Moja ya matukio yaliyochukua nafasi katika vyombo vya habari
nchini wiki hii ni kukamatwa kwa kundi la vijana wanaoendesha uhalifu
katika maeneo ya Kiwalani na Yombo kwa Limboa, Dar es Salaam
linalojulikana kwa jina la Mbwamwitu au watoto wa mbwa.
Taarifa za Polisi Mkoa Maalumu wa Ilala zinasema
kuwa vijana 14 wanaotuhumiwa kufanya uhalifu huo wamekamatwa na baadhi
yao wamekimbia nje ya Dar es Salaam ambako pia wapo waliokamatwa na
wengine wanaendelea kusakwa.
Mbali ya vijana hao wanaojiita Mbwamwitu, kuna
taarifa za kuwapo kwa makundi mengine ya kihalifu katika Jiji la Dar es
Salaam hususan maeneo ya Tabata Kisiwani, Mabibo, Kigogo na Ilala Boma.
Vijana hao wamekuwa wakiwavamia watu njiani au kuvunja nyumba wakitumia
silaha za jadi na kujeruhi na kupora mali hivyo kusababisha wakazi wa
maeneo hayo kuishi kwa wasiwasi.
Yumkini haya ni maeneo machache tu kati ya mengi
ambayo yamekuwa na vijana wenye tabia hizo chafu na zisizostahili katika
jamii. Tunalitaka Jeshi la Polisi kukaza uzi katika kupambana na aina
hii ya uhalifu kwani ikiachwa iendelee, itakwamisha shughuli nyingi za
kijamii na kimaendeleo katika maeneo husika na uhuru wa wananchi kuishi
kwa amani katika nchi yao utakuwa umetoweka.
Hata hivyo, uhalifu huu wa vijana ni matokeo ya mambo mengi yakiwamo malezi na makuzi.
Kwa upande wa malezi, tunapenda kuwakumbusha wazazi kote nchini usemi wa wahenga kwamba mtoto umleavyo ndivyo akuavyo. Haya
ni matokeo ya malezi ya watoto wetu katika jamii. Watoto hawa waliachwa
bila ya uangalizi wa wazazi au walezi na hata jamii inayowazunguka na
haya ndiyo matunda yake. Kukana wazazi wao na kujiita watoto wa mbwa ni
ushahidi tosha wa malezi mabovu yasiyozingatia maadili.
Kama Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ilala, Marieta
Minangi alinukuliwa na vyombo vya habari akisema, nasi tunasisitiza,
kila familia ijitathmini inavyolea na kudhibiti nidhamu za watoto wake.
Hilo ni jambo la msingi kabisa na kama lingekuwa limefanyika
inavyostahili, tusingekuwa na aina hii ya uhalifu.
Kwa upande wa makuzi, hapa ndipo tunapoliona lile
bomu la ajira likianza kulipuka taratibu. Idadi kubwa ya vijana
wanamaliza shule na kufeli katika ngazi mbalimbali kama vile darasa la
saba, kidato cha nne, cha tano na vyuo. Wanapofeli, wengi wao wanaishia
mitaani ambako hakuna mfumo unaoeleweka wa kuwasaidia.
Kwa mantiki hiyo, tunapenda kutumia fursa ya tukio
hili kuikumbusha Serikali kuchukua hatua madhubuti za kukabiliana na
tatizo hili.
Lazima kuwe na mikakati inayoeleweka kwa vijana
wanaofeli darasa la saba. Watoto hawa wasiachwe tu kama kuku wa kienyeji
mitaani, lazima kuwe na mpango mahsusi wa kuwaendeleza ama kielimu,
kiufundi au kujitegemea, vivyohivyo, kwa wale wanaohitimu kidato cha
nne, sita na hata vyuo.
Kuna msemo kwamba asubuhi yako inaanzia pale
unapoamka, hata kama ni saa saba mchana. Hatuna haja ya kuishia
kujilaumu kwamba tumechelewa, tuanze sasa kupanga mikakati ya kuwasaidia
vijana wetu ili waondokane na aina hii ya maisha.
Tunaamini kwamba kwa kufanya hivyo, siyo tu kwamba
kutatusaidia nasi kuishi kwa amani na utulivu, bali hawa ndio
wanaotegemewa kuwasaidia wazee wao watakapostaafu au kushindwa kufanya
kazi za uzalishaji.
Chanzo;Mwananchia
Chanzo;Mwananchia
0 comments:
Post a Comment