Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com
Home » » KAMARI ZA SOKA GUMZO KILA KONA DAR

KAMARI ZA SOKA GUMZO KILA KONA DAR

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
 Ni dhahiri sasa michezo ya kubahatisha hapa nchini imeshika kasi kutokana na ongezeko la vituo vya kamari ya soka maarufu kama ‘kubeti’.
Kamari hizi zilizowateka watu wa jinsi na rika zote, kwa sasa zimeshika kasi huku vituo vya kuchezesha vikichipuka kama uyoga katika maeneo mengi ya Dar es Salaam.
Vituo maarufu ni Premier Betting na Meridian Betting, ambavyo vyote vipo katika ushindani mkubwa wa kuchezesha mchezo na kuvuta watu wengine jijini.
Yachangia bilioni kwa mwaka
Mkurugenzi wa Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania, Abbas Tarimba alisema michezo hiyo imekuwa chanzo kikubwa cha mapato kwenye bodi hiyo na kuongeza mzunguko wa fedha unaozidi Sh2 bilioni kwa mwezi.
Alisema michezo hiyo ya kubahatisha inafanya vizuri, kwani mapato yake kwa bodi hiyo hufikia Sh1.4 bilioni kwa mwaka.
Alisema wamiliki wa vituo vya kamari hizo ni lazima wafuate kanuni zilizoainishiwa na bodi ya michezo ya kubahatisha nchini.
Tarimba alisema matatizo kadhaa yanayojitokeza kwenye michezo hiyo ni pamoja na malalamiko ya kutotendewa haki kwa wachezaji.
Wasemavyo wachezaji
Mfanyabiashara wa genge, eneo la Tabata, Mawenzi, Yohana Ibrahim alisema ameanza kucheza kamari hiyo mwaka huu na ameshashinda mara nyingi.
“Nimeshawahi kushinda Sh200,000 mara mbili, nimeshinda 70,000, 50,000 na hizi Sh10,000 ndiyo mara nyingi,” alisema.
Ibrahimu ambaye mara nyingi ‘hubeti’ kwenye kampuni ya Meridian, alisema ingawa anakosa mara moja moja, lakini mara nyingine amekuwa akishinda na kujipatia fedha ambazo huziingiza kwenye biashara yake ya genge
Kijana anayejishughulisha na kazi ya kusafisha kucha na kupaka rangi katika kituo cha Mwenge Joseph Lutumo (25), anasema kazi yake inamwingizia kiasi cha Sh60,000 kwa siku, lakini katika kiasi hicho lazima ahakikishe Sh3,000 anazitumia kucheza mchezo huo wa kubahatisha.
“Nina mwaka mmoja sasa nacheza betting, kabla hata mchezo huu haujachukua umaarufu nilikuwa naucheza. Nimewahi kushinda mara nne na wakati wote nilikuwa nashinda fedha za kawaida,” alisema Lutumo na kuongeza:
“Awali, nilishinda Sh100,000 baada ya kutumia Sh2,000, nikacheza kwa kupoteza sana na kushinda Sh50,000, ikapita miezi sita nikashinda tena na mara ya mwisho nilicheza pale Meridian nikashinda Sh5 milioni nikaenda kununua kiwanja Mkuranga. Zaidi ya miezi mitatu sasa sijashinda na bado nacheza, nina imani ipo siku nitapasua.”
Muuza mitumba Ally Ramadhani (32) na mfanyabiashara wa Mwenge, alisema kwa miaka mingi sasa anashiriki mchezo huyo. “Nacheza betting nina muda ila sijawahi kushinda. Sichezi kila siku ila ninapojisia,” Alipoulizwa iwapo anahisi kwamba mchezo huyo unamfilisi alisema: “Sichezi hela nyingi mara nyingi ni ile fedha ya ziada.”
Jinsi unavyochezwa
Wakala wa bahati nasibu ya Premier, iliyopo Msasani kwa Mgosi, Albert Franchesco alieleza jinsi kamari hiyo inavyochezwa na kuwa kushinda kunahusisha bahati na kuijua soka, wachezaji na timu zao.
“Ili kushiriki, mchezaji lazima uchukue ratiba ya timu zote. Huu ni kama mtihani wenye maswali. Maswali hayo huwa na namba ambazo kwenye kamari ni kama ‘code’.
“Kwa kawaida kila timu ina ‘code’ yake, unachotakiwa kufanya ni kuangalia pointi za timu kisha unazijumlisha pointi hizo pamoja na kiasi cha fedha unachoweka.
“Baada ya kuchagua timu zako, unapeleka karatasi yako kwa wakala ambayo huchapishwa na kutolewa kitu kinachoitwa ‘mkeka’. Baada ya kupata mkeka, unasubiri timu hizo zicheze na baada ya hapo timu zako zote ulizochagua zikishinda basi utajipatia fedha ambazo ni jumla ya kiasi cha fedha na idadi ya pointi za timu ulizochagua.
Washinda Sh2 bilioni Dar
Meneja Uendeshaji wa Premier Betting, Javier Diaz Del Rio ambayo huchezesha michezo huo hususan kwa ligi za Ulaya kama ligi ya kuu za England, Hispania, Ujerumani na Ufaransa, alisema kampuni hiyo hutoa zawadi hadi Sh2 bilioni kwa mwezi akitolea mfano Februari mwaka huu kuwa ilitoa Sh2.1 bilioni za zawadi kwa wateja wake.
“Fedha zetu huwa tunatoa papo kwa papo, mteja anaweza kuchukua kwa wakala wetu kama ni kiasi kidogo au kwenye matawi yetu mengine kama ni kiasi cha kati ila kwa kiasi kikubwa wanakuja kuchukua makao makuu.
Moja ya washindi wa mchezo huo wiki hii katika mechi ya mabingwa wa Ulaya, Fredy Auleliani alisema: “Mchezo huu ni wa haki kutokana na ulivyopangwa tofauti na michezo mingine ya bahati nasibu, kwani hapa unapewa risiti na kusubiri dakika 90 za mechi kuisha na siku inayofuata asubuhi unachukua pesa yako, ndiyo maana ukipita hapa asubuhi lazima ukute watu walioshinda wana furaha kama nini.”
Baadhi ya watu siku hizi wanategemea mchezo huu kula na wengine wanalisha familia kwa ‘kubet’, kwani huweka fedha nyingi na kushinda kiwango cha juu.
Mmoja wa washindi mwishoni mwa wiki alisema: “Mimi nimeweka timu zangu tano tu nikaweka Sh1,000 na nimeshinda Sh165,000. Ninachofuata ni alama za timu kubwa, kufuatilia timu zilizopo kwenye mkeka na kusubiri. Siku hizi najua timu zinazofanya vizuri tofauti na timu kubwa. Mimi ni shabiki wa Manchester United, lakini siku ikicheza na timu, ambayo sina uhakika kama tunaweza tukashinda siwezi kuipa alama ya kushinda.” japo kuwa ni timu yangu lakini tunangalia pesa kwanza,” alisema Bosco Mapunda mkazi wa Chang’ombe, Temeke.
Mchezaji mwingine aneyemiliki kibanda cha kubet alisema: “Watu wengi wanashinda na wengine wanakosa kutokana na kupata timu wanazoona zitashinda,” alisema kijana huyo aliyerjitambulisha kwa jina la Deo.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa