Home » » TPA, TICTS lawamani kwa kuzorotesha uchumi

TPA, TICTS lawamani kwa kuzorotesha uchumi

Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe
 
Kampuni ya kupakua na kupakia makontena bandarini (TICTS) na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) zimetupiwa lawama na wadau wa bandari mbele ya Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, kuwa chanzo cha kuzorotesha uchumi wa nchi kutokana na uzembe unaofanywa na watendaji wake katika uendeshaji wa shughuli bandarini.
 
Walitoa lawama katika kikao kilichoitishwa jana na Waziri wa Uchukuzi, Dk. Mwakyembe, jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kuzungumzia changamoto zinazoikabili bandari na idara zote zinazofanya kazi katika bandari hiyo.
 
Walimweleza Dk. Mwakyembe kuwa kampuni ya TICTS imekuwa ikichelewesha utoaji wa makontena ya wateja bandarini katika kipindi cha siku 15 ambazo zipo kisheria na baada ya hapo mteja anaambiwa atoe gharama ambazo ni Dola za Marekani 100.
 
Walisema wateja wanatozwa kiwango hicho na TICTS bila kujali kuwa mfumo wa ufuatilia wa mizigo ujulikanao kama "Cargo Management System" ulioanzishwa na TRA umegoma kufanya kazi jambo ambalo linawawia vigumu katika utendaji kazi.
 
“TICTS wanachelewesha makontena kwenda bandarini na mteja analazimika kulipa gharama za kutunza mzigo ambazo kama kontena lingeweza kutolewa ndani ya siku 15 baada ya kuwasili kutoka nje mteja asingeweza kuingia gharama hizo,” walisema.
 
Wadau hao pia waliitupia lawama TRA kutokana na mfumo wake mpya wa ufuatiliaji mizigo bandarini kuwa na usumbufu kutokana na wakati mwingine kushindwa kufanya kazi hadi siku saba.
 
Walisema hali hiyo imekuwa ikisababisha wateja hususani wanaotoka nje ya nchi kuingia gharama kubwa wakisubiri mizigo yao kutoka bandarini na mwisho wa siku wanalazimika kukimbia kuitumia bandari ya Dar es Salaam na kukimbilia bandari nyingine ambazo hazina urasimu.
 
Meneja kituo wa TICTS, Donald Talawa, alisema tatizo la ucheleweshaji wa makontena bandarini limetokana na ongezeko la mizigo kutoka makontena 600 hadi kufikia 800 katika kipindi cha Desemba mwaka jana na hivi sasa kampuni imejipanga kutatua tatizo hilo.
 
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa