Home » » Pinda kuitia hasara Serikali

Pinda kuitia hasara Serikali

  Sehemu ya Barabara ya Mlandizi- Chalinze, ikiwa imeharibika kutokana magari makubwa kuzidisha uzito na kusababisha uharibifu huo

Dar es Salaam: Uamuzi wa Waziri Mkuu Mizengo Pinda kuruhusu malori makubwa ya mizigo yaendelee kuzidisha uzito wa mizigo, umetajwa kuwa ni hatari na utaisababishia Serikali hasara ya mamilioni ya fedha.
Hasara hiyo inatokana na uharibifu wa barabara za lami ambao unachangiwa kwa kiasi kikubwa na malori yanayozidisha uzito wa mizigo kinyume cha sheria na kanuni namba 7 (3) ya Sheria ya Usalama Barabarani ya 2001.
Ujenzi wa barabara ni wa gharama kubwa na hata ukarabati wake umekuwa ukitengewa mabilioni ya fedha za walipakodi kutokana na uharibifu unaofanywa.
Mathalani katika bajeti yake ya 2013/14, Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, imetenga kiasi cha Sh314.535 bilioni kwa ajili ya mpango wa matengenezo ya barabara kuu na barabara za mikoa.
Kiasi hicho cha fedha ambacho ni zaidi ya robo ya bajeti nzima ya wizara hiyo kwa mwaka, kinatosheleza kujenga barabara mpya ya lami yenye urefu wa kilometa zipatazo 315, kwa makadirio ya kilometa moja kugharimu Sh1 bilioni. Katika mwaka huu wa fedha, bajeti nzima ya Wizara ya Ujenzi ni Sh1.226 trilioni.
Kauli ya Dk Magufuli
Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli, aliwahi kunukuliwa akisema ataendelea kusimamia sheria ya barabara namba 30 ya mwaka 1973, hadi anaingia kaburini kwa kuhakikisha hakuna magari ambayo yanazidisha uzito na kuharibu barabara.
“Nchini Ujerumani, uzito wa magari yote ni tani 40, Uingereza tani 40, Ufaransa 40, Urusi 38 lakini Tanzania tani 56, wakati mwingine tunakamata hadi tani 96,” alisema Dk Magufuli.
Hata hivyo, ujasiri wa Dk Magufuli ulizimwa na amri ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda, aliyetengua agizo la waziri huyo na kuamua kuruhusu magari yenye uzito uliopitiliza kuendelea kutumia barabara.
Wasemaji wa Serikali
Ofisa Habari wa Wizara ya Ujenzi, Martin Ntemo alisema suala hilo wameliachia Ofisi ya Waziri Mkuu. “Hilo suala liko Ofisi ya Waziri Mkuu, siwezi tena kulizungumzia,” alisema Ntemo kwa kifupi.
Hata hivyo, Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Dk Florence Turuka alisema siyo sahihi kusema kwamba Waziri Mkuu amevunja sheria kwani ilikuwa ni lazima serikali ichukue hatua jumuishi kwa kuwashirikisha wadau husika.
“Siyo sahihi kusema kuwa tunataka kuvunja sheria, sisi tumepokea mapendekezo na tutayaangalia kabla ya kutoa ripoti. Wewe vuta subira tu,” alisema Dk Turuka.
Dk Turuka alisema kamati iliyoundwa na Serikali ikiwajumuisha wadau mbalimbali wa barabara ilikamilisha kazi yake Desemba mwaka jana na kwamba hivi sasa Serikali inatafakari mapendekezo yaliyotolewa.
“Kamati ilishamaliza kazi tangu Desemba mwaka jana… tulipokea mapendekezo kwa sababu ile ilikuwa kamati jumuishi, kulikuwa na watu wa Tatoa, Taboa na Wizara ya Ujenzi na wataalamu, na sasa tunayafanyia kazi,” alisema Dk Turuka.
Baadhi ya barabara ambazo zilikuwa katika hali nzuri hivi sasa zimeharibika vibaya chanzo kikiwa ni uzito wa magari ya mizigo. Miongoni mwa hizo ni Barabara Kuu ya Morogoro - Dodoma kati ya Kijiji cha Magubike na Mji wa Gairo pamoja na Barabara ya Dar es Salaam ya Morogoro eneo la kati ya Mlandizi na Chalinze.
Hali hii ndiyo iliyomsukuma Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli kufuta waraka unaoruhusu magari ya mizigo kuzidisha uzito na badala yake kutaka sheria inayotaka malori yanayozidisha uzito uliopo ndani ya asilimia tano kupunguza mzigo, kupanga mzigo upya au kulipia uzito uliozidi mara nne ya tozo ya kawaida, ifuatwe.
Uamuzi wa Dk Magufuli ulipingwa na wamiliki wa magari makubwa ya mizigo na kuungwa mkono na wamiliki wa mabasi ya abiria, hivyo Waziri Mkuu Pinda aliingilia kati na kuamuru utaratibu wa awali uendelee, ilhali suala hilo likiwa linatafutiwa ufumbuzi wa kudumu.
Hata hivyo, Pinda alitangaza uamuzi wa kusitishwa kwa utekelezaji wa amri ya Dk Magufuli katika mkutano ambao hata hivyo waziri huyo wa sekta husika hakuhudhuria. Wakati huo kulikuwa na tishio la kusitishwa kwa usafirishaji nchi nzima kama amri hiyo isingetenguliwa.
Chanzo cha habari ndani ya Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) kinasema: “Tatizo kuna viongozi wengi wenye malori na mabasi ndiyo wanaokwaza utekelezaji wa sheria hiyo.”
Kiliongeza: “Utakuta mtu ana magari hadi 300 na yote yanazidisha uzito kwenye barabara kwa kisingizio cha kusamehewa asilimia tano, unadhani barabara zetu zitaishia wapi? Ndiyo maana Dk Magufuli kwa uchungu aliamua kuweka msimamo”.
Takwimu za vipimo
Takwimu za upimaji wa magari ambazo ziko kwenye tovuti ya wakala huyo wa barabara nchini zinaonyesha kuwa licha ya kuwepo nafuu katika sheria bado magari mengi yamekuwa yakizidisha uzito.
Mathalan 2011/12 magari 684,600 yalipimwa na kati ya hayo, 167,310 sawa na asilimia 24.44 yalikutwa yakiwa yamezidisha mizigo, huku mengine 8,856 sawa na asilimia 1.30 yalipitisha kiwango cha asilimia tano.
Chanzo;mwananchi

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa