Home » » bunge la katiba: Uteuzi wa Kingunge sasa kizungumkuti

bunge la katiba: Uteuzi wa Kingunge sasa kizungumkuti

image

UTEUZI wa wabunge wa Bunge la Katiba uliofanywa na Rais Jakaya Kikwete, hivi karibuni umezidi kupata upinzani ambapo Jukwaa la Katiba Tanzania linahoji uteuzi wa kada wa CCM, Kingunge Ngombale Mwiru, kupitia kundi la asasi za kiraia, wakati hajawahi kuwa mwanachama wa asasi yoyote.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mjumbe wa Kamati ya Uongozi ya Jukwaa hilo, Hebroan Mwakagenda, alisema nafasi 20 walizokuwa wametengewa asasi za kiraia, majina matano ni ya wanasiasa na makada wa CCM.
Alitolea mfano kwa Kingunge Ngombale Mwiru, akisema ameingizwa kwenye kundi la asasi wakati hajawahi kuwa na asasi wala hawajawahi kumshuhudia hata kwenye msiba wa mwanaharakati mwenzao.
"Watuambie Kingunge wamemtoa wapi na asasi yake ilisajiliwa wapi na inaitwaje... mimi nimekuwa kwenye asasi kwa miaka 22, lakini sijawahi kumwona hata kwenye msiba wa mwanaharakati mwenzetu, sasa iweje leo hii aibukie kwenye kundi la asasi?" alihoji Mwakagenda na kuongeza;
"Huyo ni kada wa siasa wa muda mrefu sasa ameingizwaje kwenye nafasi zetu?" Alimtaja mwingine kuwa ni Elizabeth Minde, akisema licha ya kuwa na asasi, lakini ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kilimajaro.
Alisema jina lake lilitakiwa liwe kwenye kundi la wanasiasa na si kwenye asasi, kwani sheria hairuhusu. Alimtaja mwingine aliyeingizwa kwenye nafasi zao kuwa ni Sixtus Mapunda, ambaye ni Mwenyekiti wa UVCCM.
"Tumefanya uchambuzi wa kina katika hayo majina na tumeagiza wenzetu wa Zanzibar wayachambue ili kujua majina ya wanasiasa ambayo yameingizwa maeneo ambayo si makundi yao," alisema na kuongeza; "Kwa mwelekeo huu kuna uwezekano wa kupata katiba yenye mashaka."
Alisema asilimia 90 ya wabunge wa Bunge la Katiba ni wanasiasa. Alisema tangu awali Jukwaa la Katiba lilitaka Rais Kikwete, asifanye uteuzi huo kwani walijua atateua wanasiasa wenzake ambao wataenda kuteka mchakato wa Katiba Mpya. watu wenye mlengo unaofanana.
Wakati huo huo, jukwaa hilo limeandaa mafunzo ya siku mbili kwa wabunge 201 ambao wamechaguliwa ili kuwapiga msasa na kuwaelekeza hoja za kwenda kuingia nazo bungeni.
Alisema katika mafunzo hayo Profesa Issa Shivji atafundisha namna kujenga hoja kuhusiana na maudhui ya bunge hilo la Katiba, kwani katika bunge hilo hakuna upande wa Serikali, vyama wala waziri.
Kwa upande wake mkurugenzi wa mtadao wa watetezi wa haki za binadamu,Onesmo Olengurumwa, alisema wamesikitishwa sana na Rais Kikwete, kutochagua kundi lao kwani hakuna hata mmoja aliyechaguliwa kwa ajili ya kutetea haki za binadamu.
Alitoa mfano kuwa mauaji yaliyotokea wakati wa Operesheni Tokomeza yalisababisha vifo vya watu wengi na wengine kukosa haki zao za msingi, lakini kwa jinsi Rais Kikwete, alivyofanya uteuzi wa wabunge hao ni wazi kuwa hakuna wa kwenda kuwatetea.
Alisema waliochaguliwa ni kundi kubwa la chama kimoja linaloenda kupitisha katiba hiyo, wakati suala hilo ni la Watanzania wote na si la vyama wala Serikali.

 Chanzo;majira
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa