Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » KARIBU SHERIA YA KUZUIA ULAFI WA VIONGOZI

KARIBU SHERIA YA KUZUIA ULAFI WA VIONGOZI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
Tuliwahi kusema katika safu hii kuwa, iwapo Watanzania wangetakiwa kutoa maoni kuhusu taasisi ya umma ambayo wanadhani iliundwa kulinda masilahi ya viongozi badala ya wananchi, bila shaka wengi wangeinyooshea vidole Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi. Taasisi hiyo imekuwapo kwa zaidi ya miongo mitatu sasa na kadiri siku zinavyopita, ndivyo Watanzania wengi wanavyozidi kujiuliza maswali kuhusu nini hasa nafasi ya sekretarieti hiyo katika mfumo wa utawala bora katika nchi yetu.
Maswali ambayo yamekuwa yakiulizwa kuhusu taasisi hiyo yanalenga kuhoji utendaji na ufanisi wa kazi zake tangu ilipoundwa kisheria kwa lengo la kupiga vita ufisadi na kusimamia uadilifu miongoni mwa viongozi wetu kama ilivyofafanuliwa katika Azimio la Arusha. Ni vyema ikumbukwe kwamba sababu za wananchi kuhoji uhalali wa kuwapo chombo hicho ni baada ya viongozi wa umma kujichimbia katika uozo na ufisadi na kutupilia mbali maadili ya uongozi, huku viongozi wa sekretarieti hiyo wakishuhudia pasipo kuchukua hatua. Sekretarieti hiyo imekuwa ikionekana kama kiinimacho, kwani sheria iliyoiunda inaipa nguvu kwa mkono wa kulia na wakati huohuo kuinyang’anya nguvu hizo kwa mkono wa kushoto.
Ni kichekesho kwamba sheria inatoa uhuru kwa kila mtu kwenda katika ofisi za sekretarieti hiyo kulipa ada kabla ya kukagua nyaraka za viongozi waliotangaza mali zao ili kubaini kasoro, ukweli au uongo uliomo.
Lakini sheria hiyo inamkataza mtu yeyote aliyekagua nyaraka hizo kutoa kwa mtu yeyote taarifa kuhusu kitu chochote alichokiona katika nyaraka hizo. Tafsiri pekee ya maelekezo hayo ni kwamba wananchi wanakatazwa kujua mali walizochuma viongozi wao kabla na baada ya kupewa uongozi. Vyombo vya habari ambavyo vinawajibika kuufahamisha umma kuhusu mali walizonazo viongozi wao vimekuwa vikikwazwa na “Sheria ya Maadili ya Viongozi”.
Sheria hiyo ndiyo imewapa kiburi viongozi kiasi cha kukataa kutaja mali wanazomiliki. Pamoja na viongozi wengi kuthibitika kutotangaza mali zao, Sekretarieti hiyo imekuwa kimya siyo tu kwa kuona inasimamia sheria butu, bali pia kwa sababu baadhi ya viongozi wa kitaifa pia wameshindwa au wamekataa kufanya hivyo. Baadhi yao walitaja mali zao wakati wakiingia madarakani, lakini walishindwa au walikataa kufanya hivyo walipomaliza muda wao wa uongozi.
Kwa kuwa huo ndiyo umekuwa utamaduni wa viongozi wetu unaolindwa na sheria, Sekretarieti hiyo miaka yote imekuwa kama “chui wa karatasi” au mbwa asiye na meno. Tumekuwa tukisema kwamba Sekretarieti hiyo pia imechangia hali hiyo kwa kushindwa kuhakikisha kwamba sheria iliyopo inarekebishwa, kwani kwa kukaa kimya imetoa mwanya kwa wananchi kuendelea kuhoji uhalali wake.
Ndiyo maana tumetiwa moyo na hatua ya Sekretarieti hiyo ya kuandaa warsha jijini Dar es Salaam juzi kupokea maoni ya wananchi kuhusu sheria inayotarajiwa kutungwa kudhibiti mgongano wa kimasilahi kwa viongozi na watumishi wa umma. Sheria hiyo imechelewa, lakini italeta uwajibikaji na uzingatiaji wa maadili ya viongozi. Ni matarajio yetu kwamba Sekretarieti itabadilishwa kimuundo ili iwe huru na yenye madaraka kamili ya kufanya uamuzi pasipo kuingiliwa.
Ni matarajio yetu pia kwamba sheria hiyo itaweka misingi na mifumo itakayowezesha kuwapo uwazi katika utendaji wa Sekretarieti hiyo, ikiwa ni pamoja na kudhibiti viongozi wanaotumia vibaya rasilimali na madaraka waliyopewa na umma.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa