Home » » WABUNGE WAJA JUU,UUZWAJI WA HISA UDA

WABUNGE WAJA JUU,UUZWAJI WA HISA UDA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Uuzwaji wa hisa za Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA) jana uliibuka upya bungeni baada ya Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (Chadema) kuhoji sababu za Serikali kufuta kesi kuhusu utata wa mauzo hayo.
Suali la UDA limeibuka katika kipindi ambacho ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) imebainisha ukiukwaji mkubwa wa taratibu katika mauzo ya hisa za shirika hilo ambazo zilipaswa kuuzwa na Shirika Hodhi la Mali za Serikali (CHC), badala ya bodi ya shirika.
CAG Ludovick Utouh anasema katika taarifa yake kuwa, baada ya kugundua ukiukwaji huo wa sheria aliishauri Bodi ya UDA kutouza hisa hizo, lakini alipuuzwa.
“Bodi ya wakurugenzi wa UDA iliendelea na uuzaji wa hisa bila kupata kibali cha Serikali na hata CHC,” inasema sehemu ya ripoti hiyo.
Swali hilo lilijibiwa na Naibu Waziri wa Fedha, Adamu Malima lakini majibu yake yalionekana wazi kutowaridhisha wabunge hao. Malima alisema Oktoba 2000, Serikali iliamua kuipa UDA hisa 3,631,045 kati ya 7,119,697 ambazo ni sawa na asilimia 51, hivyo kubakiza hisa 3,488,651 sawa na asilimia 49 zilizogawiwa na hadi sasa hazijauzwa.
Kwa mujibu wa Malima, UDA ilianzishwa Mei 1974 kwa mtaji wa Sh1.5 bilioni sawa na hisa 15,000,000 kwa bei ya Sh100 kwa kila hisa. Kati ya hizo, hisa 7,119,697 ziligawiwa na kulipiwa, hisa 7,880,303 zilizobaki hazikugawiwa.
Katika swali la nyongeza, Mnyika alihoji kuwa, pamoja na CAG kubaini kuna ufisadi katika kuuza hisa za UDA, iweje hadi sasa umiliki wa kampuni hiyo uko chini ya kampuni ya Simon Group na kwa nini DPP aliondoa kesi ya uuzaji huo mahakamani.
“Ni kwa nini watuhumiwa wameachiwa? Mheshimiwa Spika, haya yasipojibiwa tutaamini kuwa jambo hili linawahusu vigogo wa CCM na mnawalinda katika ufisadi huu,” alisema Mnyika.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Fedha, Adam Malima alikiri kwamba suala la UDA lina mazingira yenye utata mkubwa na kuwa DPP baada ya kubaini utata huo, aliiondoa kesi hiyo na Takukuru na vyombo vingine vya uchunguzi vinaendelea na uchunguzi.
Baadaye, akichangia mjadala wa Wizara ya Katiba na Sheria, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema alisema faili hilo lilirudishwa kwa Takukuru likafanyiwa kazi na jana ndio lilirejeshwa kwa DPP kwa ajili ya uamuzi.
“Ninamshauri DPP wakati anatoa uamuzi asizingatie mambo yaliyojadiliwa bungeni, bali afuate fikra na taratibu za kisheria,” alisema.
Hisa za Serikali
Malima alisema mwenye mamlaka ya kuuza hisa za Serikali hajaziuza na mmiliki halali wa UDA ni Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam lenye hisa asilimia 51 na Serikali asilimia 49.
Alisema mwaka 2006 Serikali iliamua kuuza hisa zake kwa lengo la kupata mwekezaji mahiri na mwenye uwezo wa kuboresha huduma za usafiri Dar es Salaam, lakini haikufanikiwa.
Alisema Januari 2010, Bodi ya UDA iliiarifu Serikali kwamba amepatikana mwekezaji, Simon Group, ambaye angeuziwa hisa za Serikali pamoja na hisa 7,880,303 ambazo hazikugawiwa mwaka 1971.
Baada ya kupokea pendekezo hilo, Serikali iliiagiza Bodi ya UDA kutoendelea na kusitisha mchakato huo, hivyo hisa za Serikali ndani ya UDA bado hazijauzwa na mgawanyo wa hisa unabaki vilevile kwa Halmashauri ya Jiji kumiliki asilimia 51 na Serikali, kupitia Msajili wa Hazina asilimia 49.
Hoja hiyo ilipingwa na Mkurugenzi wa Simon Group, Robert Kisena akisema kampuni yake ilinunua hisa zaidi ya milioni tatu za Jiji kwa kufuata sheria na taratibu zote za ununuzi wa hisa.
“Tunamiliki UDA kwa asilimia 76 na Serikali asilimia 24. Tulinunua hisa hizi kwa taratibu zilizobarikiwa na kamati ya Bunge. Tena tulilipa kwa bei ya juu baada ya kufanyiwa uthamini upya,” alisema Kisena.
Ripoti ya CAG inaonyesha thamani ya hisa hizo wakati zinatolewa ilikuwa ni Sh744.79 kwa kila moja lakini mpaka zinauzwa thamani yake ilishushwa kwa asilimia 60 na kuuzwa kwa Sh298, jambo ambalo baadhi ya wabunge wanalielezea kuwa na mwanya wa rushwa.
Mdee na DPP
Katika mchango wake kwenye mjadala wa Bajeti ya Sheria na Katiba, mbunge wa Kawe, Halima Mdee alimlipua DPP kwa kile alichodai kukumbatia majalada ya rushwa kubwa kwa maslahi yake binafsi.
Ingawa Mdee hakumtaja DPP kwa jina, lakini anayeshikiliwa wadhifa huo kwa sasa ni Eliezer Feleshi na mbunge huyo alitumia fursa hiyo kuhoji kuachiwa kwa mshtakiwa wa kesi ya ufisadi wa Sh2.4 bilioni za UDA.
Mdee alisema DPP amekuwa akilalamikiwa na mkurugenzi mkuu wa Takukuru, Dk Edward Hosea kwamba amekuwa kikwazo katika kushughulikia kesi kubwa za rushwa.
“(Dk Hosea) Akitaka kufungua shauri la rushwa kubwa, mpaka akaombe kibali kwa DPP… analalamika DPP amekuwa akibania vibali vya kufungua kesi kwa maslahi yake binafsi,” aliongeza Mdee.
Mdee alimtaka Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Migiro na AG, Jaji Fredrick Werema kulieleza Bunge ni lini watapeleka bungeni sheria ya Takukuru ya mwaka 2007 ili ifaniywe marekebisho.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa