HECHE: MADHILA YA UCHAGUZI YALIVYOFIKISHA CHADEMA ‘NO REFORMS, NO ELECTION’



Na Karama Kenyunko Michuzi Tv


SHAHIDI wa tano wa utetezi katika kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu, John Heche, ameieleza Mahakama namna matukio mbalimbali aliyodai kuyashuhudia katika chaguzi yalivyosababisha chama hicho kufikia msimamo wa “No Reforms, No Election” (Bila Mabadiliko, Hakuna Uchaguzi).

Heche, ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa CHADEMA Bara, ametoa ushahidi huo leo Septemba 9, 2026, katika Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Dar es Salaam, mbele ya Jopo la Majaji watatu wakiongozwa na Jaji Dustun Ndunguru.

Akijibu maswali ya Lissu, Heche amesema Desemba 2, 2024, Kamati Kuu ya CHADEMA ilikaa na kujadili masuala mbalimbali yaliyohusu chaguzi, ikiwemo ukiukwaji wa taratibu za uchaguzi, kuenguliwa kwa wagombea wa chama hicho na matukio ya mauaji yaliyohusishwa na chaguzi.

Heche amesema kutokana na hali hiyo, hususani uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa mwaka 2024 na chaguzi nyingine alizoshiriki na kuzishuhudia, chama hicho kiliona kuwa hazikuwa chaguzi za kawaida bali “uchafuzi”, jambo lililopelekea Kamati Kuu chini ya Mwenyekiti wa wakati huo, Freeman Mbowe, kufikia msimamo wa “No Reforms, No Election.”

Amesema mabadiliko yaliyokuwa yakihitajika yalihusisha marekebisho makubwa ya Katiba na sheria, pamoja na kuondoa madaraka makubwa ya Rais katika uundaji wa Tume ya Uchaguzi na uteuzi wa watendaji wa uchaguzi.


SOURCE : MICHUZI BLOG


KIKWETE AHIMIZA TANZANIA NA JAPAN KUIMARISHA USHIRIKIANO KATIKA USALAMA WA CHAKULA NA UCHUMI WA BULUU




 Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, leo amekutana na kufanya mazungumzo na Mtafiti Mkuu wa Taasisi ya Sasakawa Peace Foundation ya Japan, Bw. Masanori Kobayashi, katika ofisi yake ndogo iliyopo Masaki, Dar es Salaam.


Mazungumzo hayo yalilenga kufuatilia utekelezaji wa masuala yaliyoibuliwa wakati wa ziara ya kikazi iliyofanywa huko nyuma na Dkt. Kikwete nchini Japan tarehe 23 hadi 24 Julai 2025.


Katika ziara hiyo, Dkt. Kikwete alikuwa miongoni mwa viongozi mashuhuri sita kutoka Afrika walioalikwa na Serikali ya Japan kupitia taasisi za Sasakawa Peace Foundation na Nippon Foundation. Viongozi hao walishiriki katika kutoa ushauri kuhusu namna bora ya kuimarisha ushirikiano kati ya Afrika na Japan chini ya mwavuli wa Mkutano wa Kimataifa wa Tokyo kuhusu Maendeleo ya Afrika (TICAD).


Mkutano wa tisa wa TICAD ulifanyika baadaye jijini Yokohama, Japan, kuanzia tarehe 20 hadi 22 Agosti 2025.


Katika mazungumzo hayo, Dkt. Kikwete aliishukuru Serikali ya Japan, kupitia Sasakawa Peace Foundation, kwa kuendelea kudumisha ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya Tanzania na Japan, hususan katika kuimarisha mifumo ya uzalishaji na usalama wa chakula pamoja na kuendeleza uchumi wa buluu.


Dkt. Kikwete pia alisisitiza umuhimu wa kuendeleza tafiti na kuimarisha ushirikiano katika matumizi ya teknolojia za kisasa ili kuongeza tija katika shughuli za wavuvi wadogo na ufugaji wa samaki.


Aidha, alihimiza juhudi zaidi zielekezwe katika kukuza kilimo cha mwani kwenye maeneo ya mwambao wa Tanzania, hususan Zanzibar, ili kuongeza uzalishaji, thamani ya mazao na mapato ya wananchi wanaotegemea sekta hiyo.


Kwa upande wake, Bw. Kobayashi alieleza utayari wa Sasakawa Peace Foundation kutumia nafasi na ushawishi wake kuendeleza na kuimarisha zaidi ushirikiano kati ya Tanzania na Japan.

JKCI, King Salman wafanikisha upasuaji wa moyo kwa watoto 16 katika siku tatu

Watoto 16 wenye magonjwa ya moyo wamefanyiwa upasuaji wa moyo katika kambi maalumu inayoendeshwa na wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao kutoka Kituo cha King Salman Humanitarian Aid and Relief Centre ya nchini Saudi Arabia.

 

Kambi hiyo maalumu imekusudia kuwafanyia upasuaji wa moyo watoto 30 wenye matatizo ya matundu kwenye moyo, mishipa ya damu iliyopishana, pamoja na mishipa ya kupeleka damu kwenye mapafu kuziba kwa siku sita.

 

Akizungumza na mwandishi wa habari hii, Daktari Bingwa wa Upasuaji wa moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Felix Shonyela alisema ushirikiano kati ya JKCI na Taasisi ya King Salman kwa kipindi cha miaka 10 umekuwa na mchango mkubwa katika kuongeza idadi ya watoto wenye magonjwa ya moyo walilofanyiwa upasuaji wa moyo nchini.

 

Dkt. Shonyela alisema wazazi na walezi wanapaswa kuwafikisha watoto hospitali mapema pale wanapowagundua kuwa na changamoto za kiafya ili kurahisisha matibabu yao na kupata huduma mapema.

 

Kwa upande wake daktari bingwa mshauri wa magonjwa ya moyo kutoka Kituo King Salman Humanitarian Aid and Relief Centre ya nchini Saudi Arabia , Dkt. Aljohara Hamza, amesema timu hiyo ilianza kutoa huduma mara baada ya kuwasili JKCI na katika siku mbili za Jumamosi na Jumapili imefanikiwa kuwafanyia upasuaji watoto 11.

 

Dkt. Aljohara alisema kituo hicho kitaendelea kufanya kazi kwa weledi na kushirikiana na madaktari wa JKCI kuhakikisha malengo yaliyokusudiwa yanafikiwa na watoto wengi wanapata huduma kupitia kambi hiyo.

 

“Tumefurahishwa na uwezo wa wataalamu wa JKCI katika kutoa huduma bingwa za upasuaji wa moyo kwa watoto, uwezo wao ni tofauti na tulivyoanza kushirikiana miaka 10 iliyopita”, alisema Dkt. Aljohara

 


 

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa