“ Upanuzi huo ni muhimu sana kufanyika kwa sababu ukikamilika ndiyo 
unaoweza kuweka ushindani na Bandari ya Mombasa, pia itasaidia 
kuiongezea mapato Serikali.”
Zitto Kabwe 
            
Upanuzi wa Gati namba 13 na 14 katika 
Bandari ya Dar es Salaam, uliosababisha kung’olewa kwa aliyekuwa Waziri 
wa Uchukuzi, Omary Nundu, umeendelea kupata vikwazo baada ya kampuni ya 
Kichina iliyopewa zabuni ya upanuzi huo kutofika kwa kazi hiyo.
                
              
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari(TPA), Madeni
 Kipande aliiambia Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali(PAC), 
iliyofanya ziara jana katika bandari hiyo kuwa hatua  hiyo licha ya 
kuwasikitisha imesababisha kuchelewa kwa upanuzi huo.
“Hiyo kampuni ya kichina ilitakiwa iwe imeanza 
kazi tangu Oktoba mwaka jana,  lakini ajabu ni kwamba ipo kimya na 
hakuna mawasiliano ya aina yoyote. Tumeamua kufuta zabuni hiyo, 
tutatangaza nyingine mapema mwezi huu kwa kuwa tunakusudia kwamba, Julai
 tuwe tumeshaanza kazi. Hapa hatutaki siasa zimetuchosha,” alisema 
Kipande.
Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Kabwe Zitto 
aliisisitiza TPA kuhakikisha kwamba zabuni hiyo inatangazwa na 
kukamilika mapema akieleza kuwa kuendelea kuchelewesha kuanza kwa 
upanuzi huo ni kuikosesha mapato Serikali.
“ Upanuzi huo ni muhimu sana kufanyika kwa sababu 
ukikamilika ndiyo unaoweza kuweka ushindani na Bandari ya Mombasa, pia 
itasaidia kuiongezea mapato Serikali,” alisema Zitto.
Kamati hiyo pia ilisisitiza TPA kuhakikisha 
inaanza matumizi ya kupakua mafuta kwa njia ya mita kwa sababu utaratibu
 wa kupima kwa kijiti(Dip Stick) unaikosesha mapato Serikali.
“ Katika hili tumeamua kuunda kamati maalumu, 
itakayofuatilia kwa kina kubaini kwa nini tangu utaratibu huo ulipopaswa
 kuanza kutumika mwaka 2008 umekuwa ukipigwa danadana. Tunahisi kuna 
jambo, inawezekana hata ni hujuma za wafanyabiashara wa mafuta, tutaujua
 ukweli,” alisema Zitto.
Akiwa Waziri wa Uchukuzi, Dk Shukuru Kawambwa kwa 
kushirikiana na Mamlaka ya Bandari, walitafuta mkopo kutoka Serikali ya 
China kupitia Benki ya Exim ya nchi hiyo iliyoridhia kutoa Dola 524 za 
Marekani ili zisaidie upanuzi wa Gati namba 13 na 14 katika Bandari ya 
Dar es Salaam.
Chanzo;Mwananchi
Chanzo;Mwananchi
 
 
 
0 comments:
Post a Comment