Home »
» KESI YA PINDA KUUNGURUMA TENA LEO MAHAKAMA KUU
KESI YA PINDA KUUNGURUMA TENA LEO MAHAKAMA KUU
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
MAHAKAMA
Kuu, Kanda ya Dar es Salaam, leo inatarajia kuendelea kusikiliza kesi
ya kikatiba inayomkabili Waziri Mkuu, Mizengo Pinda , iliyofunguliwa na
Kituo cha Msaada wa Kisheria na Haki za Binadamu (LHRC) kwa kushirikiana
na Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS).
Katika kesi hiyo namba 24
ya mwaka 2013, LHRC na TLS,wanadai Pinda alivunja Katiba kutokana na
kauli aliyoitoa Bungeni, akiagiza vyombo vya dola kuwapiga wale ambao
watakaidi kutii sheria zinazotolewa na vyombo husika. Walalamikaji
wanadai kuwa amri kwa vyombo vya utekelezaji wa sheria kuwapiga wananchi
ni kinyume na katiba.
Hata hivyo, Pinda na Mwanasheria Mkuu wa
Serikali (AG) aliyeunganishwa katika kesi hiyo waliweka pingamizi la
awali, pamoja na mambo mengine wakidai kuwa walalamikaji na watu
walioorodheshwa katika kesi hiyo hawana mamlaka kisheria kumfungulia
kesi.
Kabla ya kesi hiyo kuahirishwa, mwaka jana, Naibu Mwanasheria
Mkuu wa Serikali (DAG), George Masaju, aliieleza Mahakama Kuu kuwa kesi
ya kikatiba inayomkabili Waziri Mkuu, Pinda ni batili, hivyo inapaswa
kufutwa.
Masaju, alisema hayo wakati alipokuwa akiwasilisha
pingamizi la awali la Pinda ,ambapo alisema sheria zinamlinda Waziri
Mkuu kutoshtakiwa wala kuhojiwa na chombo chochote juu ya kauli
aliyoitoa Bungeni.
Katika pingamizi hilo, DAG Masaju alidai kesi
hiyo ni batili na iko mahakamani isivyo halali kwa kuwa inakiuka Katiba
ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1977 na Sheria ya Mamlaka, Kinga na Haki
za Wabunge ya mwaka 1988. Akifafanua hoja hizo, DAG Masaju alisema
Pinda analindwa na Katiba Ibara ya 100 (1) na (2)
Akinukuu ibara
hizo, alisema ibara ya kwanza inaeleza kuwa kutakuwa na uhuru wa mawazo
na majadiliano bungeni, ambao hautavunjwa wala kuhojiwa na chombo
chochote, au katika mahakama yoyote nchini.
Ibara ya pili inaeleza
kuwa mbunge yeyote hatashtakiwa au kufunguliwa shauri la madai
mahakamani kwa jambo lolote alilosema, au alilolitenda, au
alililoliwasilisha bungeni kwa njia ya maombi, mswada, hoja au
vinginevyo. “Msingi wa shauri hili unatokana na jambo lililosemwa
Bungeni na mmoja wa wabunge wakati wa shughuli za bunge.”
Kwa upande
wake Wakili wa Serikali, Gabriel Mlata, alisema kesi hiyo ni batili
kuwepo mahakamani kwa kuwa walioifungua wamekiuka utaratibu wa
uwasilishaji wa mashauri kama hayo kwa mujibu wa amri na kanuni za
uendeshaji wa mashauri ya madai.
Chanzo:Majira
0 comments:
Post a Comment