Home » » NEC YATOA UFAFANUZI WA MALALAMIKO YA CHAMA CHA ACT-WAZALENDO

NEC YATOA UFAFANUZI WA MALALAMIKO YA CHAMA CHA ACT-WAZALENDO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 


Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imekishauri Chama cha ACT – Wazalendo na Vyama vingine vyenye wagombea wa Ubunge katika Uchaguzi Mdogo wa Jimbo la Dimani na Udiwani katika Kata Ishirini (20) za Tanzania Bara kuwasilisha malalamiko yao ya ukiukwaji wa Maadili ya Uchaguzi kwenye Kamati za Maadili ngazi ya Kata na Jimbo zilizo katika maeneo yao.
Akizungumza na Vyombo vya Habari leo jijini Dar es salaam, Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Bw. Kailima Ramadhan amesema kuwa NEC imepata taarifa kupitia Vyombo mbalimbali juu ya malalamiko ya Chama Cha ACT-Wazalendo kuvilalamikia Vyombo vya Dola pamoja na Watendaji wa Umma kufanya vitendo vyenye muelekeo wa kukipendelea Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Bw. Kailima amesema kuwa taarifa ya Chama hicho iliyotolewa kwenye Vyombo vya Habari Januari, 12 2017, imeeleza kuwa Watendaji wa Halmashauri ya Geita waliwakusanya Wazee katika Kata ya Nkoma waje na Vitambulisho vyao vya kupigia Kura kwa lengo la kuwapatia huduma ya afya bure jambo linalolalamikiwa na ACT- Wazalendo kuwa Watendaji hao wana lengo la kuwahadaa Wazee hao ili wakipigie Kura Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Amefafanua kuwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa  kuzingatia sehemu ya 5.4 ya Maadili ya Uchaguzi inavikumbusha Vyama vya Siasa kuwa iwapo vitakuwa na malalamiko ya ukiukwaji wa Maadili ya Uchaguzi katika Uchaguzi Mdogo wa Udiwani viwasilishe malalamiko hayo kwenye Kamati ya Maadili ngazi ya Kata ndani ya saa 72 tangu kutokea kwa tukio linalolalamikiwa.
“ Sehemu ya 5.4 ya Maadili ya Uchaguzi inaeleza wazi muda wa kuwasilisha malalamiko kwa kuvitaka vyama au wahusika wenye malalamiko yoyote  kuyawasilisha kwa maandishi kwenye Kamati ya Maadili ya Uchaguzi ya ngazi husika ndani ya saa 72 tangu kutokea kwa tukio” Amesisitiza Kailima.
Tume inapenda kuvikumbusha vyama vya Siasa kwamba, kwa mujibu wa sehemu ya 5.3 ya Maadili ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani ya mwaka 2015 ambayo yalisainiwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Serikali na Vyama Vya Siasa, Chama cha Siasa au mgombea wa nafasi husika anayeamini kwamba Maadili ya Uchaguzi yamekiukwa awasilishe malalamiko yake katika Kamati ya Maadili ya  ngazi husika.
Hivyo, tunakishauri Chama cha ACT – Wazalendo na Vyama vingine vyenye wagombea wa Ubunge katika Uchaguzi Mdogo wa Jimbo la Dimani na vyenye Wagombea wa Udiwani katika Uchaguzi mdogo kwenye Kata Ishirini (20) za Tanzania Bara kutumia haki yao kuwasilisha malalamiko ya ukiukwaji wa Maadili katika Kamati husika.
Kwa kuzingatia sehemu ya 5.4 ya Maadili ya Uchaguzi, Tume inavikumbusha Vyama vya Siasa kuwa, iwapo wana malalamiko ya ukiukwaji wa Maadili ya Uchaguzi katika Uchaguzi Mdogo wa Udiwani kuwasilisha lalamiko hayo kwenye Kamati ya Maadili ngazi ya Kata saa 72 tangu ukiukwaji huo wa maadili umefanyika.
Iwapo Chama cha Siasa au Mgombea hataridhika na maamuzi ya Kamati ya Maadili ngazi ya Kata, kwa kuzingatia sehemu ya 5.7 (a) ya Maadili ya Uchaguzi awasilishe rufaa kwa Msimamzi wa Uchaguzi ngazi ya Jimbo ndani ya saa 24 tangu maamuzi ya Kamati ya Maadili ngazi ya kata kutolewa.
Aidha, kama Chama cha Siasa hakikuridhika na maamuzi ya Kamati ya Maadili ngazi ya Jimbo, bado kwa kuzingatia sehemu ya 5.7 (b) na (c) wanayo fursa ya kuwasilisha Rufaa yao katika Kamati ya Maadili ngazi ya Taifa au ngazi ya Rufaa ambazo ni Tume ya Taifa ya Uchaguzi.
Tunavishauri Vyama vya Siasa na Wagombea kuzingatia matakwa ya Maadili ya Uchaguzi katika kuwasilisha malalamiko yao ya ukiukwaji wa maadili ya Uchaguzi.
Kwa mujibu wa sehemu ya 5.7(e) ya Maadili ya Uchaguzi, pale ambapo Chama cha Siasa au Mgombea hakuridhika na maamuzi ya Kamati ya Rufaa atakuwa na fursa ya kuwasilisha malamiko hayo ya ukiukwaji wa maadili  Mahakamani baada ya Uchaguzi kwa mujibu wa Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura ya 343 na Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa, Sura ya 292.
Aidha, katika maelezo yao ACT Wazalendo wameeleza tuhuma za wananchi kupokwa kadi zao za kupigia Kura. Nitoe wito kwa wananchi wote kwamba, ni kosa chini ya kifungu cha 88 cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura ya 343 na kifungu cha 100 cha Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa, Sura ya 292 kumiliki kadi ya kupigia kura isiyokuwa yako. Na wananchi wasikubali kumpatia mtu yeyote kadi yao ya kupigia kura isipokuwa kuionesha kwenye kituo cha kupigia kura siku ya kupiga kura tarehe 22 Januari, 2017.
Mwisho, Tume ya Taifa ya Uchaguzi inaendelea kuwasihi viongozi wa Vyama vya Siasa na Wadau wengine wa Uchaguzi kuendelea na Kampeni za kistaarabu na kuzingatia Sheria, Kanuni na Maadili ya Uchaguzi.  Tume inaendelea kufuatilia kwa karibu katika kila hatua ya Uchaguzi na hasa Kampeni.  Haitasita kuchukua hatua kwa mtu yeyote atakayekiuka Sheria za Uchaguzi.


 


0 comments:

 
Supported byBlogs za Mikoa
Copyright © 2012. Dar es salaam Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa