Na Benny Mwaipaja-WFM, Dar
es salaam
BENKI ya Maendeleo ya
Afrika-AfDB, imeipatia Tanzania mkopo wenye masharti nafuu wa dola Milioni 164,
karibu Shilingi Bilioni 360, kwaajili ya kuchangia Bajeti kuu ya Serikali
katika kipindi cha Mwaka wa Fedha 2016/2017 pamoja na kuongeza mtaji wa Benki
ya Maendeleo ya Kilimo nchini-TADB.
Mikataba miwili imesainiwa
leo Jijini Dar es salaam kati ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw.
Doto James kwa niaba ya Serikali na Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika
anayeondoka Dkt. Tonia Kandielo.
Mkataba wa kwanza
uliosainiwa ni kwa ajili ya kutunisha Mfuko Mkuu wa Serikali ambapo Benki hiyo
imetoa dola za kimarekani milioni 70 sawa na tsh 154 bilioni ambazo
zitaelekezwa kuongeza ufanisi wa utendaji kazi wa Shirika la Ugavi wa Umeme
nchini-TANESCO.
Mkataba wa pili ni
kwaajili ya kuongezea mtaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo nchini-TADB wenye
thamani ya dola Milioni 94 sawa na shilingi Bilioni 204 kwa ajili ya kuiongezea
uwezo Benki hiyo kutoa mikopo yenye riba nafuu kwa wakulima ili kuongeza
mnyonyoro wa thamani kuanzia uzalishaji, uongezaji thamani na upatikanaji wa
masoko ya uhakika ya mazao ya wakulima.
Uhai wa mikopo
yote miwili utakuwa ni miaka 40 ambapo serikali itaanza kuilipa baada ya miaka
kumi tangu kutolewa kwake, huku riba yake ikiwa chini ya asilimia 1.
Akizungumza baada
ya kusainiwa kwa mkopo huo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Doto
James, amesema mkopo huo umekuja wakati muafaka na utasaidia kukuza na kuimarisha
TANESCO na kuendeleza kilimo nchini.
“Tanzania ni nchi iliyonufaika
zaidi na mikopo yenye masharti nafuu kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika-AFDB
ikilinganishwa na nchi nyingine yoyote iliyoko katika Ukanda wa Kusini mwa Afrika” Alisema Bw.
James.
Kwa upande wake,
Mwakilishi Mkazi wa AFDB anayeondoka Dkt. Tonia Kandielo amesema kuwa hadi sasa
Benki yake imeipatia Tanzania mkopo wenye thamani ya zaidi ya dola za Marekani
bilioni 2, ambazo zimewekezwa kwenye miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa
miundombinu ya barabara, maji, nishati ya umeme, elimu na kilimo.
“Ninaamini kuwa
hatua ya kuongeza mtaji katika Benki ya Maendeleo ya Kilimo-TADB itachochea
maendeleo ya kilimo nchini, na tunaahidi kuwa tutaendelea kuiwezesha zaidi siku
zijazo” Alisema Dkt. Kandielo.
Kuhusu Sekta ya Nishati,
Dkt. Kandielo amesema kuwa Benki yake imeona umuhimu wa kuliwezesha shirika
hilo ili liweze kutoa huduma kwa ufanisi zaidi ili kuchochea uchumi wa Taifa.
“Mikopo hii
inahusiana na vipaumbele tulivyoviweka kama Benki ambavyo viko katika malengo
matano ambapo
tunataka kuwekeza katika sekta ya nishati, uzalishaji wa chakula, kuendeleza viwanda,
kuiunganisha Afrika na kuboresha maisha ya waafrika kwa ujumla" aliongeza
Dkt. Kandielo
Wakati huo huo, Waziri wa
Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, amemuaga rasmi Dkt. Tonio Kandielo ambaye
amehamishiwa nchini Afrika Kusini kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Benki hiyo atakaye
simamia Kanda ya Kusini mwa Afrika.
Dkt. Mpango, amesifu
jitihada kubwa zilizofanywa na mwana mama huyo katika kipindi cha miaka 6
aliyokuwepo hapa nchini ambapo ameweza kusimamia vizuri maslahi ya Tanzania
katika Benki hiyo.
Amesema kuwa katika
kipindi hicho Tanzania imeshuhudia maendeleo makubwa katika sekta za ujenzi wa
miundombinu ya barabara, kilimo, maji na umeme, ambapo benki hiyo ilihakikisha
kuwa miradi inatekelezwa kwa viwango vinavyotakiwa.
Amemwomba Mkurugenzi Mkuu
huyo kuwezesha upatikanaji wa fedha kwaajili ya ujenzi wa Reli ya Kati kwa
kiwango cha kimataifa (Standard gauge) inayohitaji fedha nyingi, kusimamia utekelezaji wa mradi wa umeme wa
kikanda unaoanzia nchini Zambia, uboreshaji wa Bandari ya Itungi na Mbambabay.
Akijibu hoja za Waziri wa
Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, Dkt. Tonia Kandielo amesema kuwa anaamini
mrithi wake ataendeleza mazuri aliyoyafanya na kwamba yeye binafsi atahakikisha
anafuatilia kwa karibu miradi ambayo mikataba yake imesainiwa katika nyanja za
maboresho ya sekta ya umeme na kilimo.

0 comments:
Post a Comment