Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » NHC:MCHECHU NI MKURUGENZI HALALI

NHC:MCHECHU NI MKURUGENZI HALALI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 

SHIRIKA la Nyumba la Taifa (NHC) limesema kuwa, tuhuma zinazotolewa kwa Mkurugenzi Mkuu wa shirika hilo, Nehemia Mchechu kuwa ameundiwa zengwe na bodi ya wakurugenzi ya NHC kwa nia ya kuhakikisha kuwa harejeshwi tena katika wadhifa huo baada ya kumaliza muda wake hazina ukweli wowote.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NHC, David Shambwe aliyasema hayo jana jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na waandishi wa habari.

Alisema, taarifa zilizotolewa na gazeti moja la kila siku (si Majira) zilidai kuwa, Mkurugenzi huyo ameundiwa zengwe na bodi ya wakurugenzi kuhakikisha harejeshwi tena katika wadhifa huo, baada ya kumaliza muda wake.

Pia gazeti hilo lilieleza kuwa, mizengwe hiyo inaungwa mkono na vigogo wa serikali wakiwemo wabunge ambao kuwepo kwa Mchechu katika shirika hilo kumewanyima ulaji ikiwemo kupangishwa nyumba za shirika.

Kaimu huyo alifafanua kuwa katika taarifa hiyo ilieleza pia, Mchechu amewekewa masharti magumu na bodi hiyo ya kumtaka apunguze idadi ya wakurugenzi wa menejimenti ya sasa ya shirika hilo.

Shambwe alisema kuwa, Bodi ya Wakurugenzi ya NHC ina miezi miwili tu, tangu iteuliwe na mamlaka husika na haijawahi kukaa katika kikao chochote kujadili suala la kumuondoa Mkurugenzi Mkuu na kupunguza menejimenti ya shirika iliyopo sasa.

Alisema, Mkurugenzi Mkuu na menejimenti ya shirika bado wana mikataba halali ambayo haijamaliza muda wake, hivyo hoja ya kuwa Mchechu na menejimenti yake wanaundiwa zengwe baada ya kumaliza muda wao haina ukweli wowote.

"Kutokuwepo kwa Mkurugenzi Mkuu kwenye ufunguzi wa miradi hakutokani na kuwepo mizengwe kama ilivyoandikwa na gazeti hilo, kwani alikuwa katika likizo yake ya mwaka iliyoanza Juni 30, mwaka huu hadi Julai 18,"alisema Shambwe.

Aliongeza kuwa, likizo hiyo ilikuwa stahiki halali kama walivyo watumishi wengine wa umma na hakuchukua likizo kutokana na kuwepo mizengwe ya kumuondoa kama ilivyoandikwa na gazeti hilo.

Hata hivyo alisema, NHC itaendelea kuwa mstari wa mbele kutoa habari makini kwa chombo chochote cha habari bila kuficha jambo lolote hivyo ni vyema kuhakikisha habari zinazoandikwa zinakuwa na maelezo kutoka pande zote.

Pia alisema, Watanzania wanatakiwa kufahamu kuwa hakuna mtafaruku wowote uliopo ndani ya shirika na wataendelea kutoa huduma bora katika sekta ya nyumba kama taifa lilivyowaamini. 

Chanzo:Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa