SERIKALI YAHAIDI KUTOA
USHIRIKIANO WA KUTOSHA KWA UONGOZI MPYA WA TUCTA.
Na Daudi Manongi-MAELEZO
Waziri wa Nchi Ofisi ya
Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na watu wenye ulemavu, Jenister Mhagama
amesema Serikali itaendelea kutoa ushirikiano wa kutosha kwa viongozi wa Shirikisho
la Vyama vya Wafanyakazi Nchini (TUCTA) ili kuleta tija na ufanisi katika sekta
ya kazi.
Waziri Mhagama aliyasema
hayo leo Jijini Dar es Salaam wakati wa mkutano wake na Viongozi hao wa TUCTA
waliofika ofisini kwake kwa ajili ya kujitambulisha mara baada ya kumalizika
kwa uchaguzi wa shirikisho hilo.
“Tumefarijika sana kwa
TUCTA kupata uongozi mpya ambao tuna uhakika wanachama wamezingatia masuala muhimu katika uchaguzi wao ikiwemo weledi na kutazama
dira ya sekta ya wafanyakazi nchini”.
Aidha aliongeza kuwa Viongozi
hao wana jukumu kubwa la kuleta tija na maendeleo chanya katika sekta ya kazi
nchini na kuhimiza kuwa wafanyakazi ni rasilimali muhimu katika kuleta maendeleo
ya nchi.
Kwa mujibu wa Mhagama
ameahidi Viongozi hao kufanya kikao kazi mapema iwezekanavyo kwani uchaguzi umekwisha
na sasa kilichobaki ni kufanya kazi.
Pia amesisitiza ushirikiano
wa kudumu kati ya Serikali, Waajiri na wafanyakazi ambao utasaidia kwa kiasi kikubwa
kutatua migogoro iliyopo.
Kwa upande wake Rais wa
TUCTA, Tumaini Nyamghokya alimshukuru Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kwa kusimamia
utu wa mtumishi kwa kuhaidi kuwalinda kutokana na baadhi ya viongozi kutoa lugha
zisizosahihi.
Aidha, ameishukuru Serikali
kwa kuwa karibu nao kwa muda wote na kuhaidi kuendeleza ushirikiano huo ili kuleta
tija katika kazi.
MWISHO
0 comments:
Post a Comment