Na Jacquiline Mrisho - MAELEZO
Wakala
wa Barabara Tanzania (TANROADS) wamekanusha kudaiwa fidia na wananchi
wa Kijiji cha Mazingira,Wilaya ya Handeni mkoani Tanga waliovunjiwa
nyumba zao ili kupisha ujenzi wa barabara.
Kauli
hiyo imetolewa leo Jijini Dar es Salaam na Meneja wa TANROADS Mhandisi
Alfred Ndumbaro alipokuwa akiongea na mwandishi wa habari hii juu ya
malalamiko ya wananchi wa Kijiji hicho kuhusu kutolipwa fidia zao.
”Sheria
iko wazi kuwa wanaojenga karibu na barabara wakivunjiwa hawalipwi fidia
yoyote lakini wale ambao ujenzi wa barabara uliwafuata katika maeneo
yao wana haki ya kulipwa fidia”, alisema Mhandisi Ndumbaro.
Mhandisi
Ndumbaro ameongeza kuwa zoezi la malipo ya fidia kwa wanakijiji
waliokuwa na uhalali wa malipo hayo lilishakwisha zamani kwa hiyo,
wanaodai sasa ni wale ambao nyumba zao zilivunjwa kutokana na kujenga
eneo la barabara.
Aidha,
Mhandisi huyo ametoa rai kwa wananchi kufuata sheria za ardhi ili
kupata uhalali wa viwanja vyao pamoja na kuepuka usumbufu na gharama za
kuvunjiwa nyumba zao.
Nyumba
hizo zilivunjwa ili kupisha ujenzi wa barabara ya lami yenye Kilomita
54 kutoka Mkata hadi Handeni iliyojengwa na Kampuni ya Synohydro
Corporation Limited ya China.

0 comments:
Post a Comment