibiti mambo haya?” Alihoji Sumaye.

Sumaye aliongeza kuwa ni jukumu la viongozi wa ngazi na aina zote kushirikiana katika kuelimisha jamii kuondokana na maovu haya.

Alisema viongozi wote kila mmoja kwa eneo lake na wote kwa pamoja lazima wapige vita maovu mbalimbali ndani ya jamii yetu ya Watanzania. Umoja wetu katika jambo hili ndiyo nguzo kuu ya mafanikio yetu. “Tujenge maadili mema katika jamii ili upendo wa watu kujali binadamu wenzao udumu na heshima kwa binadamu iwepo. Tukiwa wamoja tutashinda ili Tanzania iwe nchi ya raha,” alisema Sumaye.

Akizungumzia umoja, Sumaye alisema ni nguzo muhimu sana kwa nchi. Alisema nchi yenye umoja baina ya watu wake huwa katika hali ya utulivu zaidi kuliko zile ambazo zina migawanyiko ndani yao.

Alisema mifano ni mingi ya nchi ambazo zimeingia katika hali ya uvunjivu wa amani hata kupigana wenyewe kwa wenyewe kwa sababu hakuna umoja baina ya watu wake na kila upande ukipigania kuudhulumu upande mwingine au kunakuwa na chuki zimejengeka baina ya pande zinazohusika.

“Chuki hizi zinaweza kusababishwa na sababu za kisiasa, ukabila, udini, uchumi na sababu nyinginezo nyingi,” alisema na kuongeza; “Katika siasa tofauti hizi huweza kutokea pale ambapo upande mmoja huhisi kuwa unadhulumiwa au unaonewa katika maamuzi ya kisiasa hasa nyakati za kampeni, upigaji kura na wizi wa kura,” alisema na kuongeza;

“Wakati mwingine hali hii hutokea kwa upande moja kukataa tu kushindwa hata kama wameshindwa kwa halali. Jambo hili la kisiasa limeleta fujo nyingi hasa katika nchi nyingi za Kiafrika na kusababisha umwagaji wa damu.”

Alisema kwa bahati nzuri bado haijakumbwa na kadhia hiyo lakini ni eneo la kulitupia jicho sana lisije likaathiri amani na utulivu. “Ni lazima shughuli zetu za siasa zifuate sheria na taratibu zilizowekwa kwa uwazi bila kutiliwa shaka na upande wowote,” alisema na kuongeza;

“Haki ni lazima isimamiwe kikamilifu nyakati zote za kapeni hadi upigaji wa kura, kuhesabu kura na hata kutangaza matokeo.” Alitaja eneo lingine la hatari sana ni chuki za kidini au zinazotokana na imani za watu. Alisema vita vyote havina macho, lakini vita vya kidini ni vibaya zaidi na huishia kuuana bila kuwa na mshindi.

“Nchi yetu hatujawa na tatizo kubwa na jambo hili lakini hatuko salama sana. Kumekuwa kukitokea chokochoko za hapa na pale zenye sura ya imani. Hapo upendo na uzalendo vimepungua na kuathiri umoja wetu,” alisema na kusisitiza kwamba;

“Tukiwa wamoja hili halina nafasi kwa sababu hakuna dini inayofundisha chuki kwa binadamu mwenzako. Ni lazima tukubali kuwa nchini mwetu kila mtu ana uhuru wa kuabudu dini aitakayo ili mradi havunji sheria za nchi.

“Viongozi wetu wa dini mbalimbali ni bora wakasimamia vyema waumini wao ili nchi yetu isije ikakumbwa na balaa la vurugu za kidini jambo ambalo ni la hatari sana kwa amani na usalama wa nchi na watu wote. Ni vyema tudumishe upendo ili umoja wetu uendelee kudumu.”

Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa