Home » » MVUTANO MKALI WATOKE BAINA YA SERIKALI BUNGE

MVUTANO MKALI WATOKE BAINA YA SERIKALI BUNGE

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

Sasa ni dhahiri kwamba kuna msuguano wa wazi kati ya mihimili miwili ya dola, Bunge na Serikali, kuhusiana na hatua ya Serikali kuchelewa kutekeleza maazimio ya Bunge.
Msuguano huo umeshika kasi wiki hii baada ya Serikali kuwarudisha kwenye nyadhifa zao vigogo wawili wa Wizara ya Maliasili na Utalii ambao hivi karibuni waliondolewa na Waziri Lazaro Nyalandu, huku wabunge wakiapa kuibana Serikali kuwang’oa viongozi hao.
Vigogo hao ni pamoja na Mkurugenzi wa Wanyamapori, Profesa Alexander Songorwa na Mkurugenzi Msaidizi, Jaffar Kidegesho kwa madai ya kutowajibika ipasavyo katika vita dhidi ya ujangili nchini.
Mbali na sababu hiyo, lakini Nyalandu alikaririwa akisema alichukua uamuzi huo ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa mazimio 16 ya Bunge, yaliyotolewa baada ya taarifa ya Operesheni Tokomeza Ujangili.
Ikulu yatoa tamko
Wakati mvutano huo ukiendelea, Ikulu imeitaka wizara hiyo kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za kumfukuza mtu kazi.
Katibu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue alisema kuzingatiwa sheria, kanuni na taratibu za kumfukuza mtu kazi ndiyo suluhisho la msuguano unaoendelea kati ya Waziri Nyalandu na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Maimuna Tarishi juu ya hatima ya wakurugenzi hao ambao walitimuliwa kazi Februari mwaka huu.
Balozi Ombeni aliwataka viongozi hao kuhakikisha kuwa uamuzi wowote wanaoufanya kuhusu kuwaondoa kazini watumishi hao unazingatia sheria, taratibu na kanuni kwa kuwa zinaeleza wazi hatua zinazopaswa kuchukuliwa.
“Siwezi kujua kwa nini wanaendelea kuvutana, hilo waulize wao, ninachojua wanatakiwa wazingatie sheria, kanuni na taratibu katika jambo hilo,” alisema.
Alipoulizwa ni nani kati ya Nyalandu na Tarishi hafuati sheria za utumishi wa umma, alisema: “We mwenyewe nenda kazisome (sheria) utajua tu.”
Kwa mujibu Sheria ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2002, Kifungu cha IV (23) (2) inayozungumzia mamlaka ya Rais kumwondoa mtumishi aliyemteua kazini, amri ya kumfukuza mtumishi wa umma itatekelezwa iwapo
(a)hati ya mashtaka imeandikwa dhidi yake
(b)mtumishi wa umma amepewa nafasi ya kujibu mashtaka hayo
(c)Maombi yametolewa kwenye hati ya mashtaka kwa mujibu wa taratibu zilizo chini ya kifungu namba 34.
Ripoti ya uchunguzi wa matatizo katika utekelezaji wa Operesheni Tokomeza Ujangili, azimio namba saba lilimhusu Profesa Songorwa kwa jina lake na cheo chake likitaka Serikali kumwajibisha kwa kuudanganya umma kuhusu mazingira na kifo cha Emiliana Marrow wa Babati.
Uchunguzi wa madaktari huru na picha za mwili wa marehemu, zilionyesha alikufa kwa kuteswa na askari waliotekeleza Operesheni Tokomeza Ujangili, lakini taarifa ya Profesa Songorwa ikasema alikufa kwa Pressure (shinikizo).
“Bunge linaazimia Serikali ichukue hatua za kumwajibisha mkurugenzi wa wanyamapori kwa kuudanganya umma na kujaribu kuficha ukweli,” linasomeka azimio hilo la Bunge la Desemba 20.
Hata hivyo, baada ya Nyalandu kumwajibisha Profesa Songorwa na mwenzake, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Maimuna Tarishi aliwarejesha kazini akidai kukiukwa kwa sheria za utumishi wa umma.
Wabunge mbalimbali waliohojiwa jana, walidai kinachoonekana kinatoa taswira kwamba Serikali inalitunishia misuli Bunge kila mara linapotoa maazimio ya kuwawajibisha watumishi wa umma.
Kwa mujibu wa Wabunge hao, siyo mara ya kwanza hali inayotokea sasa ndani ya Wizara ya Maliasili kutokea serikalini, kwani mazingira kama hayo yalitokea pia Wizara ya Nishati na Madini.
Mwaka 2011, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, David Jairo alirudishwa kazini baada ya kusimamishwa kazi kutokana na kutuhumiwa bungeni kuchangisha zaidi ya Sh50 milioni ili zisaidie kupitisha bajeti.
“Yanayotokea sasa Maliasili ni kama yaleyale yaliyotokea Nishati na Madini… Inaonekana kama ni sinema vile, tunapitisha (Bunge) maazimio lakini Serikali haitaki kuyatekeleza,” alidai mbunge mmoja.
Waziri Kivuli Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), David Silinde alisema kinachotokea Wizara ya Maliasili na Utalii ni mwendelezo wa Serikali kupuuza maazimio ya Bunge.
“Hata kwenye Hazina tulitaka TPDC (Shirika la Maendeleo ya Petroli) libakie na asilimia 100 ya makusanyo lakini mpaka sasa Serikali imepuuza na inalipa asilimia 50 tu,”alidai Silinde.

Silinde aliongeza kusema, “ Hii ni tabia inayoanza kujengeka na sisi kama wabunge hatupaswi kuiacha izoeleke kwa hiyo mimi ni mmojawapo ambaye nitalihoji hili Bunge la bajeti wiki ijayo.”
Kwa mujibu wa Silinde, mpango wake huo unaungwa mkono na wabunge wengine na kwamba watataka maazimio yote yaliyokwishaazimiwa na Bunge yawekewe kikomo cha utekelezaji.
Mbunge wa Bunda, Alphaxard Kangi Lugola ambaye alikuwa mwiba kwa Serikali na kuchangia mawaziri wanne kujiuzulu, alisema ameshtushwa na taarifa za kurudishwa kazini kwa vigogo hao.
“Mimi ndiyo kwanza niko uwanja wa ndege narejea sijasikia kama wamerejeshwa, lakini kama ni kweli basi kuna tatizo ila subiri nithibitishe hili ili nikisema niseme nikiwa na uhakika,”alisema Lugola.
Mbunge wa Viti Maalumu, Lucy Owenya, alisema kilichofanywa na Serikali kuwarudisha vigogo hao kimejenga mazingira mabaya ya utendaji kazi kati ya Nyalandu, Tarishi na vigogo hao.
“Huku ni kumdhalilisha Nyalandu kwa sababu hata kama angekuja waziri mwingine yeyote ni lazima atekeleze maazimio hayo ya Bunge… kama kuna kasoro wazirekebishe lakini wawajibishwe,”alisema.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, James Lembeli alisema maazimio hayo hayakuwa yake kama Lembeli wala ya kamati bali yalikuwa ni ya Bunge zima.
“Hayo yanayotokea huko Maliasili nisingependa kuyazungumzia ila ninachoweza kusema maazimio ya kuwawajibisha watendaji hao yalikuwa ni ya Bunge zima na bado yanasimama kama yalivyo,”alisema.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa