Na: Lilian Lundo – Maelezo
20/05/2016
Balozi
wa kujitolea wa mazingira, Omary Kombe ameiomba Serikali kuwatambua
watu wanaobadilisha taka kuwa bidhaa kwa kuendeleza taaluma hiyo ili
kuinua uchumi na kuondokana na tatizo la uchafu nchini.
Akiongea na waandishi wa habari Mei 18, 2016 jijini Dar es Salaam, Kombe alisema kwamba kwa kuwatambua watu hao, tatizo la taka litakwisha kwa kiwango kikubwa nchini hasa katika jiji la Dar es Salaam.
“Wapo
watu ambao mara nyingi tunawaona kwenye maonyesho mbalimbali kama vile
sabasaba ambao wanauwezo wa kubadili taka kuwa bidhaa za majumbani kwa
mfano, mkaa, mapambo na bidhaa nyingine, ni vizuri Serikali ikawatumia watu hao kuondokana na tatizo la taka nchini,” alisema Kombe.
Aliongeza kwamba mazingira bado ni machafu licha ya serikali ya awamu ya tano kuweka mkazo
katika suala zima la usafi kuanzia ngazi ya familia mpaka Taifa ili
kukabiliana na magonjwa ya mlipuko kama vile kipindupindu.
Kombe
alisema kwamba, tatizo hilo la uchafu litatatuliwa kama watu wenye
uwezo wa kubadilisha taka kuwa bidhaa watatambuliwa na kufanya kazi hiyo
kuwa rasmi.
Aidha alisema kuwa, kwa kubadilisha taka kuwa bidhaa kutapunguza kiwango cha taka nchini, kuongeza ajira pamoja na kuipunguzia Serikali mzigo wa kutenga maeneo kwa ajili ya kuhifadhia taka kila mara.
Usafi
ni kauli mbiu ambayo imeshika kasi awamu hii ya tano ambapo katika
sherehe za Uhuru (Tisa Desemba) Rais Dkt. John Pombe Magufuli aliwataka
watanzania wote kushiriki usafi maeneo yanayowazunguka na vituo vya
jamii kama hospitali, zahanati na vituo vya afya.
0 comments:
Post a Comment