Home » » vita ya ujangili: Nyalandu ajipanga kijeshi

vita ya ujangili: Nyalandu ajipanga kijeshi

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

WIZARA ya Maliasili na Utalii, jana imekamilisha mchakato wa kulipa kodi ya ushuru kwa Mamlaka ya Mapato nchini ili kuruhusu upatikanaji wa silaha 500 aina ya AK 47 ili ziweze kukabidhiwa kwa wapiganaji kwenye Hifadhi za Taifa, Mamlaka ya Ngorongoro na Mapori ya Akiba kote nchini ili kupambana na ujangili.
Silaha hizo zilizuiliwa na TRA tangu Novemba 2012 baada ya Wizara hiyo, kushindwa kuzilipia ushuru wa sh. milioni 212 walizokuwa wakidaiwa kama ushuru ili waweze kuzipata.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Bw. Lazaro Nyalandu, aliyasema hayo Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari ambapo kufanikiwa kwa mchakato huo ni utekelezaji wa azimio la Bunge na ahadi ya Serikali kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maliasili, Ardhi na Mazingira.
"Silaha hizi zilinunuliwa kwa gharama ya sh. milioni 427, leo natangaza kuzipandisha hadhi kanda nane zilizopo katika pori la Akiba la Selous ili ziweze kujitegemea kiuendeshaji kwa kuwa na viongozi wake kila kanda.
"Pori la Selous lina ukubwa wa kilometa za mraba 55,000 unaokaribia Hifadhi zote za Taifa nchini zilizopo chini ya TANAPA, ambazo zina ukubwa wa kilometa za mraba 57,000," alisema Bw. Nyalandu.
Aliongeza kuwa, Mhifadhi Benson Kibonde ataendelea kuwa Meneja wa pori lote la Selous kama ilivyo sasa akisaidiwa na wakuu nane wa kanda.
Wakuu hao ni Msafiri Mashiku (Kanda ya Matambwe), Asterius Ndunguru (Msolwa), Adili Zella (Liwale), Bigilamungu Kagoma (Kingupira), William Millya (Kalulu), Munhu Ndunguru (Miguruwe), Ramadhani Mkhofoy (Ilonga) na Msiba Kombo (Likuyu- Sekamaganga).
Bw. Nyalandu alisema Wizara yake pia imechukua hatua za kuimarisha kikosi cha kupambana na ujangili nchini (KDU), katika kanda nane zikiongozwa na wakuu wake.
Aliwataja wakuu hao kuwa ni Paskal Mrina (Kanda ya Kaskazini- Arusha), Faustine Masalu (Mashariki-Dar es Salaam), John Mbwiliza (Serengeti-Bunda), Benjamin Kijija (Kanda ya Ziwa- Mwanza) na Charles Msilanga (Magharibi-Tabora).
Wengine ni Keneth Sanga (Kanda ya Kati-Manyoni), Majid Lalu (Nyanda za Juu Kusini-Iringa) na Ibeid Mmari (Kusini-Songea).
Alisema katika kuimarisha ulinzi wa tembo na mapambano dhidi ya ujangili katika Pori la Akiba la Selous, aliishukuru Frankfurt Zoological Society kwa kuwapa magari matano aina ya Land lover.
Magari hayo yatapelekwa katika kanda za Matambwe, Msolwa, Kiwale, Kingupira, Kalulu na kuongeza kuwa, Mfuko wa Wanyamapori umenunua magari 14 aina ya Toyota yenye thamani ya sh. bilioni 1.63.
Katika hatua nyingine, Bw. Nyalandu amemteua Bw. Nurdin Chamuya kuwa msemaji wa Wizara hiyo akichukua nafasi ya Bw. Chikambi Rumisha ambaye anarudi katika idara yake ya Sera na Mipango.
"Wizara yangu inachukua hatua mahususi kuwajengea uwezo watumishi wake na askari wanyamapori ili kushinda vita kubwa ya ujangili nchini," alisema Bw. Nyalandu.

Chanzo;majira

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa