Home » » Serikali yatoa mafunzo kwa watumishi 4,913

Serikali yatoa mafunzo kwa watumishi 4,913


IMG_8278
Afisa Uhusiano wa Chuo cha Serikali za mitaa Bw.Sebera Fulgence akiongea na waandishi wa habari(hawapo pichani) kuhusu mafanikio ya chuo hicho ikiwa ni pamoja na kufanya mafunzo kwa Watumishi wa Serikali  wapatao 4,913,wakati wa Mkutano uliofanyika ukumbi wa Idara ya Habari(MAELEZO) Jijini Dar es Salaam.Kushoto ni Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano toka Ofisi ya Waziri Mkuu,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI) Bi. Rebecca Kwandu.(Picha na Eliphace Marwa-Maelezo).
Chuo cha Serikali za Mitaa, Hombolo Dodoma kimetoa mafunzo kwa Watumishi zaidi ya 4,913 toka 2009 mpaka kufikia Septemba 2013 kwa  Watendaji na Viongozi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa, pia idadi ya walionufaika na mafunzo haya ni kama ifuatavyo:
a)    Wenyeviti wa Vijiji/Mitaa/Vitongoji          3,733
b)    Maafisa Watendaji wa Vijiji/Mitaa  282
c)     Maafisa Watendaji wa Kata 388
d)   Madiwani 327
e)     Wawezesha Mafunzo 52
f)      Maafisa Elimu Sekondari  48
g)    Wahudumu wa Ofisi 20
h)    Wajumbe wa ALAT 18
i)      Wakuu wa Idara 45
Pia Chuo kwa kushirikiana na Taasisi ya Forum syd ya Mwanza, tangu mwaka 2011  kimeweza kutoa mafunzo ya muda mfupi ya Uwajibikaji wa Kijamii (Social Accountability) kwa watumishi na viongozi wa ngazi zote za Serikali za Mitaa pamoja na Asasi za Kiraia, wakiwemo Wenyeviti na Maafisa Watendaji wa vijiji, Vitongoji, Mitaa na Kata, Waheshimiwa Madiwani, Wakurugenzi na wakuu wa Idara na Vitengo,  Wakuu wa Magereza, Mabenki, TAKUKURU, Wakuu wa Wilaya, Makatibu Tawala wa Wilaya na Maafisa Tarafawa Halmashauri za Wilaya za Ukerewe, Magu na Karagwe .
Mwaka 2009  Chuo cha Serikali za Mitaa kiliteuliwa na Serikali kuwa Taasisi Kiongozi ya Mafunzo (Lead Training Institution) katika kuratibu na kusimamia ubora wa mafunzo yatolewayo kwa watumishi katika Mamlaka za Serikali za Mitaa. Kazi hiyo kwa sasa inafanywa na Chuo kwa kushirikiana na wafadhili. Kwa sasa wafadhili ambao  ni JICA na GIZ. Aidha, Mwaka 2012 Chuo cha Serikali za Mitaa kiliteuliwa na Serikali kutoa mafunzo elekezi (Induction Courses) kwa watumishi wote wapya wanaoajiriwa na Mamlaka za Serikali za Mitaa. Jukumu hilo ni kwa mujibu wa Waraka namba 5 wa Utumishi wa Umma wa mwaka 2012.
Aidha, Chuo kwa kushirikiana na OWM TAMISEMI, kiliendesha mafunzo ya Semina elekezi ya Makatibu Tawala wapya wa Mikoa sita (6) ya Tanzania Bara mwezi Mei 2011 na Makatibu Tawala wa Mikoa yote tarehe 4/7/2011 hadi tarehe 13/7/2011.
Mafunzo haya yamekuwa yakifanyika hapa Chuoni na Mengine kwenye Mikoa husika ya Watumishi.
Chuo cha Serikali za Mitaa ni miongoni mwa Taasisi zilizoko chini ya OWM-TAMISEMI na kilianzishwa kwa mujibu wa Sheria Na. 26 ya mwaka 1994 (Sura ya 396 toleo lililorejewa mwaka 2002). Lengo kuu la kuanzishwa kwake ni kuziwezesha Mamlaka za Serikali za Mitaa nchini kutoa huduma bora zitakazowajengea wananchi uwezo wa kuimarisha utawala bora, kuondokana na umaskini na kuboresha maisha yao.
Madhumuni mahususi  ya Chuo ni kuchangia katika uwezeshaji wa mchakato mzima wa kupeleka madaraka  kwa wananchi, kujenga na kukuza utawala bora, kukuza uchumi na kuondoa umaskini  katika ngazi  mbalimbali za Serikali za Mitaa hapa nchini.
Chuo hiki kimesajiliwa na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (National Council for Technical Education) ambalo ndilo lenye mamlaka ya kusimamia ubora, viwango na uendeshaji wa Vyuo vya Elimu ya juu na Ufundi visivyo Vyuo Vikuu hapa nchini. 
Majukumu ya Chuo yamegawanyika katika sehemu kuu tatu:-
i)       Kutoa mafunzo ya muda mfupi na mrefu juu ya taaluma, ujuzi, stadi na mbinu za uendeshaji wa Serikali za Mitaa kwa Viongozi na Watumishi walio katika ngazi mbalimbali za Serikali za Mitaa;
ii)     Kutoa mafunzo juu ya mabadiliko yanayohusu Serikali za Mitaa kulingana na Mpango wa Uboreshaji wa Mfumo wa Serikali za Mitaa na;
iii)  Kufanya utafiti na kutoa ushauri kwa Serikali Kuu, Mamlaka za Serikali za Mitaa, Mashirika na watu binafsi juu ya masuala yote yanayohusu Serikali za Mitaa.
Chuo katika kutimiza lengo lake la kuwa ndicho Chuo Kiongozi cha Mafunzo katika Mamlaka za Serikali za Mitaa, kinaendelea na jitihada zake za kuhakikisha kuwa zinawafikia watumishi wote wa Mamlaka  za Serikali za Mitaa kupia mafunzo ya kuwajengea uwezo wao kiutendaji na kitaaluma. Pamoja na jitihada zinazofanywa na Chuo katika utoaji wa mafunzo ya muda mfupi na yale ya Muda mrefu, bado kinakabiliwa na changamoto moja kubwa kutoka Mamlaka za Serikali za Mitaa ni uhaba wa fedha za mafunzo kinachopelekea kutofanyika kwa mafunzo mengi kwa Watumishi  ndani ya Mamlaka za Serikali za Mitaa ambao ndio Wadau Muhimu.

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa